Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Naghenjwa Livingstone Kaboyoka (34 total)

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Bwawa la Kalemawe lilijengwa mwaka 1959 na kumekuwepo na makubaliano baina ya Serikali, UNCDF na wadau wengine juu ya ukarabati wa Bwawa hili.
Je, kazi ya ukarabati itaaza lini ili Wafugaji na Wakulima waondokane na shida ya uchakavu wa bwawa hilo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimwa Spika, ni kweli bwawa la Kalemawe lilijengwa mwaka 1959, lengo la ujenzi wa bwawa hilo lilikuwa ni kwa ajili ya utunzaji wa maji ya kunywa, mifugo na kilimo cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Same ina mpango wa kukarabati bwawa la Kalemawe kwa kuondoa udongo ambao umejaa kwenye bwawa hilo ili kuongeza ujazo wa ukubwa wa maji kwa ajili ya mifugo na kilimo cha umwagiliaji kwa kutumia fedha kutoka Mfuko wa Kimataifa wa United Nations Capital Development Fund.
Mheshimiwa Spika, sambamba na ukarabati wa bwawa hilo, scheme ya Kalamba yenye jumla ya hekta 350 pia itakarabatiwa kupitia mpango huo. Maji ya umwagiliaji ya scheme ya Kalamba yatatoka katika bwawa la Kalemawe. Kazi inayoendelea hivi sasa ni ya kumpata Mtaalam Mshauri (Consultant) ili aweze kufanya kazi ya usanifu na kujua gharama za ukarabati. Pindi mtaalam mshauri atakapokamilisha kazi yake kazi ya kumpata Mkandarasi kwa ajili ya ukarabati wa bwawa na scheme itaanza.
MHE. SUSAN A. J. LYIMO (K.n.y MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA) aliuliza:-
Kumekuwepo na ahadi nyingi wakati wa kampeni kutoka kwa Marais wa Awamu ya Nne na ya Tano kuwa barabara ya kutoka Mkomazi kupitia Bendera, Kihurio, Ndungu, Maore, Kisiwani hadi Same Mjini itajengwa kwa kiwango cha Lami.
Je, Serikali inatoa tamko gani kuhusu ahadi hizo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, barabara ya Mkomazi - Kihurio - Ndungu – Kisiwani hadi Same ni barabara ya mkoa yenye urefu wa kilometa 96 inayohudumiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS). Ili kuhakikisha kwamba barabara hii inapitika katika majira yote ya mwaka, Serikali imeendelea kutenga fedha za kufanyia matengenezo ya aina mbalimbali. Aidha, julma ya kilometa 19.2 zimekamilika kujengwa kwa kiwango cha lami katika maeneo yenye watu wengi ya Kisiwani, Gonja, Maore na Ndungu.
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza ahadi za Serikali kuhusu barabara hii, Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara (TANROADS) imepanga kufanya usanifu wa kina kuanzia Same- Kisiwani- Gonja- Bendera hadi Mkomazi ambapo ni kilometa 96 katika mwaka wa fedha 2016/2017 ikiwa ni maandalizi ya kujenga barabara yote kwa kiwango cha lami kama viongozi wetu wakuu walivyokuwa wameahidi. Mara usanifu wa kina utakapokamilika Serikali itatafuta fedha ili kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami.
MHE. RASHID A. SHANGAZI (k.n.y MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA)aliuliza:-
Wakulima wa zao la tangawizi katika Jimbo la Same Mashariki wanahamasishwa kulima tangawizi kwa wingi kwa matarajio kuwa Kiwanda cha Tangawizi kilichokuwa kinatarajiwa kufanya kazi kingeweza kusaga tangawizi hiyo kwa kiasi cha tani tisa kwa siku; na kwa vile kiwanda hicho hakijaweza kufanya kazi tangu kifunguliwe na aliyekuwa Rais wa wakati huo Mheshimiwa Jakaya Kikwete, tarehe 29 Oktoba, 2012 huko Mamba Miyamba, Wilayani Same Mashariki:-
Je, Serikali inawasaidiaje wakulima hao kupata soko la zao hilo ambalo imeshindikana kuliongezea thamani, processing na matokeo yake wanunuzi ni wachache na wanawapunja sana wakulima wanaponunua zao hilo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Same inaongoza kwa uzalishaji wa tangawizi hapa nchini. Hivyo ushirika wa wakulima wa tangawizi wa kata ya Mamba Miamba uliamua kujenga kiwanda ili kuongeza thamani ya zao hilo.
Baada ya kiwanda hicho kuzinduliwa, kiliweza kusindika zaidi ya tani 100, kabla ya baadhi ya mitambo yake kupata hitilafu na kusitisha usindikaji. Shirika la SIDO lilijulishwa kuhusiana na hitilafu hizo kwa kuwa ndilo lililosanifu na kutengeneza mitambo hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumjulisha Mheshimiwa Mbunge kuwa taarifa nilizopata kutoka kwa Ofisi ya RAS wa Mkoa wa Kilimanjaro ni kwamba tayari SIDO wamekamilisha matengenezo hayo na kinachosubiriwa ni taratibu za makabidhiano.
Mheshimiwa Naibu Spika, soko la tangawizi iliyosindikwa lipo la kutosha ndani na nje ya nchi. Serikali kupitia mradi wa uboreshaji miundombinu ya masoko na uongezaji thamani yaani Marketing, Infrastructure, Value Addition and Rural Financing, kwa kushirikiana na shirika la Faida Mali inaendelea kusaidia ushirika huo kutafuta na kuwaunganisha na masoko ya uhakika, tayari masoko yafuatayo yameishapatikana ambayo ni Kampuni ya Afri Tea ya Dar es Salaam, Kampuni ya Tausi ya Arusha na Kampuni ya Lion Wattle ya Lushoto. Wanunuzi hao wapo tayari kununua tangawizi, iliyosindikwa, mara tu kiwanda kitakapoanza tena kufanya kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Ushirika wa Wakulima wa Tangawizi wa Mamba Miamba, unakabiliwa pia na changamoto nyingine kama vile za uelewa mdogo wa usimamizi na uendeshaji wa kiwanda, ukosefu wa mtaji wa kutosha kwa ajili ya kununua malighafi na gharama za uendeshaji. Changamoto hizo zinapelekea kiwanda kutofanya kazi vizuri. Katika kutatua changamoto hizo, Serikali kupitia wataalam wake wa ushirika na mradi wa MIVARF inaendelea kutoa elimu ya uendeshaji na usimamizi ili hatimaye waweze kuunganishwa na vyombo vya fedha, ili waweze kukopesheka kwa ajili ya kupata mtaji na kuendesha kiwanda kwa faida ya ushirika.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Kituo cha Utafiti wa Malaria kilichopo Kata ya Vuje, Tarafa ya Gonja, Jimbo la Same Mashariki kimejengwa miaka ya 1960 na kina majengo ya kisasa kumi na kwamba Serikali ilikifanyia ukarabati mkubwa mwaka 2007, lakini mpaka sasa hakifanyi kazi badala yake kimegeuzwa kuwa nyumba za kulala wageni na pesa zinaingia mfukoni mwa watu.
