Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Augustine Vuma Holle (7 total)

MHE. AUGUSTINO V. HOLLE: Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa kama Mkoa bado hatujaunganishwa kwenye Grid ya Taifa na kumekuwa na tatizo kubwa sana la kukosa nishati hii muhimu na kupelekea mkoa wetu kuwa miongoni mwa mikoa maskini; sasa je, Wizara ya Nishati imejipangaje vipi kuhakikisha kwamba inakamilisha kwa haraka na kwa ufanisi mradi wa REA awamu ya tatu katika Mkoa wa Kigoma ambao kimsingi umezinduliwa muda umeenda sana katika Kijiji au Kata ya Lusese? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi nzuri ya kufuatilia changamoto ya nishati. Ni kweli Mkoa wa Kigoma pamoja na Mkoa wa Katavi kazi za upelekaji umeme kupitia mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa kwanza zilichelewa kutokana na matatizo ambayo yalikuwa nje ya uwezo wa Wizara yetu ya Nishati pamoja na Wakala wetu Vijijini. Hata hivyo mradi huo umeshazindua rasmi na mkandarasi anaendelea na kazi ya survey na watakamilisha hivi karibuni.
Mheshimiwa Spika,aomba niwatoe hofu wakazi wa Mkoa wa Kigoma pamoja na Katavi kwamba kwa kweli kwa maelekezo ya Serikali na mkandarasi aliyeteuliwa ana uwezo na hivyo atafanya kazi kwa haraka iwezekenavyo nakushukuru. (Makofi)
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kuishukuru Serikali kwa niaba ya wananchi wa Kata za Kalela, Kwaga, Lusesa, Kasangezi, Muzi pamoja na Bugaga kwa kweli barabara ya kutoka Kidahwe - Kasulu sasa ni lami. Wananchi hawa tangu uhuru sasa wamepata barabara ya lami na wana furaha kubwa sana wanaishukuru Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, nini kauli ya Serikali kuhusu barabara ya kutoka Kasulu - Uvinza ukizingatia wananchi wa Kata za Lungwe Mpya na Asante Nyerere na maeneo mengine wanapata tabu sana? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, nini mipango ya Serikali kuhusu barabara ya kutoka Kitanga - Kibondo ukizingatia wananchi wa Kata za Kitanga, Kigabye na maeneo ya jirani wanapata tabu sana wanapoenda Kibondo? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO (MHE. ELIAS J. KWANDIKWA): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vuma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Vuma kwa umahiri wake, najua anawapigania sana wananchi wake.

Mheshimiwa Spika, kuhusu maswali yake niseme kwamba tunazitazama hizi barabara alizozitaja lakini kwa sababu tumekuwa na changamoto ya ujenzi wa barabara za lami hususan kuunganisha Mkoa wa Kigoma, naomba wananchi hawa watuvumilie. Hata hivyo, niseme tu hii barabara ya kutoka Kasulu kwenda Uvinza kwa maana inaanzia pale Kanyani kwenda Kibaoni kilometa 53 tunajitahidi kuiweka barabara hiyo katika hali nzuri. Niwahakikishie wananchi wa maeneo haya ikiwemo wananchi wa Nguruka wataweza kupita vizuri.

