Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Dr. Godwin Oloyce Mollel (61 total)

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa bila malipo huduma za uzazi wa mpango na za afya kwa Wajawazito na Watoto chini ya umri wa miaka mitano kama Sera ya Afya inavyoelekeza?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ni mara ya kwanza kusimama hapa mbele, nitumie fursa hii kumshukuru Mungu, kushukuru Chama changu, kumshukuru Rais wetu kwa kutupa nafasi hii. Pia niwashukuru wananchi wa Jimbo la Siha kwa kuendelea kuniamini lakini nimshukuru mke wangu kwa kuendelea kunipa ushirikiano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Sera ya Afya ya mwaka 2007, ukurasa wa 19, kifungu 5.3.4 ambacho kinahusu Afya ya mama na mtoto na Tamko la Sera Kipengele (c) Sehemu ya (i), inaelekeza huduma bila malipo kwa Huduma za Afya ya Uzazi na Watoto chini ya miaka mitano. Baadhi ya maeneo wamekuwa wakifanya kinyume na tamko la kisera na hatua mbalimbali zimekuwa zikichukuliwa pale wananchi wanapotoa taarifa. Katika kipindi cha mwaka 2015-2020, Serikali ilitoa huduma kwa wenye uhitaji bila malipo likiwemo kundi hili zenye thamani ya bilioni 880.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hayo, Wizara inawaagiza Waganga Wakuu na Mikoa na Wilaya ambao ndiyo wasimamizi wakuu wa utekelezaji wa sera na miongozo ya afya katika ngazi ya mkoa na halmashauri kutimiza kikamilifu majukumu yao kwa kushughulikia haraka kero na malalamiko ya wananchi pia utekelezaji wa suala hili ambalo siyo tu ni tamko la kisera lakini pia ni utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambacho ndicho chama kilichounda Serikali. Ahsante.
MHE. HAWA M. CHAKOMA aliuliza:-

Je, ni kwa nini dawa za shinikizo la damu hazitolewi katika ngazi ya zahanati na vituo vya afya?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma,Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, dawa za kutibu shinikizo la damu zimegawanyika katika makundi kulingana na namna zinavyofanya kazi na athari zake,hivyo basi utoaji wake unazingatia utaalam na uwezo wa kitaaluma, ndiyo maana kuna dawa hutolewa katika ngazi za Zahanati, Vituo vya Afya, Hospitali za Wilaya, Hospitali za Rufaa na Hospitali ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha ushauri mzuri wa Mheshimiwa Mbunge unatekelezeka, Serikali ya Awamu ya Tano ikiongozwa na Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli imepeleka wataalam wengi wenye shahada ya udaktari mpaka ngazi ya kituo cha afya kwa lengo la kuhakikisha huduma nyingi na bora kama ulivyoshauriwa na Mheshimiwa Mbunge zinapatikana kuanzia ngazi ya chini na pia dawa hizi zimehusishwa katika mwongozo mpya wa matibabu nchini ili ziweze kutumika mpaka ngazi ya kituo cha afya na zahanati.
MHE. LUCY T. MAYENGA (K.n.y. MHE. MARIAM N. KISANGI) Aliuliza: -

Nchi yetu imekuwa na ongezeko kubwa la wagonjwa wa Afya ya Akili: -

(a) Je, nini chanzo cha ugonjwa huo?

(b) Je, Serikali ina utaratibu gani wa kuwasaidia wagonjwa hao?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Nassoro Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, afya ya akili ni ile hali ya mtu kuwa na uwezo wa kukabiliana na changamoto za kimaisha ikiwemo utambuzi, uzalishaji wa mali, kutunza familia na kumudu shughuli za kijamii. Magonjwa ya akili ni pale mtu anaposhindwa kukabiliana na changamoto za kimaisha ikiwa ni pamoja na kushindwa kumudu shughuli za kijamii, kujitunza, hisia na utambuzi ambapo sababu za magonjwa haya ni mchanganyiko wa sababu za kibaiolojia, kisaikolojia na kimazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na ongezeko la magonjwa haya, Serikali imefanya yafuatayo: -

(1) Kuandaa Sheria ya Afya ya Akili ya Mwaka 2008 ambapo sheria hii inatoa mwongozo na utaratibu wa namna ya kuwapokea na kuwahudumia watu wenye ugonjwa wa akili.

(2) Kuandaa Sera na miongozo ambapo wagonjwa wa afya ya akili ni miongoni mwa makundi maalum ambayo huduma zake zinaweza kutolewa kwa msamaha kwa watu ambao hawana uwezo.

(3) Serikali inahakikisha kuwa huduma hizi zinatolewa katika ngazi zote za huduma za afya kuanzia kwenye jamii, ngazi ya afya ya msingi, mkoa, kanda, mpaka hospitali maalum ya Taifa ya afya ya akili.

(4) Kuhakikisha upatikanaji wa dawa muhimu za afya ya akili kwenye vituo vyote vya huduma za afya.

(5) Kuongeza udahili wa wanafunzi wa uzamivu (Masters) katika masomo ya wagonjwa wa akili.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaipatia Hospitali ya Mkoa wa Iringa mashine ya CT-Scan?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa uwepo wa huduma za kibingwa za vipimo vya mionzi kwa kutumia CT-Scan. Katika kuzingatia umuhimu huu tayari ilishakamilisha kufunga mashine hizi kwenye Hospitali za Kibingwa Taifa, kanda na Hospitali mbili za Rufaa za Mikoa zilipata mashine hizi mnamo Desemba, 2020 ambazo ni Mwananyamala na Sekou Toure.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa zoezi hili ni endelevu, Serikali inaendelea kuziwezesha hospitali zingine zote za Rufaa za Mikoa ikiwemo Iringa kufunga mashine hizi kwa kadri ya upatikanaji wa rasilimali fedha za utekelezaji wa mpango huu.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA Aliuliza: -

Je, ni lini ujenzi wa wodi ya wazazi utaanza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christina Christopher, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga ni miongoni mwa Hospitali za Rufaa za Mikoa zinazoboreshwa. Napenda kumjulisha Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kwamba Mshauri Elekezi wa Ujenzi wa Wodi ya Wazazi ameshapatikana, ambaye ni Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Aidha, hatua inayoendelea hivi sasa, ni mchakato wa zabuni ya kupata mkandarasi atakayefanya kazi ya ujenzi, ambapo ujenzi huo unategemewa kuanza mwezi Machi, 2021. Mradi huu utatekelezwa kwa kutumia fedha za ndani.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA Aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua tatizo la hospitali ambazo zinaendelea kutoza fedha akinamama wanaojifungua kwa njia ya kawaida?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Sera ya Afya ya mwaka 2007, Ukurasa wa 19, kifungu 5.3.4 ambacho kinahusu afya ya mama na mtoto na Tamko la Sera Kipengele (c) Sehemu ya (i), inaelekeza kuhusu huduma bila malipo kwa Huduma za Afya ya Uzazi na Watoto chini ya miaka mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha mwaka 2015 - 2020 Serikali ilitoa huduma kwa wenye uhitaji bila malipo likiwemo kundi hili, zenye thamani ya shilingi takriban bilioni 880. Hivyo, Wizara inasisitiza watoa huduma wote kuzingatia utekelezaji wa tamko hili la kisera.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumtaarifu Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kuwa tayari Wizara imewaelekeza na kuwataka Waganga Wakuu wa Mikoa na Halmashauri ambao ndio wasimamizi wakuu wa utekelezaji wa Sera na Miongozo ya Afya katika ngazi ya Mikoa na Halmashauri kutimiza kikamilifu majukumu yao kwa kushughulikia haraka kero na malalamiko ya wananchi ikiwemo vituo vya kutolea huduma za afya kuacha kuwatoza fedha wajawazito na watoto wanapofika kituoni kupata huduma.
MHE. MAIDA HAMAD ABDALLAH Aliuliza: -