Je, Serikali inafahamu jambo hilo na kama inafahamu inatoa kauli gani?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu na Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki kuwa ni kweli Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) inamiliki maabara, jengo la utawala na nyumba ya wageni (rest house) katika kituo chake cha Gonja Maore, Wilayani Same. Kulingana na jiografia ya Gonja, rest house hiyo ilijengwa kwa madhumuni ya kufikia wafanyakazi wa taasisi kutoka vituo vyake vingine wanaokwenda pale Gonja katika maeneo hayo kwa malengo ya kikazi.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa rest house, licha ya kuhudumia wafanyakazi wa taasisi pia inatoa huduma kwa wananchi ikiwa pia ni mojawapo ya vyanzo vya mapato kwa taasisi. Taasisi imeweka taratibu na miongozo mahsusi inayoongoza utoaji wa huduma katika rest house zake zote ikiwemo ile ya Gonja, katika utaratibu huo wageni wote wanaohitaji huduma katika rest house huwajibika kujisajili katika register ya wageni ya rest house na stakabadhi hutolewa kwa malipo yoyote yatakayofanyika. Hivyo, majengo yote ya kituo yanatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Kumekuwa na mgogoro kati ya wafugaji na wakulima wa Jimbo la Same
Mashariki dhidi ya TANAPA:-
(a) Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwapatia wafugaji hao shamba
darasa kupitia hekta 346,000 zinazofaa kwa ufugaji?
(b) Ili kutatua tatizo la maji na malisho kwa wafugaji wa Same
Mashariki: Je, Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi haioni umuhimu wa
kuanzisha mradi wa kuvuna maji ya mvua ambazo hunyesha mara kwa mara?
(c) Je, Waziri yuko yatari kuambatana na wataalam wake
kutembelea Jimbo la Same Mashariki ili kuona ni jinsi gani anaweza kuwasaidia
wafugaji kuanzisha mitambo ya Biogas kwenye mazizi yao pamoja na
kuwaelimisha matumizi bora ya mbolea ya samadi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa KIlimo, Mifugo na Uvuvi,
napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge
wa Same Mashariki, lenye sehemu (a) (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Shamba darasa la unenepeshaji mifugo limeanzishwa katika Kijiji
cha Ruvu mferejini, Kata ya Ruvu kati ya hekta 2,754 zimepimwa kutokana na
hekta 346,000 zilizoainishwa na vijiji mbalimbali katika Wilaya kwa ajili ya ufugaji.
Uainishaji wa maeneo umefanyika katika Kata zote zinazopakana na mbuga za
Mkomazi na upimaji utafanyika kulingana na upatikananji wa fedha.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaona umuhimu wa kuvuna maji
ya mvua ili kutatua tatizo la maji kwa mifugo katika Jimbo la Same Mashariki;
ambapo kwa kushirikiana na taasisi binafsi ya Women and Youth Empowerment,
Enviro Care and Gender Trust Fund (WOYOGE) na TANAPA, imewezesha ujenzi
wa birika la maji katika Kijiji cha Muheza katika Kata ya Maole na maji yanaingia
katika birika hilo kutokana na chanzo cha maji kutoka Milima ya Mbaga. Aidha,
uvunaji wa maji ya mvua unatarajiwa kutekelezwa kwa ufadhili wa Shirika la
United Nations Capital Development Fund (UNCDF) kwa kukarabati bwawa
katika Kata ya Kalemawe kwa matumizi ya maji kwa kilimo, mifugo, uoteshaji wa
miti na ufugaji wa samaki ambao utasaidia upatikanaji wa maji kwa kipindi cha
mwaka mzima utakapokuwa umetekelezwa.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia CAMARTEC ikishirikiana na
sekta binafsi ya Tanzania Domestic Biogas Program imeendelea kutoa elimu kwa
jamii juu ya matumizi ya biogas katika Jimbo la Same Mashariki ambapo jumla ya
mitambo 106 ya biogas imejengwa katika Vijiji vya Bwambo, Goha, Kirangare,
Bendera, Kihurio, Mtii, Vuje, Njagu, Ndungu, Myombo, Mjema, Maore, Mvaa na
Mpirani. Aidha, Serikali imekwishaanza kutoa uhamasishaji wa matumizi ya biogas
na mbolea ya samadi. Hata hivyo, kukiwa na uhitaji kama alivyoomba
Mheshimiwa Mbunge, Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi na kwa sababu inahusu
nishati na Waziri wa Nishati na Madini wanaweza kuambatana na wataalam
wao kutembelea Jimbo la Same Mashariki.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA Aliuliza:-
Wilaya ya Same ni miongoni mwa Wilaya zinazokumbwa na baa la njaa mara kwa mara na Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kupeleka chakula cha msaada; na kwa kuwa Wilaya ya Same ina mito mikubwa na maeneo yanayofaa kwa umwagiliaji:-
(a) Je, Serikali inasema nini juu ya maombi ya muda mrefu yaliyowasilishwa Wizarani ya kujenga Bwawa la Yongoma ili maji yatumike kwa ajili ya umwagiliaji kwenye mashamba yaliyoko katika Kata za Maore, Ndungu, Kihurio na Bendera;
(b) Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kujenga bwawa hilo ili kuokoa maisha ya wananchi na fedha nyingi za Serikali zinazotumika kununua chakula cha msaada mara kwa mara?
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kutokana na mabadiliko ya tabianchi, nchi yetu imekuwa inakumbwa na upungufu wa chakula katika maeneo machache. Ili kuondokana na hali hiyo, hivi sasa Wizara yangu inafanya mapitio ya mpango kabambe wa Taifa wa Umwagiliaji wa mwaka 2002.
Mheshimiwa Spika, bwawa la Yongoma ni bwawa ambalo litakuwa na ukubwa wa kati na litahudumia Kata za Maore na Ndungu. Serikali inashauri bwawa hilo lipewe kipaumbele na Halmashauri husika kama hatua muhimu ya kukabiliana na suala zima la mabadiliko ya tabianchi. Aidha, bwawa la Kalimawe ambalo linahudumia Kata za Kihurio, Bendera, Kalimawe na Ndungu, Wizara inashauri lifanyiwe ukarabati na Halmashauri.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inahusika na ujenzi wa mabwawa makubwa ya kimkakati ambayo yanaweza kutumika kwa shughuli mbalimbali zikiwemo matumizi ya maji ya kawaida ya majumbani, umwagiliaji na uzalishaji umeme. Kwa sasa, Wizara inatekeleza miradi ya mabwawa ya Farkwa (Dodoma), Lugoda (Iringa) na Kidunda (Morogoro Vijijini). Aidha, Wizara imekuwa ikitoa maelekezo kwa Halmashauri zote nchini kuweka kwenye mipango yake utaratibu wa kujenga mabwawa ya ukubwa wa kati na madogo. Wizara ipo tayari kutoa msaada wa kitaalam utakapohitajika.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatengeneza miundombinu ya maji katika Hifadhi ya Mkomazi ili kuzuia wanyamapori kuzurura kwenye makazi ya wananchi wakitafuta maji na kuharibu mazao yao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi inapatikana katika nyanda kame na hivyo kukabiliwa na uhaba wa maji kwa ajili ya matumizi ya wanyamapori. Wizara imefanya juhudi za kuchimba mabwawa kwa ajili ya kuhifadhi maji ambapo hadi sasa kuna jumla ya mabwawa tisa ambayo ni Mabata, Kuranze, Zange, Ndindira, Nobanda, Ngurunga, Mbula, Kavateta na Maore. Hata hivyo, kutokana na mabadiliko ya tabianchi ni mabwawa matatu tu yanahifadhi maji mwaka mzima.
Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto hiyo ya upungufu wa maji, Serikali inaendelea kuchimba mabwawa sita ili kukidhi mahitaji ambapo bwawa moja lilikamilika katika mwaka wa fedha wa 2016/2017 na mengine matano yatachimbwa katika mwaka huu wa fedha 2017/2018.
Aidha, katika mwaka 2017/2018 kisima kirefu kimoja kitachimbwa kwa ajili ya kusukuma maji na kujaza mabwawa yanayokauka ili kukidhi mahitaji ya maji wakati wa kiangazi kikali na wakati huo huo doria za kudhibiti wanyamapori wasitoke nje ya hifadhi zinaendelea kuimarishwa.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Jimbo la Same Mashariki lina Kata 14 lakini lina Kituo kimoja cha Polisi kilichopo Kata ya Maore na vituo vidogo vilivyopo Kata ya Ndungu na Kihurio; vituo vyote hivyo vipo katika tarafa moja yenye kata tano, kata nyingine tisa ambazo zipo katika tarafa mbili zilizoko mlimani na zipo mbali sana na vituo hivyo vya Polisi zinapata shida sana kutoa ripoti za uhalifu. Kwa kuwa wananchi wa tarafa hizo mbili za mlimani tayari wametenga maeneo ya kuweka vituo vya Polisi:-
(a) Je, Serikali ipo tayari kuanzisha Vituo vya Polisi katika Tarafa ya Mamba/Vunta na Tarafa ya Gonja?
(b) Kama Serikali ipo tayari kuanzisha Vituo hivyo vya Polisi, je, ni lini Polisi hao wataanza kazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani, najibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na Vituo vya Polisi katika ngazi ya Kata na Tarafa nchi nzima, Mamba/Vunta na Gonja zikiwemo. Katika Tarafa ya Gonja kuna Kituo cha Polisi, Daraja B kinachotoa huduma za kipolisi katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Tarafa ya Mamba wananchi wamejitolea eneo hilo kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Polisi ambapo kwa sasa majadiliano kati ya Jeshi la Polisi na wananchi kuhusu ujenzi wa Kituo cha Polisi, Daraja la B yanaendelea. Hata hivyo, kwa sasa Tarafa ya Mamba ina Kituo kidogo Daraja la C ambacho kinatoa huduma kwa wananchi katika Tarafa hiyo. Aidha, Jeshi la Polisi hufanya doria mara kwa mara katika maeneo hayo ya milimani ambayo hafikiwi kirahisi na vyombo vya usafiri kutokana na jiografia yake.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Sehemu kubwa ya Misitu ya Hifadhi ndani ya Wilaya ya Same ni Msitu wa Shengena ambao ni chanzo cha Mito mikubwa ya Nakombo, Hingilili, Yongoma na Saseni ambayo maji yake yanatumiwa na wakazi wa Majimbo ya Same Mashariki, Mlalo na Korogwe Vijijini:-
• Je, ni lini Serikali itaanzisha doria kulinda Msitu wa Shengena kuzuia uharibifu unaoendelea ikiwemo uchomaji moto ambao pia unaathiri maisha ya watu?
• Je, Serikali haioni umuhimu wa kuanzisha utaratibu wa uvunaji wa miti iliyokomaa katika Msitu wa Shengena na kuweka mkakati wa kuotesha miti mingine ili msitu uwe endelevu?
• Je, Serikali inasema nini juu ya athari za kimazingira zinazotokana na uchimbaji wa madini ya Bauxite unaoendelea katika Msitu wa Shengena?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara kupitia Wakala wa Huduma za Misitu kwa kushirikiana na Mamlaka ya Serikali ya Wilaya ya Same imekuwa ikitekeleza shughuli za doria na operations za mara kwa mara katika hifadhi za misitu ambapo wahalifu wanaopatikana na hatia ikiwa ni pamoja na uchomaji moto huchukuliwa hatua za kisheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kwa kuwa uharibifu wa misitu unahusisha baadhi ya wananchi wasiozingatia Sheria, Serikali inakamilisha mpango wa usimamizi shirikishi na wananchi wa vijiji vyote 23 alivyovitaja vinavyopakana na hifadhi ya Chome ushiriki ambao utaboresha ulinzi wa hifadhi.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, uhifadhi wa misitu ya mazingira asilia pamoja na mambo mengine unazingatia kutokuvuna miti hata baada ya kukomaa na pia kuacha miti ya asili iendelee kuota yenyewe badala ya kupanda miti mingine ili kulinda hifadhi na kuendeleza mfumo wa kiikolojia na bioanuwai zilizopo ndani ya hifadhi. Aidha, hatua hii inalenga kutunza, kuhifadhi na kuendeleza mfumo wa ikolojia ikiwa ni pamoja na vyombo vya maji na viumbe hai waliopo.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, uchimbaji wa madini katika maeneo ya hifadhi husimamiwa na sheria zikiwemo Sheria za Madini ya mwaka 2010, Sheria ya Misitu namba 14 ya mwaka 2002 na Sheria ya Usimamizi wa Mazingira (NEMA) ya mwaka 2004.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa hakuna taarifa rasmi zinazohusu uchimbaji wa madini ya Bauxite katika Hifadhi ya Msitu wa Shengena. Aidha, iwapo mtu yoyote binafsi au taasisi itahitaji kufanya shughuli za uchimbaji madini ndani ya hifadhi hiyo, atatakiwa kufuata taratibu za kisheria zitakazozingatia masuala yote muhimu ikiwemo kufanyika kwa tathmini ya athari ya mazingira kabla ya kuanza kwa uchimbaji huo.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Uharibifu wa mazingira kwenye Msitu wa Chome (Shengena) umeleta athari kubwa ya uchafuzi wa maji hasa katika Mito mikubwa ya Yongoma na Saseni; mito hiyo kuanzia kwenye vyanzo vya maji imebadilika rangi na kuonesha rangi yenye matope. Kwa kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii ilikanusha kwamba hakuna ushahidi unaoonesha kwamba athari za mazingira katika msitu huo zinatokana na uchimbaji wa madini ya bauxite.
• Je, Serikali ipo tayari kuunda Kamati ya kuchunguza chanzo cha uharibifu huo katika Msitu wa Shengena?
• Je, Serikali ipo tayari kuwapatia wananchi miti ya asili inayoongeza maji ili kudhibiti upungufu wa maji katika vyanzo vya maji mito hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, uharibifu wa mazingira kwenye msitu wa Chome - Shengena unachangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo shughuli za kilimo katika maeneo jirani yanayozunguka mlima Shengena na wachimbaji wadogo wa madini ya dhahabu waliovamia msitu huo miaka ya nyuma kati ya mwaka 2008 na 2010. Katika kutatua changamoto hii Serikali iliunda timu ya watalaam kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais, Baraza la Taifa la Hifadhi ya Mazingira yaani NEMC, Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), Ofisi ya Madini Mkoa wa Kilimanjaro na Bodi ya Mto Pangani ambayo ilitembelea eneo hilo kwa nyakato tofauti.