Mheshimiwa Spika, tukikamilisha ujenzi wa barabara hii kubwa ambayo nimeitaja kwenye jibu la msingi, tutatazama namna nzuri ya kufanya ili tuone tunafanya maboresho makubwa kwenye barabara hii. Hii ni pamoja na kuiangalia kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara yake ya pili hii aliyoitaja kutoka Kitanga kwenda Kibondo ni barabara ambayo inasimamiwa na TANROADS, Mkoa wa Kigoma na ipo katika hali nzuri. Niseme tu kuna changamoto katika Daraja hili la Mto Malagarasi, eneo hili ndiyo wananchi wanapata shida kuvuka kwenda Kibondo. Nimhakikishie Mheshimiwa Vuma na wananchi wa maeneo haya kwamba mara baada ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami, lipo daraja la chuma katika Mto Malagarasi, tutaangalia uwezekano wa daraja hili kulihamishia kwenye maeneo haya ili wananchi wa Kitanga waweze kupita kwenda Kibondo bila matatizo yoyote. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nishukuru kwa majibu mazuri na niishukuru Serikali kwa shilingi milioni 500 ambayo mmetuletea kwenye Chuo cha Nyamidaho, naamini kwamba mwakani kinaanza kufanya kazi kama alivyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, ni dhahiri kwamba hata baada ya kupokea fedha hizo, ujenzi utakapokuwa umekamilika, bado tutakuwa na uhitaji wa jiko, bwalo la kulia chakula, bweni la wanafunzi wa kiume pamoja na uzio kwa ajili ya usalama wa wanafunzi ambao watakuwa wanasoma kwenye chuo kile pamoja na nyumba za watumishi, maana hakuna mpango wa kujenga nyumba hata moja ya watumishi. Je, Serikali ina kauli gani kuhusu haya mahitaji ambayo yatakuwa yamebakia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Waziri yuko tayari kuongozana na mimi kwenda kuona mazingira jinsi yalivyo ili iweze kutoa msukumo katika kumalizia mambo haya na kuweka mazingira mazuri kwa ajili ya watoto kusoma kwenye Chuo cha Nyamidaho?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Vuma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utaniruhusu, kabla ya kujibu maswali hayo, naomba nitumie nafasi hii kwa msisitizo mkubwa kueleza ni namna gani Mheshimiwa Mbunge amehusika katika kupatikana kwa chuo hiki. Kwa kweli lazima niseme, kama isingekuwa yeye, kwa namna alivyokuwa anatusumbua, mpaka pale ofisini anafahamika kama king’ang’anizi, chuo hicho kisingepatikana. Naomba nitumie nafasi hii kumpongeza na nimuombe Mungu wapiga kura wake wasikie kwamba kwa kweli amejitahidi na napenda kumpongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kama Serikali iko tayari kuongeza majengo na miundombinu mingine ambayo bado kuna upungufu, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba punde chuo kitakapoanza mwaka 2020 kama tunavyotarajia, tutaangalia upungufu uliopo na kuendelea kuboresha na kuongeza kadri uwezo wa fedha utakavyoruhusu. Kwa hiyo, naomba nihamhakikishie kwamba hatutaishia hapa, tutaendelea kukiboresha chuo kile ili Wanakasulu na Watanzania wengine waweze kusoma katika mazingira mazuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuandamana naye, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba niko tayari kuandamana naye. Pia najua kwenye mkoa wake wapo vilevile Wabunge wa Viti Maalum ambao nao vilevile wamekuwa wakisaidia kusukuma ujenzi wa vyuo hivi, nao vilevile wakiwepo itasaidia tutaandamana kwenda kuangalia chuo hicho. Nashukuru sana.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza swali mpja la nyongeza. Kwa kuwa Jimbo la Kasulu Vijijini hasa Kata za Kalela, Kwaga, Rusesa, Muzye, Bugaga na Kagerankanda zina shida kubwa sana ya maji.