Pamoja na jitihada zinazofanywa na Serikali za kupambana na ugonjwa wa Malaria, bado ugonjwa huo unaendelea kuwaathiri wananchi wakiwemo watoto: -

Je, Serikali inaweza kutuambia hatua zilizofikiwa za kutokomeza ugonjwa huo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maida Hamad Abdallah, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau imekuwa ikitekeleza afua na kazi mbalimbali za kudhibiti ugonjwa wa malaria nchini na kufanikiwa kupunguza kiwango cha maambukizi ya Malaria kutoka zaidi ya asilimia 40 mwanzoni mwa miaka ya 2000 mpaka asilimia 7.5 mwaka 2017.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Wizara inatekeleza Mpango Mkakati wa Malaria (National Malaria Strategic Plan 2021 – 2025) ambao umeweka malengo ya kupunguza kiwango cha Malaria kutoka asilimia 7.5 mwaka 2017 hadi kufikia asilimia 3.5 ifikapo mwaka 2025. Lengo mahususi ni kutokomeza kabisa ugonjwa wa Malaria ifikapo 2030.
MHE. MWANTUMU M. ZODO Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukabiliana na upungufu wa Watumishi wapatao 16,000 kwenye Sekta ya Afya nchini?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantum Mzamili Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Tanga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya upungufu wa watumishi katika sekta ya afya ambayo kwa kiasi kikubwa hivi sasa imetokana na mahitaji mapya yanayotokana na ujenzi na upanuzi wa hospitali za rufaa za kanda, mikoa, ujenzi wa hospitali za Halmashauri, ujenzi na ukarabati wa vituo vya afya na zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kuwa, Serikali inachukua hatua mbalimbali kukabiliana na changamoto ya uhaba wa watumishi ambapo katika kipindi cha miaka mitano iliyopita 2015 hadi 2020 Serikali iliajiri watumishi wapatao 14,479 na zaidi ya watumishi 565 walipatiwa ajira za mkataba kwa kugharamiwa na makusanyo ya vituo vya kutolea huduma za afya. Pia katika mwaka wa fedha 2020/2021 sekta ya afya inatarajia kuajiri jumla ya watumishi wapya 12,476.
MHE. MARIAM M. NYOKA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuifanyia ukarabati mkubwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Ruvuma kwa kuwa ni ya muda mrefu na majengo yake yamechakaa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariamu Madalu Nyoka, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na ukarabati wa majengo chakavu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Ruvuma kwa kubomoa majengo chakavu manne; jengo la Masjala ya zamani, choo cha nje cha wagonjwa, jengo la viungo bandia na jengo la zamani la huduma za kifua kikuu, kwa ajili ya kujenga jengo la kisasa la wagonjwa wa dharura ambalo limefikia asilimia 95. Mradi huu unagharimu jumla ya shilingi 630,340,507.00, ambapo hadi sasa fedha hiyo imetolewa yote. Ujenzi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Oktoba, 2021. Ahsante.
MHE. JANETH E. MAHAWANGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wajasiriamali wadogo kupata Bima ya afya kupitia utaratibu wa vikundi ambao ulikuwa msaada mkubwa sana kwenye jamii?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Janeth Elias Mahawanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya inatoa kitita mahususi cha mafao kwa makundi maalum ya wajasiriamali ambao wamejirasimisha shughuli zao kupitia mwamvuli wa jumuiya au vyama vyao vilivyorasimishwa.

Mheshimiwa Spika, makundi ya wajasirimali yanayonufaika na utaratibu wa bima ya afya ni pamoja na makundi ya wakulima kupitia Vyama vya Ushirika 225 vyenye idadi ya wanachama 6,196; vikundi 17 vya umoja wa wamachinga; wajasiriamali wadogo; wachimbaji wa madini; wavuvi; na mamalishe ambavyo vina idadi ya wanachama 2,315; na vikundi vya umoja wa madereva bodaboda, malori na daladala ambavyo vina idadi ya wanachama 303.

Mheshimiwa Spika, kwa makundi ya wananchi ambao ni wajasiriamali lakini hawamo katika mwamvuli wa jumuiya za wajasiriamali zilizorasimishwa, Mfuko umeanzisha vifurushi vya bima ya afya vya hiari ambavyo vinazingatia umri, ukubwa wa familia, aina ya huduma na gharama halisi za matibabu nchini ambapo hadi tarehe 31 Machi, 2021 wanachama 32,343 wameshajiunga na mpango huu.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua umuhimu wa kuwa na Bima ya Afya kwa jamii na kwa kutambua matatizo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameainisha na Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakiyaainisha, Serikali inakamilisha Rasimu ya Muswada wa kutunga Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote ambayo itawasilishwa Bungeni mwezi Juni, 2021.
MHE. MARTHA N. GWAU aliuliza:-

Je, ni kiasi gani cha Zebaki kinaingizwa nchini kila Mwaka?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Nehemia Gwau, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2019 kiasi cha Zebaki kilichoingizwa nchini kilikuwa ni tani 24.42, ambapo mwaka 2020 kilikuwa ni tani 22.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kwamba zebaki ni kemikali inayotakiwa kudhibitiwa kwasababu ina madhara ya afya ya binadamu kama vile kusababisha upofu, kutetemeka viungo, kupoteza kumbukumbu, kuharibika ngozi, tatizo la ini na figo.

Mheshimiwa Spika, hivyo basi Serikali, kupitia Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali imeendelea kuchukua hatua za kudhibiti uingizaji wa Zebaki kwa kuwasajili wale wanaoingiza Zebaki nchini na kuchukua hatua kwa wale wanaokiuka sheria.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI aliuliza:-

Je, lini Jengo la Mama na Mtoto katika Hospitali ya Mawenzi litakamilika na kuanza kutoa huduma stahiki?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuena Athumani Bushiri, Mbuge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inaendelea na ujenzi wa jengo la kuwahudumia mama na mtoto ambalo kwa sasa ujenzi umefikia asilimia 70. Mradi huo unagharimu jumla ya shilingi bilioni 10.5 ambapo hadi sasa kiasi cha shilingi bilioni 5.3 kimetolewa na kutumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha wa 2021/2022, Serikali imetenga kiasi cha dhilingi bilioni 57 kwa ajili ya ukamilishaji wa miundombinu ya Hospitali za Rufaa za Mikoa, ikiwemo Hospitali ya Rufaa ya Mawenzi ambayo imetengewa kiasi cha shilingi bilioni 3.6 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi na shilingi bilioni 1.6 kwa ajili ya vifaa na vifaatiba. Aidha, huduma zitaanza kutolewa baada ya kukamilika kwa ujenzi na ukamilishaji usimikaji wa vifaa ifikapo Januari, 2022.
MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuanzisha utaratibu maalum wa kuvuna viungo vya binadamu kama vile figo na moyo kwa ajili ya Watanzania wenye uhitaji wa viungo hivyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose Cyprian Tweve Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Hospitali ya Taifa Muhimbili na Hospitali ya Benjamin Mkapa zimeanza kutoa huduma ya uvunaji na upandikizwaji wa figo nchini tangu mwezi Novemba, 2017 kutoka kwa wachangiaji walioridhia. Hadi sasa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili imepandikiza figo 62 na Hospitali ya Benjamin Mkapa imepandikiza figo 18. Aidha, kwa upande wa upandikizaji wa moyo, Serikali inaendelea kujenga uwezo wa ndani wa kutoa huduma hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya upandikizaji wa viungo nchini kama ambavyo Mbunge ameainisha, Serikali imeandaa Muswada wa Kutunga Sheria itakayoongoza taratibu za uvunaji, utunzaji na upandikizaji wa viungo ambayo ipo kwenye hatua ya ukusanyaji wa maoni kutoka kwa wadau. Hata hivyo, kwa kuwa huduma zimeanza kutolewa, kwa sasa nchi inatumia miongozo ya kimataifa inayosimamia uvunaji na upandikizaji wa viungo.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE aliuliza:-