Mheshimiwa Mwenyekiti, timu hiyo ya wataalam ilibaini changamoto za uharibifu wa mazingira katika eneo hilo na kupendekeza hatua za kuzuia uharibifu huo ambazo zimetekelezwa ikiwa ni pamoja na kuzuia shughuli za uchimbaji wa madini ndani ya msitu kwa kuweka ulinzi ambao unafanywa na Jeshi la Kujenga Taifa (SUMA JKT).
Hivyo, Serikali itapitia upya mapendekezo ya timu ya wataalam na kuhakikisha kuwa ina…
hivyo, Serikali itapitia upya mapendekezo ya timu ya wataalam na kuhakikisha kuwa yanatekelezwa kikamilifu na iwapo itaonekana ni lazima kuunda Kamati, Serikali haitasita kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Serikali kupitia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) imeanza kuchukua hatua za kuwapatia wananchi miti ya asili na rafiki kwa mazingira kwa ajili ya kuhifadhi vyanzo vya maji katika Mito ya Yongoma na Saseni. Aidha, katika jitihada za kutunza vyanzo vya maji katika eneo hili, Serikali kupitia TFS imepanda miti ya asili takribani 2500 kati ya mwaka 2012 mpaka 2017 ndani ya eneo la Msitu wa Chome lililoharibiwa na shughuli za uchimbaji wa madini ya dhahabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nitumie fursa hii kuwasihi viongozi na watendaji wa Serikali katika ngazi zote kuchukua hatua kadri itakavyowezekana kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Usimamizi wa Mazingira ili kudhibiti uharibifu wa mazingira nchini.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Kwa kuwa Ripoti za Ukaguzi za Ufanisi unaofanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali zimeonesha kuna mapendekezo yanayotolewa baada ya ukaguzi mengi hayafanyiwi kazi na kwamba upungufu unaoibuliwa hujirudia mwaka hadi mwaka.
(a) Je, Serikali inakubaliana na pendekezo la kuanzisha kitengo maalum kitakachoratibu utekelezaji wa mapendekezo ya kaguzi za ufanisi?
(b) Je, Serikali inakubaliana na pendekezo kuwa baada ya Kamati ya PAC kujadili taarifa ya Ukaguzi wa Ufanisi ipeleke maoni yao kwa Kamati za Kisekta ili kutoa fursa kwa Kamati hizo kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa mapendekezo ya CAG hasa katika maeneo ya kisera na kiutendaji kwa mujibu wa Kanuni za Bunge?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ukaguzi wa ufanisi wa miradi unaratibiwa na kufanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ambaye hutoa mapendekezo yanayohitajika kutelekelezwa na wakaguliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mara baada ya taarifa ya kaguzi za ufanisi kukamilika, huwasilishwa Bungeni na Waziri mwenye dhamana na sekta husika, mfano Kilimo, Elimu, Maji na kadhalika, tofauti na ilivyo kwa taarifa za Ukaguzi wa Serikali Kuu na mashirika ya umma, ambapo taarifa zake huwasilishwa Bungeni na Waziri mwenye dhamana ya masuala ya fedha na taarifa ya kaguzi za Mamlaka za Serikali za Mitaa kuwasilishwa Bungeni na Waziri mwenye dhamana na masuala ya Mamlaka za Serikali za Mitaa. Vilevile utekelezaji wa mapendekezo ya taarifa za ufanisi (performance audit) huratibiwa na Wizara husika. Wizara za kisekta ndizo ambazo hufuatilia na kuhakikisha kuwa mapendekezo ya CAG yanafanyiwa kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na maelezo haya, haitakuwa vyema kuanzisha kitengo maalum cha kuratibu utekelezaji wa mapendekezo ya Taarifa ya Ukaguzi wa Ufanisi kwani kwa kufanya hivyo ni kuongeza gharama za uendeshaji wa Serikali. Hata hivyo Wizara, Idara au taasisi zinatakiwa kuwa na mpango kazi wa kuhakikisha kuwa mapendekezo yanayotolewa na CAG kupitia taarifa hizo, yanatekelezwa ipasavyo. Aidha, kupitia taarifa hizo za ufanisi, kunakuwa na masuala ambayo utekelezaji wake ni wa muda mfupi, muda wa kati na muda mrefu.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali siku zote ipo tayari na inatekeleza majukumu yake kwa mujibu wa Katiba, Sheria na Kanuni zilizowekwa zikiwemo Kanuni za Bunge. Hata hivyo, Serikali haina mamlaka ya kupanga au kuingilia majukumu yanayopaswa kutelekezwa na Kamati za Kudumu za Kisekta za Bunge. Hivyo basi, Bunge lako tukufu lina nafasi ya kuamua juu mapendekezo ya Mheshimiwa Mbunge.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-
Hali ya sekta ya kilimo na mifugo katika Jimbo la Same Mashariki ni mbaya licha ya kuwepo wafanyakazi wa Serikali wanaosimamia sekta hizo kwenye Wilaya, Kata na hata Vijiji. Wengi wa wafanyakazi hao wanatumia muda mwingi kufanya kazi zao binafsi badala ya kuwasaidia wakulima na wafugaji kuleta mabadiliko katika sekta hizo.
(a) Je, Serikali inatumia kigezo gani kutathmini utendaji kazi wa waajiriwa hao kupima ufanisi wao?
(b) Je, Serikali ipo tayari kupunguza idadi ya waajiriwa hao waliopo vijijini ili fedha itakayookolewa kutoka katika mishahara yao isaidie kutengeneza miundombinu ya umwagiliaji na malambo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPH G. KAKUNDA) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuwasimamia maofisa ugani kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa, Wizara za Kisekta hutoa miongozo inayoainisha viwango vya kitaalam na ikama. Mamlaka za Serikali za Mitaa husimamia masuala ya kiutawala na utendaji kazi wa siku kwa siku ikiwemo kupima ufanisi na tija kwa kutumia Mfumo wa Wazi wa Upimaji wa Watumishi wa Umma (Open Performance and Review Appraisal System – OPRAS) ambapo kila mtumishi hukubaliana na mwajiri kuhusu malengo yatakayotekelezwa kwa mwaka mzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa bado kuna upungufu mkubwa wa maafisa ugani wa kilimo na mifugo nchini, badala ya kupunguza idadi yao, mpango uliopo kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi Ibara ya 22(b) ni kuongeza idadi ya Maafisa Ugani kutoka 9,558 waliokuwepo mwaka 2014 hadi 15,082 ifikapo mwaka 2020.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuwakumbusha maafisa ugani wote na wasimamizi wao kutekeleza maagizo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu yaliyowataka Maafisa Ugani kutokaa ofisini na badala yake kwenda vijijini kuwasaidia wakulima na wafugaji. Nazikumbusha mamlaka za nidhamu kuchukua hatua kali dhidi ya Maafisa Ugani wazembe wasiowajibika kwa umma.
MHE. RUTH H. MOLLEL (K.n.y. MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA) aliuliza:-

