Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Anthony Calist Komu (5 total)

MHE. JAMES F. MBATIA (K.n.y. MHE ANTONY C. KOMU) aliuliza:-
Tarehe 13/8/2012 Halmashauri ya Wilaya ya Moshi ilitangaza zabuni Tenda Na. LGA/046/2011/2012/RWSSP/1 katika gazeti la Mwananchi. Tenda hiyo ilihusu mradi wa mfumo wa kusambaza maji na ungehusisha Vijiji vya Mande na Tella katika Kata ya Oldmoshi Magharibi. Hadi sasa mradi huo haujaanza pamoja na ufuatiliaji wa karibu wa Diwani na Kamati za Maji za Vijiji vya Tella na Mande hawakufanikiwa kupata majibu juu ya mradi tajwa.
Je, ni lini Serikali itaanza kujenga mradi huo muhimu kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Antony Calist Komu, Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2012/2013, Halmashauri ya Wilaya ya Moshi ilitangaza zabuni kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mikubwa mitatu ya maji yaani Korini, Bori na Tella-Mande ambapo Kampuni ya Jandu Plumbers Limited ya Arusha ilipata Zabuni hiyo. Kulingana na upatikanaji wa fedha, kipaumbele kiliwekwa kuanzia utekelezaji wa mradi wa Korini na Bori ambayo imekamilika. Mradi wa Korini umegharimu shilingi bilioni 1.2 na umekamilika mwaka 2014 na mradi wa Bori umekamilika mwezi Juni, 2016 na kuzinduliwa na mbio na Mwenge.
Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi wa Tella na Mande umepangwa kuaanza mwaka 2016/2017 baada ya kukamilika kwa miradi mikubwa miwili ya Korini na Bori. Mradi huo umetengewa shilingi milioni 759.4 kwa ajili ya kuimarisha chanzo cha Masokeni pamoja na miundombinu mingine ya kusambaza maji kuwafikia wananchi.
MHE. ANTONY C. KOMU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya mara kwa mara ya kuyapima upya mashamba yaliyotaifishwa wakati wa Azimio la Arusha ambayo hivi sasa yamebadilishwa matumizi na kujengwa Shule, Zahanati, Hospitali, Makazi na kadhalika?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Antony Calist Komu, Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna mashamba kadhaa nchini yaliyotaifishwa wakati wa Azimio la Arusha. Baadhi ya mashamba hayo yaligawiwa kwa mashirika na taasisi za Umma kwa ajili ya kuyaendeleza hususan kwa kilimo cha kahawa na mkonge.

Hata hivyo, baadhi ya mashamba hayo yamebadilishiwa matumizi na yamekuwa yakitumiwa na wananchi kwa matumizi mbalimbali ya kiuchumi na kijamii ikiwemo makazi, shule, zahanati, hospitali na kadhalika. Wizara yangu kwa kushirikiana na Halmashauri mbalimbali nchini, imeendelea kuyakagua, kuyaandalia mipango ya matumizi ya ardhi na kupima upya baadhi ya mashamba hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya mashamba ambayo Wizara yangu kwa kushirikiana na Halmashauri imeyaandalia mpano wa matumizi ya ardhi ni pamoja na Kihuhwi Estate, Sagulas Estate, Lewa Estate, Bombwera Estate, Geiglitza Azimio, Kilapula pamoja na Kibaranga yote ya Mkoa wa Tanga. Mashamba mengine ni New Msovero Farm, Mvumi Farms/Estate Kilosa pamoja na Luipa Estate yaliyopo Mkoani Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi jukumu la kuandaa mipango ya matumizi ya mashamba hayo ni la Halmashauri husika yalipo mashamba hayo. Hivyo, ninaagiza Halmashauri zote nchini kuendelea kukagua mashamba yaliyotaifishwa wakati wa Azimio la Arusha ili yaandaliwe mipango ya matumizi ya ardhi na kupimwa.