Mwaka 2018 KFW Germany walisitisha udhamini kwa huduma za Afya kwa Mama na Mtoto Mkoani Tanga: -

(a) Je, ni juhudi gani zimefanyika kuhakikisha Mdhamini huyo anaendelea na udhamini wake Mkoani Tanga?

(b) Je, Serikali ina mpango gani kupata Mdhamini mwingine?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Eng. Mwanaisha Ng’anzi Ulenge, Mbunge Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Ujerumani kupitia Benki ya KFW ilianzisha mpango wa Bima ya Afya kwa akinamama wajawazito na watoto. Mpango huo ulitekelezwa kwa makubaliano ya kipindi maalum toka 2012 hadi 2018. Mpango huo umechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza uelewa wa dhana na umuhimu wa kuwa na Bima ya Afya katika jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali inakamilisha Rasimu ya Muswada wa kutunga Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote ambao utawasilishwa Bungeni mwezi Juni 2021, swali la Mheshimiwa Mbunge lenye kipengele (a) na (b) litaenda kupata suluhisho. Hata hivyo, Serikali inaendelea kuwahamasisha wadau mbalimbali katika kuchangia miradi ya Sekta ya Afya, ikiwemo Bima ya Afya kwa Wote.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itamaliza ujenzi wa Hospitali ya Rufaa Katavi kwani ujenzi huo unakwenda kwa kusuasua?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Mpanda Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inaendelea na ujenzi wa Hospitali ya Mkoa wa Katavi ambapo kwa sasa ujenzi umekamilika kwa wastani wa asilimia 70. Ujenzi kwa upande wa maabara umefikia asilimia 98 na jengo kuu la hospitali umefikia asilimia 42. Mradi huo unagharimu jumla ya shilingi bilioni 9.82 ambapo hadi sasa kiasi cha shilingi bilioni 3.97 kimetolewa na kutumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha wa 2021/2022, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 57 kwa ajili ya ukamilishaji wa miundombinu ya Hospitali za Rufaa za Mikoa, ikiwemo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Katavi, ambapo kiasi cha shilingi bilioni 5.85 zitatumika kukamilisha ujenzi huu ifikapo Januari 2022.
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itamaliza ujenzi wa Hospitali ya Mkoa wa Katavi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa hospitali ya Mkoa wa Katavi umekamilika kwa wastani wa asilimia 70, ambapo ujenzi kwa upande wa maabara umefikia asilimia 98 na jengo kuu la hospitali umefikia asilimia 42. Mradi huu unagharimu jumla ya shilingi bilioni 9.82 ambapo hadi sasa kiasi cha shilingi bilioni 3.97 zimetumika na bilioni 5.85 zimetengwa katika bajeti ya mwaka 2021/2022 na zitatumika kukamilisha ujenzi huu ifikapo Januari, 2022. Ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO aliuliza:-

Je, ni nini mpango wa Serikali wa kukamilisha Mradi wa Jengo la Mama na Mtoto katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro ya Mawenzi ambao umeanza tangu mwaka 2008/2009 bila kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa niaba ya Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini kama ifuatavyo;-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa jengo la kuwahudumia mama na mtoto katika Hospitali ya Mawenzi umekamilika kwa asilimia 70. Mradi huo unagharimu jumla ya shilingi bilioni 10.5 ambapo hadi sasa kiasi cha shilingi bilioni 5.3 kimetolewa na kutumika.

Aidha, kiasi cha shilingi bilioni 5.2 kimetengwa kwa mwaka 2021/2022 ambapo kati ya fedha hizo, shilingi bilioni 3.6 zitatumika kukamilisha ujenzi na kiasi cha shilingi bilioni 1.6 kitatumika kununulia vifaa tiba na ujenzi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo Januari, 2022.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaandaa utaratibu mzuri wa matibabu kwa watu wenye ulemavu wakati ikisubiri Bima ya Afya kwa wote?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL). alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Ikupa Alex Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka utaratibu wa kuwatambua watu wenye ulemavu kupitia Kamati za Watu Wenye Ulemavu kuanzia ngazi ya kijiji na kuwaunganisha kwenye vituo vyetu vya kutolea huduma za afya kulingana na mahitaji yao. Aidha, kupitia mipango kabambe ya afya ya halmashauri Serikali imeendelea kuwatengea rasilimali kulingana na mahitaji yao. Mfano kwa walemavu wa ngozi wanawezeshwa mafuta ya kuzuia jua (Sun Cream) ambayo kwa sasa hutengenezwa katika Hospitali ya Kanda ya KCMC, na bidhaa hii imeingizwa kwenye orodha ya bidhaa za afya zinazosambazwa na Bohari ya Dawa (MSD).

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imetoa miongozo ya miundombinu ya kutolea huduma kwa kuzingatia haki za watu wenye ulemavu. Pia, Wizara imeendelea kutengeneza miongozo na mafunzo kwa watoa huduma ili kuwezesha na kuboresha utoaji wa huduma kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mswada wa Bima ya Afya kwa Wote unakuja, hii ni fursa muhimu sana kwa sisi Wabunge kutengeneza sheria nzuri zitakazolinda haki za watu wenye ulemavu. Ahsante.
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawapatia wazee hasa wa vijijini bima ya afya ikiwemo ya CHF inayotolewa na Halmashauri?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shamsia Azizi Mtamba, Mbunge wa Mtwara Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, huduma za tiba ni haki ya msingi ya wazee wote. Serikali imeendelea kuimarisha upatikanaji wa matibabu hususan kwa wazee wasiojiweza nchini kwa kuanzisha madirisha kwa ajili ya matibabu kwa wazee. Serikali imeendelea na zoezi la utambuzi wa wazee na kuwapatia vitambulisho vya matibabu. Hadi kufikia Machi, 2021 jumla ya wazee 2,344,747 wametambuliwa sawa na asilimia 87 ya makadirio ya wazee wote nchini. Kati yao wanaume ni 1,092,310 na wanawake ni 1,252,437. Aidha, wazee wasio na uwezo 1,087,008 na wamepatiwa vitambulisho vya matibabu bure na wazee 856,052 wamepatiwa kadi za matibabu za Afya ya Jamii yaani CHF.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na kukamilisha rasimu ya Muswada wa Bima ya Afya kwa Wote ili kuwezesha wananchi wote wakiwemo wazee kupata huduma za matibabu bila kikwazo cha fedha kwa mfumo rasmi na ulio mzuri zaidi. Ahsante.
MHE. HASSAN S. MTENGA aliuliza: -