SUMA-JKT Idara ya Zana za Kilimo ilikopesha 5,355,153,000/= kwa idara mbalimbali ndani ya SUMA-JKT. Taarifa za CAG zimeonesha kuwa hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2016 ni kiasi cha Sh.534,785,000/= ambayo ni kiasi chini ya asilimia 10 ndio kilirejeshwa:-

(a) Je, ni kiasi gani hadi sasa kimerejeshwa kwenye Idara hiyo ya Zana za Kilimo?

(b) Je, Serikali itakubaliana na mimi kwamba, uzembe huu wa kutohakikisha mikopo ya fedha za Serikali inarudishwa kwa wakati ili wakulima wengine nao waweze kukopeshwa kumechangia kukwamisha juhudi za kupunguza umaskini nchini?

(c) Je, Serikali inachukua hatua gani kuwawajibisha waliohusika na utoaji huo wa mikopo bila kuhakikisha inarudishwa kwa wakati?
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, lenye Sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa mradi wa zana za kilimo wa SUMA-JKT ulikopesha miradi mingine ndani ya SUMA-JKT jumla ya shilingi 5,355,153,000/= kama ilivyoelezwa katika Taarifa ya CAG ya mwaka 2015/2016 na kwamba mpaka kufikia tarehe 30 Juni, 2016, kiasi cha shilingi 534,785,000/= ndicho kilikuwa kimerejeshwa. Hadi kufikia tarehe 31 Januari, 2019, jumla ya shilingi 2,389,082,000/= zimerejeshwa katika mradi wa zana za kilimo ambayo ni sawa na asilimia 45 ya fedha zote zilizokopeshwa. Hivyo, mpaka sasa fedha ambazo bado hazijarejeshwa ni shilingi 2,966,071,000/=.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo kubwa la kukopesha fedha hizo lilikuwa ni kuiwezesha kimtaji miradi ndani ya SUMA-JKT pamoja na miradi mingine mipya baada ya kujiridhisha kuwa ina tija. Hivyo, lengo hili halikwamishi juhudi za kupunguza umasikini nchini, basi linaongeza mapato katika miradi ya shirika kwa ujumla.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, Shirika la SUMA-JKT limeendelea kuhakikisha fedha zilizobaki zinarejeshwa katika mradi wa zana za kilimo kwa kuchukua hatua zifuatazo:-

(i) Kuhakikisha uwepo wa mikataba kati ya mradi wa zana za kilimo na mkopaji, pia mikataba iliyokuwa na upungufu imerekebishwa;

(ii) Kuhakikisha miradi iliyokopeshwa inazalisha kwa faida ambapo sehemu ya fedha hiyo huwasilishwa moja kwa moja katika mradi wa zana za kilimo; na

(iii) Kuweka baadhi ya miradi iliyokopeshwa chini ya usimamizi wa moja kwa moja wa mradi wa zana za kilimo.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

Kata za Bendera na Makanya zina jasi nyingi na jasi inaweza kutoa malighafi kutengeneza gypsum boards, mabomba ya maji machafu, saruji, POP na mbolea:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia kupatikana kwa mwekezaji ili aanzishe viwanda hivyo katika maeneo hayo ya Wilayani Same?
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, UWEKEZAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba kujibu swali la Mheshimwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ni kujenga uchumi wa kati unaoongozwa na sekta ya viwanda ifikapo mwaka 2025. Aidha, viwanda vinavyotumia rasilimali zinazopatikana nchini na kuzalisha bidhaa zinazotumika kwa wingi vimepewa kipaumbele. Kutokana na utekelezaji wa azma hiyo, nchi yetu sasa imeweza kuzalisha baadhi ya bidhaa zinazotosheleza soko la ndani na ziada kuuza nje ya nchi ikiwemo bidhaa zinazotokana na malighafi ya jasi.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua lengo la Serikali ni kuongeza uzalishaji wa ndani na kupunguza uagizaji wa bidhaa kutoka nje katika maeneo yote yenye rasilimali zinazoipa Tanzania faida ya ushindani (competitive advantage), Serikali itaendelea kuvutia uwekezaji katika maeneo yote yenye rasilimali ikiwemo jasi inayopatikana katika Kata za Bendera na Makanya Wilayani Same.

Mheshimiwa Spika, aidha, napenda kutumia fursa hii kuupongeza uongozi wa Mkoa wa Kilimanjaro na Wilaya ya Same kwa kutenga eneo katika Kata ya Makanya kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda cha saruji na kuingizwa katika Mwongozo wa Uwekezaji wa Mkoa wa Kilimanjaro na hatua za kutafuta wawekezaji zinaendelea. Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na taasisi zingine kama vile Kituo cha Uwekezaji Tanzania, Mamlaka ya EPZ, Tume ya Madini na wadau wengine tutaendelea kushirikiana kuzitangaza fursa za uwekezaji za Wilaya ya Same ili kuvutia na kutekeleza uwekezaji katika jasi iliyoko wilayani Same.

Aidha, napenda kuzikumbusha Wizara, taasisi za Serikali na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuendelea kusimamia mikakati ya kuboresha mazingira ya uwekezaji katika maeneo yao ikiwemo kuainisha na kuyapembua kiyakinifu maeneo yote yenye rasilimali, kuyatenga na kuyarasimisha kwa ajili ya uwekezaji ili kupunguza migogoro isiyo ya lazima na wawekezaji ili kufikia dhamira ya Serikali kufikia uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. NAGHENJWA L. KABOYOKA) aliuliza:-

Umeme wa maji unaonekana kuwa wa bei nafuu, na Same kuna maporomoko ya Mto Hingilili yanayoangukia Kata ya Maore na ya Mto Yongoma yanayoangukia Kata ya Ndungu; na Chuo cha Ufundi Arusha wameonesha utaalamu mkubwa wa kutengeneza umeme kwa kutumia maji hayo:-

Je, Serikali ipo tayari kukiwezesha Chuo hicho ili kiweze kujenga mitambo ya kuzalisha umeme wa maji Kata za Maore na Ndungu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua muhimu ya awali katika uendelezaji wa mradi wa kufua umeme ukiwemo wa maporomoko ya maji ni kufanya upembuzi yakinifu ambapo pamoja na mambo mengine tathmini ya wingi wa maji katika kipindi cha kuzalisha umeme (water resource assessment) lengo ni kujua kiasi cha umeme utakaozalishwa na gharama za kutekeleza mradi na manufaa yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Serikali kupitia TANESCO na wadau wengine inaendelea kufanya tathmini za awali katika vyanzo mbalimbali vya kuzalisha umeme wa maporomoko ya maji makubwa na madogo ikiwemo maporomoko ya Mto Hingilili. Tathmini hizo zitafanyiwa kazi kulingana na matokeo yake na maeneo yanayohusika yatajulishwa ikiwa ni pamoja na Chuo cha Ufundi Arusha.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

Wananchi wa Jimbo la Same Mashariki wako tayari kuanzisha misitu ya vijiji kwenye maeneo yenye ukame kama vile Kata za Bendera, Kihurio, Ndugu na Maore ili kuhifadhi mazingira.

Je, Serikali ipo tayari kuanzisha miradi ya utunzaji wa mazingira katika kata tajwa kwa kufundhisha wanavijiji uanzishwaji wa misitu ya vijiji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Same kiikoloji na kijiografia imegawanyika katika Kanda kuu mbili, yaani ukanda wa mlimani ambapo hali yake ya hewa ni nzuri ukilinganisha na ukanda wa tambarare ambapo hali ya hewa ni ukame. Kwa maana hiyo, kata zilizotajwa na Mheshimiwa Mbunge zipo katika ukanda wa tambarare na kwa bahati nzuri zina uoto wa misitu.

Mheshimiwa Spika, Wizara imeweka utaratibu wa kushirikiana na halmashari za wilaya na wananchi katika kutekeleza majukumu yake ya usimamizi wa maliasili. Mathalani, katika halmashauri ya Wilaya ya Same, utunzaji wa mazingira umehusisha utoaji wa elimu kwa wananchi na kuanzisha Kamati za Maliasili na Misitu, kuandaa mipango ya usimamizi na kutunga sheria ndogo za usimamizi wa maliasili. Vilevile, kupitia utaratibu huu wananchi wanashirikiana na Wizara na halmashauri kupanda miti kwenye maeneo ya wazi.