Je, Naibu Waziri yuko tayari kuongozana na mimi kwenda Jimbo la Kasulu Vijijini kabla ya Mwaka huu wa Fedha kuisha ili tuangalie ukubwa wa tatizo na ajionee na hatimaye tuweze kuwa na mkakati wa kumaliza tatizo hili la maji kama sio kupunguza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kwanza kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya katika Jimbo lake lakini nataka nimhakikishie sisi kama Wizara ya Maji tumeiona hiyo changamoto katika Jimbo lake. Bunge lako tukufu limetuidhinishia zaidi ya milioni 987 katika kuhakikisha tunaenda kutatua tatizo la maji katika Jimbo la Kasulu Vijijini. Na ninataka nimhakikishie kama Naibu Waziri niko tayari kwenda katika Jimbo lake kuangalia namna gani tunaweza tukashirikiana kutatua tatizo la maji. (Makofi)
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Wilaya ya Kasulu kuna mgao mkubwa sana wau meme. Yako maeneo hasa maeneo ya Makele, kila ikifika jioni lazima umeme ukatike na wananchi wanakosa huduma ya kuangalia tarifa ya habari, lakini na maeneo mengine mengi ya Wilaya ya Kasulu. Nataka kujua majibu ya Serikali nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba tena wa muda mfupi, kwamba unakomesha mgao huu?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Mkoa wa Kigoma, REA awamu ya III imeanza kwanza kwa kuchelewa lakini pili maeneo mengi hayajafikiwa na mradi, lakini pia mradi huo unasuasua. Je, Waziri yupo tayari kutuma wataalam wake au yeye mwenyewe kuja Mkoa wa Kigoma hasa Kasulu Vijijini ili kuhakikisha kwamba anakutana na wakandarasi ili waweze ku-speed up utekelezaji wa mradi? Nashukuru sana.
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri wangu, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Vuma, Mbunge wa Kasulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Vuma pamoja na Wabunge wengine wote kutoka Kigoma, kwa kazi kubwa walizofanya katika kufuatilia Mkoa wa Kigoma kupata Gridi ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kulikuwa na changamoto kubwa sana ya kiumeme katika Mkoa wa Kigoma na Mkoa wa Katavi, lakini kama ambavyo limejibiwa kwenye swali la msingi, Serikali imeanza kutekeleza mradi wa kupeleka umeme wa Gridi katika Mkoa wa Kigoma kutoka Tabora. Tumeanza kujenga toka mwaka jana mwezi Januari, kutokea Urambo, tunajenga sub-station na tumeshaanza kujenga na tumeshaanza kujenga sub-station ya pili tunajenga Nguruka na ujenzi unaendelea na sub-station ya tatu tunajenga Kidahwe Mjini Kigoma, nako ujenzi unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunajenga njia ya kusafirisha umeme mkubwa kilovoti 400 kutoka Kigoma na kusambaza maeneo yote ya Wilaya ya Kigoma ikiwemo, Kasulu, Kibondo, Kakonko na maeneo mengine na ujenzi umeshaanza. Naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Vuma, Mheshimiwa Profesa Ndalichako na Waheshimiwa Wabunge wengine wa Kigoma kwamba tunatarajia kukamilisha mwakani mwezi Desemba, shughuli zote na Gridi ya Taifa itakuwa imefika kwenye Mkoa wa Kigoma.

Pia kwa upande wa matumizi pia ya umeme Kigoma kwa sasa wanatumia mashine za mafuta ni vema nikawaambia Waheshimiwa Wabunge ili wajue, ingawa uendeshaji kwa kweli ni mkubwa na kwamba tunatambua mahitaji ya umeme, hatuna namna mbali na kuwalisha umeme kwa utaratibu huo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, mahitaji ya wananchi wa Kigoma kwa siku ni megawatt 5.2 pamoja na kwamba mashine tulizonazo pale ni megawatt 2.6 na tunazidisha mara nne zinafikisha kama megawatt 8 lakini kwa sababu ya njia kuwa ndefu na umeme unachotwa kwenye mafuta bado umeme ule unakuwa hauna nguvu. Ndio maana mnaona mara nyingi umeme unakatika sio mgao isipokuwa umeme unakatika kutokana na njia kuwa ndefu na source yake ni mafuta. Nimeona niliweke vizuri suala hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, maeneo ya REA yaliyobaki ni kweli katika Mkoa wa Kigoma na hasa Kasulu kwa Mheshimiwa Vuma, Mheshimiwa Vuma ana vijiji 61 na tumeshapeleka umeme kwenye vijijini 42 bado vijiji 19 na tulizindua pale Lusesa na Lusesa kazi inaendelea. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Vuma anavyofuatilia masuala haya na kwa sababu utekelezaji wa umeme katika vijiji vyote kama alivyoeleza Mheshimiwa Naibu Waziri unaanza tarehe 15 mwezi huu na tunarajia ndani ya miezi 18 kukamilisha vijiji vyote katika nchi yetu, vijiji vyote vya Mheshimiwa Vuma vitapata umeme mapema sana. Hata hapo Makere umeme unaokwenda kutoka pale mpaka mpakani mwa Rwanda na Burundi tutaunganisha na majirani zetu wa Rwanda na Burundi kupitia mradi wa Rusumo ili maeneo ya mipakani mwa Tanzania, Rwanda na Burundi nayo yapate umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Waziri, naomba kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa inafahamika wazi kwamba baada ya Kambi ya Wakimbizi kuondoka, Serikali ilifanya expansion, yaani iliongeza mipaka ya Kambi ile ikamega Vijiji vya Katonga, Mgombe, Nyamusanzu na Buhoro bila kufuata taratibu. Bahati mbaya wakawa wamekabidhiwa Jeshi; na kumekuwepo na jitihada za Ofisi ya Mkuu wa Wilaya wakishirikiana na Jeshi kutaka kuwarudishia wananchi maeneo. Sema walitaka kuwarudishia kipande kidogo, wananchi wakawa wamegoma.