Aidha, natoa rai kwa Halmashauri zote nchini kuhakikisha zinatenga bajeti kwa ajili ya kupanga na kupima mashamba husika ili yaweze kutumika kwa tija kulingana na mahitaji halisi ya sasa.
MHE. ANTHONY C. KOMU aliuliza:-

Mkoa wa Kilimanjaro unao kilimo cha umwagiliaji kinachotumia vyanzo vya asili kama chemchem za maanguko ya Mlima Kilimanjaro lakini kutokana na sababu mbalimbali ikiwepo mabadiliko ya tabianchi maji yamepungua sana hivyo mifereji ya asili inahitajika kujengwa kwa zege kuhakikisha matumizi mazuri ya maji:-

Je, Serikali inasaidiaje kutatua changamoto hii?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO (MHE. OMARY T. MGUMBA) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anthony Calist Komu, Mbunge wa Jimbo la Moshi Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto za kilimo cha umwagiliaji katika Mkoa wa Kilimanjaro ikiwemo upungufu wa maji kutokana na mabadiliko ya tabianchi. Katika kukabiliana na changamoto hizo Serikali inatekeleza mradi wa kuendeleza skimu za wakulima wadogo (Small Scale Irrigation Development Project) ambapo hadi sasa imefanya ukarabati wa mifereji na miundombinu mingine ya umwagiliaji katika skimu Nane za Mkoa wa Kilimanjaro.

Mheshimiwa Naibu Spika, Skimu hizo ni skimu ya Mawala iliyopo Wilaya ya Moshi kwa gharama ya shilingi milioni 147, skimu ya Kikafuchini shilingi milioni 294, skimu ya Musamwinjanga shilingi milioni 275 na skimu ya Nsanya milioni 275 zilizoko Wilaya ya Hai. Skimu zingine ni skimu ya Mowonjamu Shilingi milioni 165 na skimu ya Kishisha Shilingi milioni 165 zilizoko Wilaya ya Siha, na skimu ya kivulini Shilingi milioni 125 na skimu ya kileo Shilingi milioni 216 zilizoko Wilaya ya Mwanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha kilimo cha umwagiliaji kinakuwa chenye tija Wizara kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji katika mwaka wa Fedha wa 2019/ 2020 imetenga kiasi cha shilingi milioni 412 kwa ajili ya ujenzi wa bwawa dogo la Orumwi lililoko Wilaya ya Siha litakalokuwa na mita za ujazo 58,000 na kutumika kuhifadhi maji ya kilimo cha umwagiliaji. Aidha, Wizara kupitia Tume ya Taifa ya Umwagiliaji imekamilisha ukarabati wa miundombinu ya skimu ya umwagiliaji ya Soko iliyoko Wilaya ya Moshi Vijijini. Ukarabati huu ulihusisha kusakafia mifereji ambapo utapunguza upotevu mkubwa wa maji uliokuwa ukitokea kabla ya ukarabati huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kukarabati skimu mbalimbali za umwagiliaji zilizoko nchini kama zilivyoainishwa kwenye mpango kabambe wa umwagiliaji wa mwaka 2018 – 2035, ambapo skimu za umwagiliaji za Mkoa wa Kilimanjaro zitaendelezwa na kukarabatiwa kutokana na mipango hiyo. (Makofi)
MHE. ANTONY C. KOMU aliuliza:-

Serikali imetekelza mradi wa maji katika Kata ya Mbokomu lakini maji mengi yanavuja barabarani na kusababisha kukosekana kwa maji maeneo mengi ya mradi kama vile vijiji vya Korini Kusini, Kiwalaa na Korini Kaskazini.

Je, kwanini Serikali isihakiki ukamilifu wa mradi huo na kufanya marekebisho ikiwa ni pamoja na kubainisha waliohusika na kasoro zitakazobainika na kuwachukuliwa hatua stahiki?
WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Antony Komu, Mbunge wa Moshi Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mradi wa maji Korini ni moja ya miradi ya maji katika vijiji sita iliyotekelezwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Moshi kupitia Awamu ya I ya program ya maendeleo ya sekta ya maji na ulikamilika tarehe 31 Julai, 2014 ukiwa unahudumia wananchi wapatao 10467 wa Vijiji vya Korini Juu, Korini Kati na Korini Kusini.