Mheshimiwa Spika, Serikali iko tayari kuendelea kutekeleza azma ya kuwasaidia wananchi wa Kata za Bendera, Kihurio, Ndungu na Maore kuhusu shabaha yao ya kutunza misitu hiyo ya asili. Hii inatokana na ukweli kwamba pamoja na kuwa vijiji hivi viko nyanda za ukame bado vina uoto mzuri wa asili ambao ukitunzwa vizuri utasaidia kuboresha hali ya hewa, uhifadhi wa baionuai na huduma za kijamii kama maji.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya Same – Kisiwani hadi Mkomazi ambayo inaunganisha Majimbo matano ya Same Magharibi, Same Mashariki, Mlalo, Mkinga na Korogwe Vijijini?

(b) Je, ni fedha kiasi gani zimetumika kuanzia mwaka 2015/2016 – 2019/2020 kwa ajili ya kukarabati barabara hiyo?
WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO alijibu:

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu kwa pamoja swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Same – Kisiwani – Mkomazi imekuwa ikifanyiwa matengenezo ya aina mbalimbali kila mwaka. Aidha, kuanzia Mwaka wa Fedha 2015/2016 hadi 2019/2020, kiasi cha Sh.3,299.365 kimetumika kwa ajili ya matengenezo mbalimbali ya barabara hiyo. Kufuatia kufanyika na kukamilika kwa upembuzi yakinifu pamoja na usanifu wa kina kwa kilometa zote za barabara hiyo kilometa 100.5, Serikali kupitia Wizara yangu imetenga kiasi cha shilingi bilioni tano (Shilingi milioni 5,000.00) katika Mwaka wa Fedha 2020/2021 ili kitumike kuanza ujenzi kwa barabara hiyo kwa kiwango cha lami.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawalipa wakulima wa tangawizi Mamba Myamba, Wilaya ya Same Mashariki ambao walifungiwa na SIDO mashine zisizo na kiwango cha kuchakata tangawizi?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ushirika wa Wakulima wa Mamba Myamba uliopo Wilaya ya Same, tarehe 21/05/2010 uliwapa SIDO kazi ya kutengeneza mtambo wa kuchakata tangawizi kupitia Halmashauri ya Same ambao ulikuwa unahusisha hatua tano za uchakataji ambazo ni kuosha, kukata, kukausha, kusaga na kufungasha. SIDO iliingia mkataba na Halmashauri ya Same na Chama cha Ushirika cha Msingi cha Mazao na Masoko. Mradi huo ulikuwa na thamani ya shilingi 88,895,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtambo huo ulikamilika na kulisimikwa tarehe 29/10/2012 na ulifanya kazi. Hata hivyo katika ufanyaji kazi wake kulikuwa na changamoto mbalimbali ambazo baadaye zilirkebishwa na mtambo huo tena kusimikwa upya tarehe 27/2/2015.

Aidha, SIDO ilinunua tangawizi kutoka kwa wakulima na kufanya majaribio katika mtambo huo ambao ulionekana kufanya kazi vizuri. Mpaka sasa mtambo huo unaendelea kufanya kazi vizuri na wana ushirika wanaendelea na shughuli zao za uchakataji wa zao la tangawizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa mkataba ulioingiwa na SIDO, majukumu ya SIDO yalikuwa ni kutengeneza na kufunga mtambo kazi ambayo ilikamilika. Hata hivyo, baada ya changamoto zilizojitokeza Serikali imeielekeza SIDO ishauriane na Halmashauri ya Same namna bora ya kutatua changamoto ambazo zimejitokeza kwa kushirikiana na Ushirika wa Mamba Myamba ili kuona changamoto walizonazo zinatatuliwa.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka vitendea kazi Kituo cha Afya Kata ya Mtii, Jimbo la Same Mashariki baada ya kukamilika kwa vyumba 12 vya Jengo la OPD?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuweka kumbukumbu sahihi kwanza naomba nianze kwa ufafanuzi kwamba jengo linalojengwa eneo la Mtii ni zahanati na si kituo cha afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zahanati ya mpya inayojengwa kwa nguvu za wananchi, fedha za Mfuko wa Jimbo, wadau wa maendeelo pamoja na fedha za Halmashauri. Majengo yanayojengwa ni pamoja na Jengo la Wagonjwa wa Nje na Jengo la Huduma ya Kliniki ya Afya ya Mama na Mtoto ambayo tayari yamekamilika na ujenzi wa Jengo la Huduma za Uzazi unaendelea. Aidha, Halmashauri ya Wilaya ya Same imepokea fedha shilingi milioni 150 iliyotengwa kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021 ambapo Zahanati ya Mtii imepokea shilingi milioni 50 itakayotumika kukamilisha Jengo la Wazazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Zahanati ya Mtii itakapokamilika itapatiwa usajili na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na kuwekewa utaratibu wa kupatiwa vitendea kazi.

Aidha, kwa sasa Serikali imeweka kipaumbele cha ununuzi wa vifaa tiba katika Hospitali za Halmashauri na Vituo vya Afya vilivyojengwa na kukarabatiwa na kote nchini, vikiwemo Vituo vya Afya vya Ndungu, Shengena na Kisiwani ambavyo vimepokea shilingi milioni 400 kila kimoja na Zahanati ya Kasapo iliyopokea shilingi milioni 154 vilivyoko kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Same ambavyo tayari vimepokea fedha hizo na shughuli za ujenzi zinaendelea ujenzi na ukarabati wa vituo hivyo umekamilika na huduma sasa zinatolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Halmashauri ya Wilaya ya Same iweke kipaumbele kwa kutenga bajeti kwa kupitia mapato yake ya ndani kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba vya zahanati mpya ya Mtii pindi itakapokamailika na kupatiwa usajili.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa maboma ya Shule za Sekondari Bombo na Ndungu ili Kidato cha Tano kianze baada ya mabweni ya wasichana kukamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Shule za Sekondari Bombo na Ndungu zilizopo Halmashauri ya Wilaya ya Same ni shule za kutwa zinazopokea wanafunzi wa kidato cha kwanza hadi cha nne. Serikali ina mpango wa kuzipandisha hadhi shule hizi ili ziweze kuchukua wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita. Katika kutekeleza mpango huo katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Same shilingi milioni 150 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni mawili katika Shule ya Sekondari Bombo na shilingi milioni 75 kwa ajili ya ujenzi wa bweni moja katika Shule ya Sekondari Ndungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa bweni moja katika Shule ya Sekondari Bombo umekamilika na ujenzi wa bweni moja unaendelea; na ujenzi wa bweni katika Shule ya Sekondari Ndungu umekamilika. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Same shilingi milioni 50 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa bweni katika Shule ya Sekondari Bombo na shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa bwalo la chakula katika Shule ya Sekondari Ndungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Same kwa kushirikiana na wananchi inaendelea na ujenzi wa vyumba vinne vya madarasa katika Shule ya Sekondari Ndungu. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 120 kwa ajili ya ujenzi wa bweni moja na maktaba ya TEHAMA katika Shule ya Sekondari Ndungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu hiyo inatarajiwa kukamilika mwezi Septemba, mwaka 2022 hivyo kuwezesha Shule hizo kuanza kuchukua wanafunzi wa Kidato cha Tano na Sita.
MHE. CECILIA D. PARESSO K.n.y. MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatatua mgogoro uliopo katika eneo lenye madini ya Jasi kati ya Wananchi wa Kata ya Bendera Mkoani Kilimanjaro na Wananchi wa Kata ya Mkomazi Mkoani Tanga?
NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Madini kupitia Tume ya Madini, imetoa leseni za uchimbaji mdogo katika maeneo hayo ya Kata ya Bendera iliyopo Mkoani Kilimanjaro na Kata ya Mkomazi iliyopo Mkoani Tanga.