Majengo mengi katika Hospitali ya Mkoa wa Mtwara yamechakaa; je, ni lini Serikali itaanza ukarabati wa Hospitali ya Mkoa wa Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto naomba kujibu swali la Hassan Seleman Mtenga, Mbunge wa Mtwara mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mtwara - Ligula ni moja kati ya Hospitali za muda mrefu hapa nchini ambazo miundombinu yake imechakaa sana. Katika jitihada za kuboresha miundombinu ya Hospitali hiyo, kwenye bajeti ya 2020/2021 kiasi cha shilingi milioni 201 kimetolewa kwa ajili ya ukamilishwaji wa jengo la kuhifadhia maiti ambalo ujenzi wake umekamilika na vifaa vimenunuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 kiasi cha shilingi bilioni moja kimetengwa kwa ajili ya ukarabati wa Majengo ya Wagonjwa wa Nje (OPD), wodi za wanaume na wanawake, upasuaji, wodi ya uangalizi maalum na kichomea taka. Ukarabati huo unatarajiwa kukamilika Machi, 2022. Ahsante.
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati Hospitali ya Wagonjwa wa Afya ya Akili ya Mirembe ambayo Miundombinu yake imeharibika?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Alice Karungi Kaijage, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kumtumia Wakala wa Majengo (TBA) imeanza upembuzi yakinifu wa majengo yatakayofanyiwa ukarabati pamoja na yale yatakayobomolewa na kujengwa upya. Aidha, kupitia upembuzi huo Serikali itabaini gharama halisi za ujenzi na
ukarabati wa Hospitali hiyo. Kazi hii inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Oktoba, 2021.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, ni lini Hospitali ya Kanda ya Kusini itaanza kutoa Huduma kwa Wananchi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) alijibu: -

Mheshimiwa Spika ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Mlapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Kanda ya Kusini Mtwara imewekewa jiwe la msingi tarehe 26/07/2021 na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango na huduma zimeanza tarehe 1 Oktoba, 2021. Ahsante.
MHE. AGNES E. HOKORORO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutafuta teknolojia mbadala ili kunusuru afya za wananchi wanaotumia zebaki kwa matumizi mbalimbali?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Agnes Elias Hokororo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kushirikiana na taasisi zake, ipo kwenye mpango wa kutafuta teknolojia mbadala na tayari vikao vya pamoja na taasisi zinazohusika na uchimbaji wa dhahabu vinafanyika ili kupata teknolojia isiyohitaji zebaki katika uchenjuaji wa dhahabu na hivyo kuondoa athari za kiafya kwa jamii na mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa elimu juu ya matumizi sahihi, kupunguza na hatimaye kuondoa kabisa katika siku za usoni matumizi ya zebaki ni dhamira ya Serikali katika kulinda afya ya jamii na mazingira. Ahsante.
MHE. HALIMA J. MDEE aliuliza: -

(a) Je, tangu janga la Corona lianze ni Watanzania wangapi wamepata maambukizi; wangapi wamekufa; na wangapi wamepona?

(b) Je, ni fedha kiasi gani zimetengwa na Serikali na zimefanya nini na wapi katika kukabiliana na janga hili?

(c) Je, nini kinapelekea gharama za kupima Covid- 19 kuwa kubwa na ni dawa gani zilizofanyiwa uchunguzi na kuthibitishwa kuwa zina uwezo wa kuzuia au kutibu Covid-19?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Halima James Mdee, Mbunge wa Viti Maalum, lenye vipengele (a), (b) na (c), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zimeathirika na mlipuko wa Ugonjwa wa Covid-19. Hadi kufikia tarehe 25 Oktoba 2021, idadi ya Watanzania 26,164 ndio waliothibitika kuwa na maambukizi. Kati ya hao, 725 walifariki na 25,330 walipona.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, takribani kiasi cha shilingi bilioni 158 zimetumika kununua vifaa mbambali ikiwemo mitambo 19 ya kuzalisha hewa ya oxygen yenye uwezo wa kuzalisha mitungi 200 hadi 300 ambapo mitambo saba tayari imeshasimikwa na 12 ipo katika hatua ya usimikaji. Fedha nyingine zilinunua PPE, dawa, vifaa, vifaa tiba, vitendanishi pamoja na magari 105 ya kubebea wagonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, Sekta ya Afya imepokea kiasi cha shilingi bilioni 466.78 ambazo zitatumika katika kupambana na Uviko-19 ikiwemo kujenga na kusimika vifaa katika majengo ya matibabu ya dharura (EMD) 115, ujenzi wa wodi za uangalizi maalum (ICU) 67, ununuzi wa magari 253 ya kubebea wagonjwa, magari nane ya damu salama, usimikaji wa mitambo 10 ya kuzalisha hewa ya oxygen, vitanda 2,700 kwenye vituo 225 vya kutolea huduma za afya, kununua na kusimika mashine 95 za X-Ray, CT-Scan 29, mashine 4 za MRI pamoja na kufanya tafiti sita kuhusu tabia za virusi vya korona.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama halisi ya kumpima mgonjwa mmoja ni Dola 135 na Serikali sasa inatoza Dola 50. Hivyo Serikali inachangia Dola 85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti mbalimbali zimefanyika duniani kuhusu dawa, ila hadi sasa dawa zilizopo zinatumika kutibu tu madhara yatokanayo na virusi. Hata hivyo kilichothibitika kwa sasa kusaidia kuondoa vifo ni chanjo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
MHE. REGINA N. QWARAY aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kusimamia kikamilifu Sera ya Afya ili akinamama wajawazito na watoto wasitozwe gharama katika vituo vya afya?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Regina Ndege Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, licha ya kuwepo kwa sera na miongozo inayotaka huduma itolewe bure, kumekuwepo na malalamiko ya baadhi ya wananchi walio katika makundi hayo katika maeneo mbalimbali kudaiwa fedha katika vituo vya umma vya kutolea huduma. Ili kuepukana na malalamiko hayo, Serikali inawaagiza Waganga Wakuu wa Mikoa, Waganga Wakuu wa Wilaya, Bodi za Afya na watoa huduma za afya kutekeleza Sera na miongozo inayohusu matibabu bure kwa mama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali inawakumbusha Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakurugenzi kuwa ni jukumu lao pia kusimamia miongozo inayotolewa na Serikali. Ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Wodi za Wagonjwa wenye matatizo ya Ubongo na Akili katika Hospitali za Temeke, Amana na Mwananyamala?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, lakini vilevile kumshukuru Rais wetu kwa kuendelea kutuamini mimi na Mheshimiwa Ummy Ali Mwalimu kusimamia Wizara ya Afya kwa niaba yake Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Nassoro Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Rufaa ya Temeke ipo katika mchakato wa kukarabati jengo lililokuwa likitumika kwa wagonjwa wa kisukari ili liweze kutumika kwa ajili ya kulaza wagonjwa wa akili. Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala imetenga kiasi cha shilingi milioni mia mbili kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la wodi ya wagonjwa wa akili. Pia, Hospitali ya Rufaa ya Amana kwa kuwa ujenzi huo upo kwenye mpango mkakati wa miaka mitano wameelekezwa kutenga bajeti ya ujenzi wa jengo la afya ya akili katika bajeti ya mwaka 2022/2023. Ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA Aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua changamoto ya upungufu wa Madaktari Bingwa na vifaa tiba katika Hospitali ya Rufaa ya Kitete Mkoani Tabora?
NAIBU WAZIRI WA AFYA Alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Rufaa Kitete ina Madaktari Bingwa watatu wanaotoa huduma ya wanawake na watoto. Pia, Serikali imetoa ufadhili wa masomo kwa Madaktari sita wa hospitali hii ambao wanasomea fani mbalimbali za kibingwa; fani hizo ni Wanawake na Afya ya Uzazi mmoja, Masikio, Pua na Koo mmoja, Magonjwa ya Ndani wawili, Huduma za Dharura mmoja na Mionzi (Radiolojia) mmoja. Madaktari hao wanatarajiwa kuhitimu mwaka wa masomo 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imetoa jumla ya Shilingi Bilioni 10.5 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la wagonjwa mahututi (ICU) pamoja na vifaa vyake, jengo la huduma ya mama na mtoto, jengo la dharura (EMD) pamoja na vifaa vyake na ununuzi wa CT-Scan Pamoja na jengo lake ambapo shughuli hizo zote zimeanza.
MHE. LUHAGA J. MPINA K.n.y. MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza: -