Mheshimiwa Spika, wakati mradi huu unaanza kutekelezwa kulikuwa na mradi wa maji wa zamani ambao ulikuwa unahudumia Kata hii ambayo ni mradi wa maji wa Mbokomu Mashariki na mradi wa maji wa Mbokomu Magharibi. Katika kipindi cha Septemba mwaka 2018 kulikuwa na ukarabati wa barabara kwenye Kata ya Mbokomu ambao ulisababisha bomba la maji la mradi wa zamani kuharibiwa na mtambo wa kutengeneza barabara na kusababisha maji kuanza kuvuja barabarani. Hata hivyo, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Moshi kwa kushirikiana na Mkandarasi wa barabara waliweza kukarabati na kumaliza tatizo la uvujaji maji barabarani kwa gharama ya shilingi milioni 1,437,000,000.
MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y. MHE. ANTONY C. KOMU) aliuliza:-

Shamba la miwa la TPC lina eneo lenye ukubwa wa zaidi ya hekta 6,000 ambalo halifai kwa kilimo cha miwa lakini zipo taarifa kiuwa wawekezaji wanataka kulitumia eneo hilo kuanzisha hifadhi ya wanyamapori:-

(a) Je, ni kwa nini Serikali inaruhusu mwekezaji huyo kuanzisha mradi tofauti kabisa?

(b) Je, ni kwa nini Serikali isitoe eneo hilo kwa wananchi wanaozunguka shamba hilo kwa ajili ya malisho ya mifugo yao?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anthony Calist Komu, Mbunge wa Jimbo la Moshi Vijijini, lenye sehemu (a) na (b), kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kampuni ya TPC ina takribani hekta 13,000 ambapo hekta 8,500 zimeendelezwa kwa kilimo cha miwa na eneo hekta 4,500 ambazo zipo kusini mwa Kiwanda cha TPC katika Vijiji vya Mawala na Mikocheni halina udongo wa kuwezesha kilimo cha miwa ya sukari kutokana na hali ya udongo kuwa na magadi. Tangu mwaka 1936 ambapo shamba hilo lilikuwa linamilikiwa na Serikali kabla ya ubinafsishwaji, eneo hilo la hekta 4,500 halikuwahi kulimwa zao lolote. Aidha, eneo hilo lilikuwa ni korido ya wanyamapori waliokuwa wakihama kutoka Tarangire kupitia Msitu wa Tembo kwenda hadi Ziwa Jipe. Ilipofika mwaka 2014 Serikali iliipatia Kampuni ya TPC leseni Na.1 ya kuanzisha shamba la wanyamapori (Certificate of Game Ranching) baada ya kukubali maoni ya TPC.

Mheshimiwa Spika, kutokana na maendeleo ya kazi za binadamu katika vijiji vilivyopo Kata ya Msitu wa Tembo wilaya ya Simanjiro, Vijiji vya Kahe, Mawala, Chemchem na Mikocheni Wilaya ya Moshi Vijijini vimesababisha korido hizo kuvunjika na wanyama kuendelea kuwepo katika maeneo hayo. Kwa hali hiyo, ili kuzuia uharibifu wa misitu na uwindaji holela wa wanyamapori, kiwanda cha TPC kilipewa leseni ya eneo hilo kwa ajili ya kuendeleza hifadhi ya mazingira ikiwemo misitu pamoja na wanyamapori waliomo katika eneo hilo. Aidha, ikumbukwe kwamba uamuzi huo wa Serikali ulizingatia umuhimu wa hifadhi ya maliasili iliyoko katika eneo hilo, pamoja na ukweli kuwa udongo katika eneo hilo usingeweza kutumika kwa kilimo hata kama sehemu hiyo ingekabidhiwa kwa wenyeji wa vijiji vinavyozunguka eneo hilo.