Mheshimiwa Spika, katika maeneo hayo ya kata hizo mbili, hivi tunavyoongea, hakuna mgogoro wowote unaohusiana na leseni za uchimbaji mdogo wa madini ya Jasi na wachimbaji wanaendelea na shughuli zao kama kawaida. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanzisha Vituo vya Polisi katika Tarafa za Gonja na Mamba/Vunta?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na vituo vya Polisi katika maeneo mbalimbali nchini. Katika Tarafa ya Gonja kuna Kituo cha Polisi cha Daraja B kinachoongozwa na Mrakibu Msaidizi wa Polisi na kina Askari 16 na gari moja. Tarafa ya Mamba haina Kituo cha Polisi wala haijatenga eneo kwa ajili ya ujenzi wa kituo na makazi ya Askari. Hivyo tarafa, hiyo hupata huduma za Polisi toka kituo cha Polisi Gonja na vituo vidogo vya Polisi vya Kihurio na Ndungu vilivyo katika Tarafa ya Mamba.

Mheshimiwa Spika, ni ushauri wetu kwa Mheshimiwa Mbunge kushirikisha Halmashauri ya Wilaya ya Same kutenga eneo katika Tarafa ya Mamba kwa ajili ya kujenga Kituo cha Polisi, pamoja na nyumba za makazi ya Askari ili Serikali iweze kuingiza katika mpango wa kukitengea bajeti ya ujenzi.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, ni nani mwenye jukumu la kusafisha mifereji na kuzibua makaravati ya barabara zinazojengwa chini ya TARURA au TANROADS?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghejwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, jukumu la usafi wa barabara na mifereji ikiwa ni pamoja na kuzibua makaravati ni la msimamizi wa barabara husika. Hivyo, kwa barabara za TANROADS mhusika ni TANROADS na za TARURA mhusika ni TARURA.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanzisha vituo vya Polisi katika Tarafa za Gonja na Mamba/Vunta?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge Wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na vituo vya Polisi katika maeneo mbalimbali nchini kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi. Tarafa za Gonja na Mamba/Vunta hazina vituo vya polisi wala maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya polisi na Nyumba za Makazi ya Askari. Wananchi wa Tarafa za Gonja na Mamba/Vunta hupata huduma za polisi toka vituo vya polisi vya Same mjini na Gonja, na vituo vidogo vya polisi vya Kihurio na Ndungu.

Mheshimiwa Spika, ni ushauri wangu kwa Mheshimiwa Mbunge kushirikisha Halmashauri ya Wilaya ya Same kutenga maeneo katika tarafa za Mamba na Gonja kwa ajili ya kujenga kituo cha Polisi pamoja na Nyumba za Makazi ya Askari, ili Serikali iweze kuweka kwenye mpango wake wa Bajeti kwa ajili ya utekelezaji. Nashukuru. (Makofi)
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha za kutosha za ujenzi wa barabara za Wilaya ya Same baada ya kutengewa 9.5% tu ya fedha za TARURA kwa mwaka 2018/2019?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Same ina mtandao wa barabara zipatazo kilometa 874.64 ambazo ni sawa na asilimia 18.89 ya mtandao wote wa barabara katika Mkoa wa Kilimanjaro wenye kilometa 4,629.45.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2018/2019 Wilaya ya Same ilitengewa jumla ya shilingi bilioni 1.29 sawa na asilimia 12.81 ya bajeti ya Mkoa wa Kilimanjaro ya shilingi bilioni 10.13. Hata hivyo, bajeti kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya Same imekuwa ikipanda kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Wilaya ya Same ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 3.70 sawa na asilimia 16.24 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 22.83. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 5.80 sawa na asilimia 18.32 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 31.65.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya ya Same kadri ya upatikanaji wa fedha kwa kuzingatia mtandao wa barabara uliopo.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha za kutosha za ujenzi wa barabara za Wilaya ya Same baada ya kutengewa 9.5% tu ya fedha za TARURA kwa mwaka 2018/2019?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Same ina mtandao wa barabara zipatazo kilometa 874.64 ambazo ni sawa na asilimia 18.89 ya mtandao wote wa barabara katika Mkoa wa Kilimanjaro wenye kilometa 4,629.45.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2018/2019 Wilaya ya Same ilitengewa jumla ya shilingi bilioni 1.29 sawa na asilimia 12.81 ya bajeti ya Mkoa wa Kilimanjaro ya shilingi bilioni 10.13. Hata hivyo, bajeti kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya Same imekuwa ikipanda kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Wilaya ya Same ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 3.70 sawa na asilimia 16.24 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 22.83. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 5.80 sawa na asilimia 18.32 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 31.65.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya ya Same kadri ya upatikanaji wa fedha kwa kuzingatia mtandao wa barabara uliopo.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga fedha za kutosha za ujenzi wa barabara za Wilaya ya Same baada ya kutengewa 9.5% tu ya fedha za TARURA kwa mwaka 2018/2019?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Same ina mtandao wa barabara zipatazo kilometa 874.64 ambazo ni sawa na asilimia 18.89 ya mtandao wote wa barabara katika Mkoa wa Kilimanjaro wenye kilometa 4,629.45.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2018/2019 Wilaya ya Same ilitengewa jumla ya shilingi bilioni 1.29 sawa na asilimia 12.81 ya bajeti ya Mkoa wa Kilimanjaro ya shilingi bilioni 10.13. Hata hivyo, bajeti kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya Same imekuwa ikipanda kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Wilaya ya Same ilitengewa kiasi cha shilingi bilioni 3.70 sawa na asilimia 16.24 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 22.83. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 5.80 sawa na asilimia 18.32 ya bajeti ya Mkoa ya shilingi bilioni 31.65.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Wilaya ya Same kadri ya upatikanaji wa fedha kwa kuzingatia mtandao wa barabara uliopo.
MHE AIDA J. KHENANI K.n.y. MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, kwa nini Serikali isitumie mbao za Mitiki zenye ubora sawa na Mninga/Mkongo kwani tenda za Serikali zinataka Mninga/Mkongo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, shughuli za ujenzi na utengenezaji wa samani ambazo kiuhalisia zimekuwa zikikua sambamba na ongezeko la watu, zinategemea sana rasilimali ya misitu kama chanzo cha malighafi.