Mwaka 2018 Mkoa wa Simiyu ulitenga eneo kwa ajili ya ujenzi wa Kiwanda cha Kuzalisha Vifaa Tiba vitokanavyo na malighafi ya pamba na utaratibu wa kuanza ujenzi umeshakamilika, lakini kibali cha ujenzi toka Serikali kuu kimechukua muda mrefu.

Je, ni lini Serikali itatoa kibali kuruhusu ujenzi kuanza?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Midimu, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia mifuko ya WCF na NHIF ilipanga kujenga kiwanda cha kuzalisha vifaa tiba vinavyotumia malighafi ya pamba chenye thamani ya shilingi bilioni 59.4. Wakati wa upembuzi yakinifu wa awali ilionekana kutumia miundombinu tuliyonayo, kiwanda hicho kinaweza kujengwa kwa shilingi bilioni 8.4 na kuokoa shilingi bilioni 51.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tathmini ya mwisho inamalizika mwishoni mwa mwezi wa pili ili kukutanisha mifuko husika na Serikali ya Mkoa wa Simiyu kupeana mwelekeo.
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE aliuliza: -

Je, Serikali imejipangaje katika kupunguza ama kumaliza kabisa changamoto ya ukosefu wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Alice Karungi Kaijage, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imepeleka Bohari ya Dawa (MSD) shilingi bilioni 333.8 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba ambapo sasa Bohari ya Dawa ipo katika hatua mbalimbali za manunuzi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kupeleka fedha kwa ajili ya manunuzi, Serikali imetoa shilingi bilioni 18 kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda cha dawa eneo la Idofi, Mkoani Njombe ambacho kitakuwa na uwezo wa kuzalisha vidonge ndani ya siku mbili vya kutosha nchi nzima kwa miezi mitatu na ujenzi umefikia 70%. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiwanda cha kuzalisha gloves kilichopo Njombe kimekamilika kwa asilimia 100 na sasa kipo kwenye majaribio; na kikikamilika kitaweza kukidhi mahitaji ya nchi kwa 85%. Aidha, kiwanda cha Keko kimefufuliwa na kinazalisha kwa sasa aina 12 za dawa. Ahsante. (Makofi)
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA K.n.y. MHE. KABULA E. SHITOBELA aliuliza: -

Je, Serikali imefikia wapi kuhusu kufanya uchunguzi ili kujua chanzo cha ugonjwa wa saratani katika Mkoa wa Mwanza na Kanda ya Ziwa na ina mpango gani wa kudhibiti ongezeko la ugonjwa huo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabula Enock Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum lenye vipengele (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali imeshafanya utafiti wa kina nchi nzima uliosaidia kutambua kuwa Kanda ya Ziwa ni saratani zipi zinaongoza ambazo ni saratani ya kibofu cha mkojo, saratani ya mji wa uzazi wa kinamama, saratani ya damu, macho na figo. Aidha, wataalamu wamekusanya sampuli za damu za watu 7,000 ambao hawana saratani ili kulinganisha na sampuli za damu za wenye saratani. Utafiti huu utasaidia kubaini chanzo cha hizo saratani. Hivyo, kwa sasa bado utafiti unaendelea na visababishi vinavyosemwa bado ni nadharia tu kutokana na shughuli za kijamii katika maeneo husika.

(b) Mheshimiwa Spika, hadi sasa mpango wa kudhibiti ongezeko umejikita katika kutoa elimu ya afya kwa viashiria vinavyodhaniwa pamoja na kuzingatia mkakati wa kitaifa kwenye maeneo saba yaliyoainishwa ili kudhibiti viashiria vya saratani. Ahsante.
MHE. NEEMA W. MGAYA aliuliza: -

(a) Je, ni kwa nini Serikali iliifuta iliyokuwa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA)?

(b) Je, Serikali haioni kwa kuifuta TFDA itashindwa kudhibiti ubora wa vyakula ipasavyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) ilifutwa kwa kufuatia kupitishwa kwa Sheria ya Fedha Na. 8 ya mwaka, 2019 iliyohamishia majukumu ya udhibiti wa chakula na vipodozi kutoka TFDA kwenda Mamlaka ya Udhibiti wa Viwango (TBS). Lengo la kuhamisha majukumu haya ilikuwa ni kuondoa mwingiliano wa majukumu, kati ya TFDA na TBS na kuweka mazingira wezeshi ya uendeshaji wa biashara nchini.

(b) Serikali imeendelea kudhibiti ubora wa chakula kupitia Taasisi ya Viwango Nchini (TBS). Aidha, wataalam wa chakula waliokuwa TFDA pamoja na vifaa vya maabara vya uchunguzi wa ubora wa chakula vilivyokuwa vinatumika TFDA vilihamishiwa TBS ikiwa ni pamoja na shughuli zote zinazohusiana na udhibiti wa ubora wa chakula. Hivyo, kufutwa kwa TFDA hakuwezi kuathiri usimamizi wa ubora wa chakula nchini. Ahsnate. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO K.n.y. MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza kuharakisha utoaji wa matokeo ya tafiti za ndani za tiba asilia za kutibu maradhi mbalimbali kama inavyofanya kwenye tafiti za nje ya nchi kwa kuziundia Tume ya Jopo la Wachunguzi mapema?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Kembaki Michael, Mbunge wa Tarime Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikitoa taarifa za utafiti mbalimbali zinazohusiana na dawa za asili zilizofanywa kupitia Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) zinazolenga kuonyesha ufanisi na usalama wa dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha kuanzia mwezi Aprili mpaka Septemba 2021, Wizara ya Afya kwa kushirikiana na taasisi ya NIMR, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Hospitali ya Benjamin Mkapa, Hospitali ya Rufaa ya Kanda Bugando, Hospitali ya Rufaa ya Kanda KCMC, zilitekeleza utafiti wa ufuatiliaji wa ufanisi wa dawa saba za asili zilizosajiliwa na Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala kwa lengo la kupambana na maambukizi ya UVIKO-19. Matokeo ya utafiti huu yalitolewa na kutangazwa kwa umma kupitia vyombo vya habari mbalimbali. Ahsante. (Makofi)
MHE. JACQUELINE K. ANDREA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Hospitali ya Kanda ya Magharibi kama ilivyoainishwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Kainja Andrea, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia Ilani ya Chama cha Mapinduzi, Serikali kupitia Wizara ya Afya imetenga fedha za ujenzi wa Hospitali ya Kanda ya Magharibi kwa mwaka wa fedha 2022/2023 na tayari kazi ya kuandaa michoro ya hospitali hiyo imeshaanza na upembuzi yakinifu wa eneo ambalo itajengwa kwa kuzingatia ukaribu wa wananchi wote katika mikoa inayounda Kanda ya Magharibi. Ahsante. (Makofi)
MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza: -

Je ni lini Serikali itakabidhi majengo yaliyokuwa ya Hospitali ya Muhimbili kwa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo ili kupunguza uhaba wa majengo katika Hospitali hiyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Muharami Shaban Mkenge, Mbunge wa Bagamoyo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba majengo hayo yanayomilikiwa na Chuo Kikuu cha Afya Kishiriki cha Muhimbili (MUHAS) na chuo kimekuwa kikiyatumia majengo hayo kwa ajili ya mafunzo ya vitendo kwa wanafunzi wake.

