Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Jacqueline Kandidus Ngonyani (Msongozi) (1 total)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali imeweka mkazo mkubwa katika kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini Tanzania, licha ya jitihada hizo kuna baadhi ya Maafisa wanakwamisha wawekezaji. Je, Serikali inatoa kauli gani kwa Watendaji wa aina hii?

Mheshimiwa Spika, ahsante.

SPIKA: Unaweza ukajaribu kutoa hata kamfano kidogo Mheshimiwa Jacqueline, maana yupo Waziri wa Uwekezaji naye ajifunze ni ukwamishaji gani unaotokea?

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wawekezaji wanapokuja nchini unakuta labda kwa mfano anakwenda katika Mkoa wa Mwanza anataka aweke kiwanda cha usindikaji wa samaki lakini unakuta kwenye, labda Sekta ya Ardhi au kwenye Halmashauri zetu katika sekta mbalimbali wanakuwa wanaweka vikwazo mbalimbali labda kutengeneza mazingira labda ya rushwa na mambo kadha wa kadha. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Msongozi, Mbunge kutoka Mkoa wa Ruvuma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu kwa sasa tumeweka utaratibu mzuri sana wa uwekezaji na tunaendelea kuhamasisha uwekezaji nchini wa ndani na nje ya nchi. Natambua kwamba tulipoanza kutoa wito wa uwekezaji kwa yeyote mwenye nia ya kuwekeza hapa nchini tulianza katika mapito mbalimbali, watendaji, wengine walikuwa hawajajua philosophy ya Serikali, lakini pia maeneo muhimu ya uwekezaji bado ilikuwa hayajachanganuliwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imeweka utaratibu mzuri sana, kwanza kwa kuunda Wizara ya Uwekezaji ambayo sasa itashikilia Sera ya Uwekezaji kwa ujumla, pia Serikali ina chombo kinachoshughulikia uwekezaji, Taasisi ya Uwekezaji Tanzania (TIC) ambayo sasa tumerahisisha mambo yote ya uwekezaji yako hapo ndani, anayetaka ardhi anapata huko ndani, anayetaka huduma za TRA anakuta huko ndani, usajili wa kampuni anakuta huko. Sekta zote zinazogusa uwekezaji sasa zinapatikana pale TIC kwa maana tumeanzisha One Stop Center ambayo kila mwekezaji anapokuja shughuli zote zinaishia hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tumeleta mamlaka kwenye ngazi za Mikoa na Halmashauri kupokea Wawekezaji wenye nia ya kuwekeza kwenye ngazi hizo na Mikoa sasa itawezesha kuhakikisha kwamba mwekezaji huyo anapata huduma ya uwekezaji na atapata maelekezo sahihi. Yako mambo yanawezeshwa hukohuko kwenye ngazi ya Halmashauri au ngazi ya Mkoa lakini mengine lazima yaende TIC na mengine lazima yaende Wizarani kukutana na Waziri kwa ajili ya Sera ya ujumla.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa utaratibu huu kama bado kuna mtendaji anakwamisha uwekezaji huyu atakuwa hana nia njema na nchi yetu. Na popote ambako wananchi, Waheshimiwa Wabunge unaona kuna Mtendaji wa Serikali tumempa jukumu la kusimamia shughuli za Serikali ikiwemo na uwekezaji, uwekezajia ambao sasa kila siku tunatoa wito watu wawekeze, tena wawekezaji wa ndani na wa nje ya nchi na anakwamisha process hiyo hatua kali dhidi yake zitachukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, bado Serikali inatoa wito wa uwekezaji. Tumerahisisha uwekezaji kwa sababu pia tumekuwa na vikao na makundi mbalimbali ya wafanyabiashara, wawekezaji. Mheshimiwa Rais amekutana na wafanyabiashara wengi, wawekezaji wengi na sisi watendaji huku chini tumekutana na makundi hayo mbalimbali tukapata kero zinazowagusa hao wafanyabiashara.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tumeandaa mfumo tumetengeneza ile blueprint kile kitabu ambacho kinaonesha mabadiliko ya mifumo mbalimbali ya uwekezaji ambayo yanarahisisha uwekezaji hapa nchini kuwa uwekezaji rahisi zaidi. Ndiyo kwa sababu sasa unaona idadi ya wawekezaji nchini inaongezeka na tunaendelea kupokea kero za wawekezaji ili tuendelee kuboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kutoa wito kwa wawekezaji wote wasihofu kuja nchini tuna ardhi, tunazo maliasili lakini tuna rasilimali za kuendeshea kilimo uwekezaji huo kama ni viwanda au tukitaka kuchakata madini, tunayo. Muhimu zaidi ni kufuata sheria, kanuni na utaratibu wa ndani ya nchi ili uweze kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba tumesikia, tumepata ujumbe wako ndani ya Serikali tutaendelea kusimamia vizuri kwa watendaji ambao hawaelewi bado philosophy ya Serikali na malengo ya nchi kwa ajili ya kuleta uwekezaji ulio sahihi na bora. Mazingira ya uwekezaji kwa sasa tumerahisisha na tutaendelea kurahisisha zaidi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)