Mheshimiwa Spika, kutokana na kukua kwa mahitaji na changamoto ya upatikanaji wa miti migumu kutoka katika misitu ya asili hasa jamii ya mninga na mkongo, Wizara imefanya utafiti kuhusu tabia na sifa za mbao za matumizi kutoka kwenye miti isiyofahamika sana. Utafiti huo uliolenga kutambua tabia na sifa za kimwonekano, kiufundi na kianatomiki za mbao za miti isiyojulikana sana, ulionesha kuwa mti wa mitiki, una sifa ama sawa au zinazokaribiana sana na miti ya mkongo na mninga.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia matokeo ya utafiti huo, Serikali inaangalia uwezekano wa kuongeza miti mipya iliyofanyiwa utafiti katika orodha ya miti iliyoainishwa katika Sheria ya manunuzi inayosimamiwa na PPRA ili itumike katika kutengeneza samani za Serikali.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaweka katazo la kisheria la kuswaga mifugo ili kuzuia uharibifu wa mazingira?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, usafirishaji wa mifugo hufanyika chini ya Sheria ya Magonjwa ya Wanyama, Sura 156 na Kanuni zake za Udhibiti wa Usafirishaji wa Wanyama na Mazao ya Wanyama, G.N. 28 za mwaka 2007, ambapo usafirishaji wa mifugo kutoka wilaya moja kwenda nyingine hufanyika baada ya mifugo kukaguliwa na wataalam na kupatiwa kibali cha kusafirishwa. Aidha, Waraka wa Rais Na.1 wa Mwaka 2002 uliziagiza Serikali za Mitaa kote nchini kutunga sheria ndogo ili kuzuia uswagaji wa mifugo.

Mheshimiwa Spika, kwa maelezo hayo hapo juu inathibitisha kwamba sheria ipo. Hivyo basi, wafugaji wanahimizwa kuzingatia Sheria ya Magonjwa ya Wanyama, Sura 156 pamoja na sheria ndogo zilizopo ndani ya halmashauri zao zinazozuia uswagaji wa mifugo. Pia, nitumie fursa hii kuzielekeza halmashauri ambazo mpaka sasa hazijatunga sheria ndogo za kuzuia uswagaji wa mifugo zifanye hivyo mara moja.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuanzisha masomo yatakayoibua vipaji vya watoto kuanzia shule za msingi?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa masomo yanayoibua vipaji vya watoto kuanzia ngazi ya elimu ya msingi. Kwa kuliona hilo Wizara ilianzisha somo la sayansi na teknolojia kuanzia darasa la tatu; stadi za kazi pamoja na sanaa na michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika masomo hayo mada mbalimbali zinazochochea vipaji zinafundishwa. Kwa mfano katika somo la stadi za kazi wanafunzi hujifunza muziki, uigizaji, ufinyanzi na ususi. Katika somo la michezo na sanaa wanafunzi hujifunza michezo sahili, michezo ya jadi, riadha na mpira. Aidha kwa upande wa somo la sayansi na teknolojia wanafunzi hujifunza matumizi ya nishati, majaribio ya kisayansi, mashine na kazi na kuelea na kuzama kwa vitu.

Aidha, Wizara imetoa mwongozo wa ubainishaji na utambuzi wa wanafunzi wenye vipawa na vipaji wa mwaka 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Serikali kwa sasa inaendelea na mapitio ya mitaala ikiwemo Mtaala wa Elimu ya Msingi ambapo ushauri wa Mheshimiwa Mbunge utazingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, lini Serikali itatoa elimu kwa wafugaji kuhusu matumizi ya biogas ili kuhamasisha ufugaji wa kisasa?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mifugo na Uvuvi imekuwa ikitoa elimu ya ufugaji bora ikiwa ni pamoja na matumizi ya samadi kuzalisha biogas ambayo ni nishati mbadala ya kupikia na rafiki kwa mazingira.

Mheshimiwa Spika, matumizi ya nishati mbadala ya biogas ambayo inatokana na kinyesi cha mifugo ikitumika vizuri, itapunguza matumizi ya kuni na mkaa hivyo kuboresha maisha ya wafugaji na kuhifadhi mazingira. Kutokana na umuhimu huo, Wizara kupitia Wakala ya Mafunzo ya Mifugo (LITA), inatoa mafunzo ya utengenezaji wa biogas kwa wanafunzi wanaosoma katika vyuo vyake katika ngazi ya cheti na diploma ili watakapohitimu masomo hayo, wawe na ujuzi wa teknolojia ya biogas na waweze kuwafundisha wafugaji matumizi sahihi ya teknolojia hiyo pia. LITA hutoa mafunzo ya muda mfupi kwa wafugaji au vikundi vya wafugaji vinavyohitaji mafunzo hayo katika kampasi za Mpwapwa na Tengeru.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

Je, ni ni kwa nini Serikali pindi inapotwaa maeneo ya wakulima isiwatengee maeneo mengine mbali ya kulipa fidia?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI, alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingston Kaboyoka Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi, Sura 113 kifungu cha 3 Kifungu kidogo cha (1)(g), malipo ya fidia ni takwa la kisheria pindi Serikali inapotwaa ardhi kutoka kwa wananchi. Kimsingi, fidia kwa mujibu wa Sheria inajumuisha thamani ya ardhi na maendelezo yaliyopo juu ya ardhi. Fidia yaweza kulipwa kwa fedha au kupewa ardhi mbadala au vyote kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitekeleza fidia ya ardhi mbadala au fedha au vyote kwa pamoja kutokana na mazingira ya eneo la mradi, ahsante.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafanya tathmini ya kampuni zilizo chini ya NARCO ili kuona tija zake katika uchumi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) inamiliki ranchi 15 na imewekeza katika ranchi nane kati ya hizo. Aidha, NARCO imegawa vitalu na kukodishwa kwa wafugaji na kampuni binafsi kwa ajili ya ufugaji wa kisasa na wa kibiashara. Mwezi Oktoba, 2022 Serikali kupitia Kampuni ya Ranchi za Taifa (NARCO) ilifanya tathmini kwenye vitalu 116 ambavyo vimekodishwa kwa wafugaji ili kubaini hali ya uwekezaji kulingana na mipango ya biashara iliopo kwenye mikataba yao. Katika tathmini hiyo ilibainika kuwa wawekezaji 76 wamewekeza kulingana na mkataba na wawekezaji 40 wameonesha kutofanya vizuri kulingana na mikataba yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tathimini ilibaini kuwa NARCO inakabiliwa na changamoto za kimtaji, hivyo imeandaa andiko la mabadiliko ili kuiwezesha kupata mtaji kutoka vyanzo mbalimbali vya fedha. Hata hivyo, ili kuimarisha Kampuni ya NARCO na kuongeza tija, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imewekeza kiasi cha shilingi bilioni 4.6 kwa ajili ya kununua ng’ombe wazazi, kuchimba visima virefu na kununua mitambo ya kulima, kuvuna na kuhifadhi malisho ya mifugo.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

Je, lini Serikali italeta Bungeni Muswada wa Sheria wa kulinda ardhi ya Kilimo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kulinda ardhi ya kilimo kama ilivyobainishwa katika Sera ya Taifa ya Kilimo ya mwaka 2013. Kwa msingi huo, Wizara inapitia na kuchambua Sheria Mbalimbali zinazohusiana na usimamizi na matumizi ya ardhi ya kilimo ikiwemo Sheria ya Ardhi ya Vijiji, Sura ya 114, Sheria ya Ardhi, Sura ya 113 na Sheria ya Mipango ya Matumizi bora ya Ardhi, Sura ya 116 na Sheria ya Utwaaji wa Ardhi, Sura ya 118.

Mheshimiwa Spika, uchambuzi huo utabainisha upungufu uliopo katika sheria hizo na kuainisha maeneo ambayo yatajumuishwa kwenye Sheria ya Maendeleo ya Kilimo inayopendekezwa kutugwa ambayo itakuwa na sehemu ya masuala ya usimamizi wa ardhi ya kilimo. Baada ya uchambuzi huo wa kitaalam, itawasilishwa kwenye ngazi za maamuzi kuhusu mapendekezo ya sheria hiyo.