Mheshimiwa Spika, aidha, Chuo kikuu MUHAS bado kina mipango ya uendelezaji na upanuzi wa eneo hilo ili kutimiza majukumu yake, katika kuzalisha wataalam wa afya nchini.

Mheshimiwa Spika: Serikali tayari imepeleka fedha shilingi milioni 300 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la huduma za dharura kwenye Hospitali ya Bagamoyo na hivyo naomba majengo ya Chuo Kikuu MUHAS yaendelee kutumika kwa shughuli za ufundishaji na utafiti kwa wanafunzi wa Chuo cha MUHAS. Hata hivyo uwepo wa Chuo cha MUHAS ni fursa kwa ukuaji wa Hospitali ya Bagamoyo na ni fursa kwa watu wa bagamoyo kitiba na kiuchumi. Ahsante sana.
MHE. KASSIM HASSAN HAJI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kuongeza maduka ya kutolea dawa kwa kutumia Bima ya Afya ili kuondoa usumbufu wanaopata wananchi wa Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassim Hassan Haji, Mbunge wa Mwanakwerekwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba idadi ya maduka na vituo vinavyotoa huduma za Bima ya Afya Zanzibar ni vichache ambapo kwa kipindi cha miezi sita kuanzia Juni, 2021 hadi Desemba 2021 idadi ya vituo vimeongezeka kutoka 19 hadi 65.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuhamasisha wamiliki wa vituo vya kutolea huduma za afya na maduka ya dawa kujiunga na huduma ya bima ili kuwafikia wananchi wote. Ahsante.(Makofi)
MHE. MWANTUMU DAU HAJI aliuliza: -

Je, ni kwa nini ugonjwa wa TB hauwezi kuonekana kwa mara moja unapompata mwathirika?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ugonjwa wa TB huchelewa kuonekana kutokana na tabia na mwenendo na vimelea vya TB kuzaliana taratibu mwilini na mara nyingi hudhibitiwa na kinga ya mwili wa aliyeambukizwa. Hivyo kila mgonjwa ataanza kuonesha dalili za ugonjwa kutegemea hali ya kinga ya mwili wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa wito kwa wananchi kuwahi mapema katika vituo vya kutolea huduma za afya kupimwa mara tu wanapojisikia dalili zifuatazo; homa za mara kwa mara, kikohozi cha wiki mbili au zaidi, kutoa makohozi yaliyochanganyika na damu, kupungua uzito kwa haraka bila sababu ya msingi na kutokwa jasho jingi hasa usiku. Aidha, ninashauri jamii iwe na utaratibu wa kupima afya mara kwa mara ili kutambua magonjwa mapema na hatimaye kuanza matibabu mapema. Ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI K.n.y MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza: -

Je, Serikali haioni haja ya kufanya utafiti wa chanzo cha watoto wachanga kugeuka njano baada ya kuzaliwa na Mama kuishiwa nguvu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Nassoro Kisangi Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti nyingi zimefanyika Kitaifa na Kimataifa kujua chanzo cha watoto wachanga kugeuka njano mara baada ya kuzaliwa. Tafiti hizo zimeonyesha kuwa hali ya umanjano inayotokea ndani ya masaa 24 baada ya kuzaliwa inaonyesha tatizo la kiafya (Pathological) na linahitaji kutambua sababu na kutoa tiba stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo likitokea baada ya masaa 24, mara nyingi linatokana na sababu za kawaida za mwili wa mtoto kupunguza chembechembe nyekundu nyingi alizokuwa nazo tumboni kwa Mama, hata hivyo hili pia uchunguzi wa kina ni muhimu ili kujihakikishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la utafiti ni muhimu na ni suala endelevu katika afya. Ahsante.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka Madaktari Bingwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Rukwa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziriwa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Rukwa hadi sasa ina jumla ya Madaktari Bingwa watano wa fani za afya kama ifuatavyo; mama na uzazi wawili, magonjwa ya watoto wawili pamoja na madaktari bingwa wa magonjwa ya ndani (physician) mmoja. Katika kuongeza idadi ya madaktari bingwa, Wizara imepeleka kusoma jumla ya madaktari watano kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Rukwa, ambao ni madaktari wawili wanasomea upasuaji, daktari mmoja anaesomea upasuaji wa mifupa, daktari mmoja anasomea magonjwa ya dharula na daktari mmoja anaesomea kinywa, sikio na koo, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA aliuliza: -

Je, nini chanzo cha vifo kwa akinamama wanaojifungua kwa njia ya upasuaji siku chache baada ya upasuaji?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christina Christopher Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ufuatiliaji wa vifo vitokanavyo na uzazi uliofanywa na Wizara ya Afya kuanzia mwaka 2018 hadi 2021 umeonesha kuwa vifo ambavyo vilisababishwa na matatizo ya dawa za ganzi (nusu kaputi) na upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni ni 58 yaani 3.3% mwaka 2018; vifo 80 yaani 4.8% mwaka 2019; vifo 65 yaani 4.0% mwaka 2020; na vifo 65 yaani 4.1% mwaka 2021.

Mheshimiwa Spika, sababu kuu za vifo hivi ni nne ambazo ni ajali ya dawa za ganzi/nusu kaputi, kupoteza damu wakati au baada ya upasuaji, tatizo la damu kuganda na maambukizi ya bakteria baada ya upasuaji.

Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na vyama vya kitaaluma inatekeleza mkakati wa kuwajengea uwezo watumishi wa vituo vya huduma za afya kuanzia ngazi ya zahanati hadi hospitali za Taifa katika eneo la utoaji ganzi (nusu kaputi) na upasuaji kwa usalama kwa kuzingatia miongozo ya Wizara ya Afya. Ahsante.
MHE. IDRISSA JUMA ABDUL-HAFAR aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupambana na visababishi vya maradhi yasiyoambukiza?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Idrissa Juma Abdul-Hafar, Mbunge wa Jimbo la Mtoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga shilingi milioni 725 kwa ajili ya kutekeleza Mpango Mkakati wa Tatu wa Kitaifa wa Kuzuia na Kudhibiti Magonjwa Yasiyoambukiza (2021 – 2026) ambao umeainisha mikakati mahsusi ya udhibiti wa visababishi vya magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo:-

(1) Kuimarisha uratibu na ushirikishwaji wa sekta mtambuka;

(2) Kuimarisha miundombinu ya utoaji wa huduma;

(3) Kuwajengea uwezo watumishi katika kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza;

(4) Kuimarisha na kusimamia shughuli za utafiti; na

(5) Kuhamasisha wananchi kuhusu njia za kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza.

Njia hizi ni pamoja na kufanya mazoezi, pamoja na kuzingatia kanuni bora za lishe.
MHE. TECLA M. UNGELE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kupeleka Madaktari Bingwa wa Magonjwa ya Ndani na Mifupa katika Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Lindi?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tecla Mohamed Ungele, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hadi sasa Hospitali ya Rufaa ya Lindi ina jumla ya Madaktari Bingwa watano ambao ni Daktari Bingwa wa Upasuaji mmoja, Madaktari Bingwa wa Afya ya Uzazi na Mtoto wawili, Daktari Bingwa wa Mionzi mmoja na Daktari Bingwa wa Dawa za Usingizi mmoja.

Mheshimiwa Spika, katika kuongeza idadi ya Madaktari Bingwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi, Wizara imepeleka kusoma jumla ya Madaktari saba, ambao Madaktari wawili wanasomea Udaktari Bingwa wa Watoto, Madaktari wawili Ubingwa wa Upasuaji, Daktari mmoja Ubingwa wa Mionzi, Daktari mmoja Ubingwa wa Mifupa na Daktari Bingwa wa Afya ya Uzazi na Watoto mmoja.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Ndani, Serikali inakamilisha taratibu za uhamisho ili kumpeleka Hospitali ya Lindi. Ahsante.
MHE. NANCY H. NYALUSI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya uhaba wa madaktari bingwa katika Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Iringa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nancy Hassan Nyalusi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa hadi sasa ina jumla ya madaktari bingwa kumi na moja. Madaktari bingwa wa afya ya akina mama na uzazi wanne, madaktari bingwa wa upasuaji wawili, daktari bingwa wa magonjwa ya ndani mmoja, madaktari bingwa wa watoto wawili, daktari bingwa wa macho mmoja na daktari bingwa wa mionzi mmoja.

Mheshimiwa Spika, katika kuongeza idadi ya madaktari bingwa, Wizara imepeleka kusoma jumla ya madaktari kumi na mbili kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Iringa, ambapo madaktari wawili wanasomea


kinywa, sikio na koo, madaktari bingwa wa mifupa wawili, daktari wa magonjwa ya dharura mmoja, madaktari bingwa wa watoto wawili, madaktari bingwa wa magonjwa ya ndani wawili, daktari bingwa wa meno mmoja, daktari bingwa wa usingizi mmoja na daktari bingwa mbobezi wa masuala ya watoto mmoja. Ahsante.
MHE. GHATI Z. CHOMETE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuimarisha huduma za afya zikiwemo dawa muhimu katika hospitali zetu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ghati Zephania Chomete, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha na kuimarisha upatikanaji wa huduma za afya nchini kwa kuboresha miundombinu ikiwemo kuweka vifaa tiba vya kisasa, kuajiri wataalam wa afya pamoja na kuwapandisha madaraja ili kuongeza morali ya kuendelea kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga bajeti ya shilingi bilioni 200 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba na hadi kufikia tarehe 30 Oktoba, 2022, Serikali imekwisha toa jumla ya shilingi bilioni 74.3 kwa ajili ya manunuzi ya dawa na vifaa tiba ili kuimarisha upatikanaji wake katika ngazi zote za utoaji wa huduma za afya nchini. Ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO aliuliza: -

Je, kuna Wataalam wangapi wa huduma za utengamano na mazoezi ya viungo physiotherapist katika Mkoa wa Morogoro?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Morogoro una jumla ya wataalam 15 kati ya 30 wanaohitajika wa huduma za utengamao na mazoezi ya viungo ambapo Kilosa kuna mtaalam mmoja, Hospitali ya Rufaa Morogoro kuna wataalam wanne, Mvomero mtalaam mmoja, Ifakara Hospitali wanne na Mzinga Hospitali wataalam watano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha watalaam tisa wa huduma za utengamao wameombewa kibali cha ajira katika bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE aliuliza: -

Je, Serikali imejipangaje katika kupambana na changamoto ya upungufu wa Wataalam wa Mazoezi Tiba na huduma ya Utengamao nchini?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Alice Karungi Kaijage, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeajiri jumla ya wataalam 84 wa mazoezitiba na huduma mtengamao katika ajira za mwezi Julai, 2022. Hata hivyo, kufanya idadi ya wataalam wa mazoezitiba na huduma mtengamao kuongezeka kutoka 653 hadi 737.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa kuna jumla ya vyuo vikuu vinne ambavyo ni Muhimbili, KCMC, Bugando na Zanzibar vinavyotoa taaluma, hivyo kupunguza changamoto ya uwepo wa wataalam katika soko la ajira.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA aliuliza: -

Je, kuna utafiti wowote ambao umefanyika ili kubaini dawa za ganzi/nusu kaputi zinazosababisha vifo kwa wanaojifungua kwa upasuaji?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christina Christopher Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tafiti mbalimbali zilizofanyika zinaonesha kuwa sababu zimegawanyika katika makundi matatu:-

(a) Sababu za vinasaba (DNA);
(b) Sababu zinazohusiana na ganzi ila siyo za moja kwa moja; na
(c) Sababu zenye mahusiano ya moja kwa moja na ganzi.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, vifo vya namna hii hutokea mara chache sana na ndiyo maana wakati wote tunawashauri akinamama wajawazito kuhudhuria kliniki ili kutoa muda wa kutosha kufuatiliwa na pale inapohitajika kufanyiwa upasuaji usiwe wa dharura. Aidha, jamii inahamasishwa kutoa lishe bora kwa wajawazito.
MHE. NANCY H. NYALUSI atauliza: -

Je, ni lini Serikali itafunga Mtambo wa Mashine ya Oxygen katika Hospitali ya Rufaa ya Iringa ili kuhudumia wagonjwa wa dharura?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nancy Hassan Nyalusi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni 599.3 kwa ajili ya manunuzi ya mtambo wa kuzalisha Hewa Tiba ya Oksijen na ujenzi wa chumba cha kuhifadhia mtambo huo katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa na tayari hatua za manunuzi zimeanza na mradi huu utakamilika mwishoni mwa mwezi Juni, 2022.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA K.n.y. MHE. NORAH W. MZERU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwajengea wahudumu wa kada mbalimbali za afya nyumba bora ili kuboresha makazi yao?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imejenga nyumba 176 na katika mwaka wa fedha 2022/2023 itajenga nyumba 300 za kukaa familia tatu kwa kila nyumba. Ahsante.
MHE. AGNES M. MARWA K.n.y. MHE. STELLA A. IKUPA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa kuna vyumba maalum kwa ajili ya kujifungulia wanawake wenye ulemavu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Alex Ikupa, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeshalitambua tatizo hilo na kwa muda mrefu sasa marekebisho yamekuwa yakifanyika kwenye miundombinu isiyo rafiki kwa wanawake wenye ulemavu na tayari kwenye ramani mpya za ujenzi wa vituo vya afya, hospitali, ununuzi wa vifaa tiba, mahitaji kwa watu wenye mahitaji maalum yamezingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaboresha kadi ya kliniki ya Watoto chini ya miaka mitano ili kusaidia ufuatiliaji wa wingi wa damu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Mwanaisha Ng’azi Ulenge, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kadi za kiliniki ya watoto ziliboreshwa tangu mwaka 2011 kwa kuzingatia miongozo ya Shirika la Afya Duniani, ambapo maboresho hayo yamezingatia maeneo yasioacha maeneo hatarishi yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwongozo unaelekeza kutumia mbinu za kitabibu kutambua wingi wa damu kwa mtoto bila kumtoboa na wale wenye dalili za upungufu hupelekwa kwenye vipimo zaidi, ahsante.
MHE. MARGARET S. SITTA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itabadilisha Sera ya Chanjo kitaifa ili kuwakinga watu wengi zaidi badala ya kutibu mtu aliye na ugonjwa tayari?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa, gharama za kutibu ugonjwa wowote ni kubwa zaidi kuliko gharama za Kinga kupitia chanjo, kwa magonjwa yanayozulika kwa chanjo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Serikali imelifanyia kazi suala hilo kwa kupitia Sheria ya Afya ya Jamii ya Mwaka 2009 kifungu 19 ambapo inawataka wazazi na walezi kuhakikisha Watoto chini ya mwaka mmoja na wajawazito wanapatiwa chanjo ili kuwakinga na magonjwa yanayozuilika na chanjo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutoa wito kwa wazazi, walezi na wajawazito kuhakikisha wanafika vituo vya kutolea huduma za afya ili kupatiwa chanjo.
MHE. DOROTHY G. KILAVE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupunguza gharama za malipo kwa Akinamama wanaojifungua kawaida na wale wa operesheni?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dorothy George Kilave, Mbunge wa Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Afya inaendelea kutekeleza Sera ya Afya ya mwaka 2007 inayoelekeza kutoa huduma za matibabu bure kwa makundi maalum, ikiwemo akinamama wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka mitano. (Kipengere 5.3.4 chenye Tamko linalosema “Serikali kwa kushirikiana na sekta binafsi inayotoa huduma bila faida na mashirika ya Kimataifa itaendelea kutoa huduma bila malipo kwa wanawake wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano”).

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vituo vya binafsi visivyo na ubia na Serikali ukamilishaji wa Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote utakapopitishwa utakuwa suluhisho la tatizo hili.
MHE. AGNES E. HOKORORO aliuliza: -

Je, kwa nini huduma za afya kwa Watoto Njiti zinatozwa fedha ilihali Sera ya Afya inaelekeza huduma bure kwa Watoto chini ya miaka mitano?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Agnes Elias Hokororo, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, utoaji wa huduma za afya kwa watoto chini ya miaka Mitano wakiwepo Watoto Njiti kwa vituo vya Serikali na vile vya binafsi vilivyo na ubia na Serikali ni bure na ni takwa la kisera.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukamilishaji wa Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote utamaliza utata huu kwa wananchi wanaotibiwa katika vituo binafsi vya huduma za afya.
MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA aliuliza: -

Je, Serikali imejipangaje kutoa elimu juu ya ugonjwa wa fistula?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aleksia Asia Kamguna, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kupambana na ugonjwa wa fistula Serikali imekuwa ikitoa elimu kwa njia zifuatazo: -

a. Kuzuia mimba za utotoni kupitia elimu ya uzazi kwa vijana.

b. Kuwaelemisha akinamama kuhudhuria kliniki mapema ili wapate huduma muhimu na kupata ushauri wa mpango wa kujifungua.

c. Kutoa elimu kwa wajawazito kujifungulia katika vituo vya afya ili kuwahi kupatiwa msaada kama kutatokea tatizo la uchungu pingamizi au jingine.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafanya upanuzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2021/2022 na 2022/2023, Serikali imetoa kiasi cha shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya upanuzi wa miundombinu ya majengo ya huduma za dharura, huduma za wagonjwa mahututi, huduma za mionzi ambapo majengo haya yamekamilika na yanatumika. Pia ununuzi wa vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi bilioni 1.8, umefanyika. Pamoja na maboresho hayo, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni 350 kwa ajili ya umaliziaji wa jengo la upasuaji wa mifupa ambapo jengo hili litakamilika mwezi Juni, 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara inaendelea kushirikiana kwa karibu na Ofisi ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Morogoro kwa ajili ya usanifu wa majengo yanayokusudiwa kujengwa ikiwa ni sehemu ya mpango wa upanuzi wa hospitali hii.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA aliuliza: -

Je, ni lini Hospitali ya Kanda ya Kusini iliyopo Mtwara itakamilika?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Stella Martin Manyanya, Mbunge wa Nyasa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 4.4 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la huduma za mama na mtoto katika Hospitali ya Kanda ya Mtwara.

Mheshimiwa Spika, hadi sasa hospitali hii inatoa huduma ya wagonjwa wa nje (OPD) na wagonjwa wa kulazwa (IPD). Aidha, Serikali itaendelea kuipa hospitali hii kipaumbele katika mpango wa bajeti ili kuhakikisha kuwa inakamilika ifikapo mwaka 2025.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA aliuliza: -

Je, ni kwa nini Serikali isitoe matibabu bure kwa watoto wenye ugonjwa wa selimundu?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Matibabu ya watoto chini ya miaka mitano wenye matatizo ya kiafya ikiwemo Selimundu ni bure kwa mujibu wa Sera ya Afya ya mwaka 2007. Hivyo utambuzi na matibabu ya watoto wenye tatizo la selimundu hutolewa bila malipo.

Mheshimiwa Spika, suluhisho la tatizo hili ni Bima ya Afya kwa Wote.
MHE. BAHATI K. NDINGO K.n.y. MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha Bima za Afya za Wazee ili ziweze kutumika wakiwa nje ya Mikoa ambayo wamepewa Bima hizo.
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali ikiendelea na mchakato wa kukamilisha Muswada wa Bima ya Afya kwa wote, Serikali inaelekeza vituo vyote vya huduma kuwapatia huduma wazee wasio na uwezo waliotimiza vigezo hata wakiwa nje ya maeneo yao. Ahsante. (Makofi)
MHE. BAHATI K. NDINGO K.n.y. MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha Bima za Afya za Wazee ili ziweze kutumika wakiwa nje ya Mikoa ambayo wamepewa Bima hizo.
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali ikiendelea na mchakato wa kukamilisha Muswada wa Bima ya Afya kwa wote, Serikali inaelekeza vituo vyote vya huduma kuwapatia huduma wazee wasio na uwezo waliotimiza vigezo hata wakiwa nje ya maeneo yao. Ahsante. (Makofi)
MHE. MUSSA R. SIMA K.n.y MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha huduma za Afya kwa Wazee hasa wa Mkoa wa Arusha kwa kuwapatia dawa kupitia mfumo wa bima tofauti na iliyopo sasa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaytun Seif Swai, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekwishatoa maelekezo kwa wasimamizi wa vituo vya kutolea huduma za afya kuwa wazee wasio na uwezo na waliotimiza vigezo wapewe huduma za Afya wakiwa nje na ndani ya mikoa yao. Aidha, Serikali ipo kwenye hatua ya ukamilishaji wa Muswada wa Bima ya Afya kwa wote utakaowezesha makundi yote kupata huduma za afya.
MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupambana na magonjwa yasiyoambukiza?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa Serikali katika kupambana na magonjwa yasiyoambukiza ni kutoa elimu kinga, kusomesha Madaktari Bobezi kwenye eneo hili pamoja na ununuzi wa dawa na vifaa tiba vya teknolojia ya juu katika utambuzi na tiba ya magonjwa yasiyoambukiza.