Je, Serikali haioni kwamba kuna haja ya kufanya jambo hili kwa haraka ili wananchi wale waweze kupata haki yao ya mashamba hayo ambayo yamechukuliwa kwa muda mrefu, aidha kwa fidia ya maeneo au fidia ya fedha? (Makofi)
WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vuma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza uniruhusu nimpongeze tu Mheshimiwa Vuma, kwa juhudi zake anazozifanya kuhakikisha kwamba mgogoro ambao ulijitokeza tunaweza kuumaliza. Nampongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wafahamu kwamba Jeshi ni la kwao. Hili ni Jeshi la Wananchi wa Tanzania. Watambue kwamba uwepo wa Jeshi ni kwa manufaa yetu sote. Kwa hiyo, tumekuwa na maeneo makubwa katika maeneo yetu, lakini lengo lake ni kuhakikisha kwamba maeneo hayo yanatumika kwa ajili ya shughuli za Jeshi na vifaa vya Jeshi. Kwa hiyo, wananchi wakitambua hivyo, nawaomba tu wawe na ushirikiano. Nafahamu ipo migogoro kadhaa lakini nafahamu pia juhudi imefanyika kuhakikisha migogoro mingi tumeweza kuimaliza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namhakikisha Mheshimiwa Vuma kwamba suala la kumaliza mgogoro tunamaliza kwa kuwa kuna hatua nzuri tumezifikia. Vikao vya awali kama nilivyosema, vimeshafanyika, lakini sasa vikao ambavyo vitakuja kuendelezwa ni kuhakikisha kwamba tunamaliza mgogoro huu. Zipo Sheria za Ardhi na Sheria za Vijiji zitatumika ili kuhakikisha wananchi hawa wanapata haki zao.

Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, lakini naomba tuendelee kushirikiana; na wananchi wavute subira, tuko kwenye hatua nzuri ya kumaliza mgogoro huu. (Makofi)
MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa uvumbuzi wa vipaji, lakini pia na uendelezaji wa vipaji unapaswa kuanzia ngazi ya chini kabla ya kufika kwenye National level hasa kwenye shule zetu za sekondari, vyuo na huko halmashauri kwa ujumla. Je, Serikali haioni haja kwamba inapaswa kutenga fedha za kutosha kwenye bajeti yake ili kuendeleza vipaji vya michezo mashuleni, vyuoni na huko chini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; tumesikia kwamba, Serikali imeanzisha combination za elimu ya michezo (physical education). Nataka kujua utekelezaji wa jambo hili umefikia wapi mpaka sasa? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Vuma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge maana yeye ni mdau mkubwa wa michezo, lakini pia niwapongeze Wabunge wote pamoja na Waheshimiwa Madiwani katika halmashauri zao kwa jinsi ambavyo wamekuwa wakishirikiana na Wizara hii kwa suala zima la michezo. Swali lake la kwanza alitaka kufahamu ni kwa kiasi gani Serikali inatenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha michezo katika ngazi za chini inapewa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo ni la muhimu sana. Sisi kama Wizara nimesema tangu mwaka 2019/2020 tumeanza, lakini nitoe rai sasa kwa Waheshimiwa Madiwani na Waheshimiwa Wabunge katika ngazi za halmashauri, fedha za michezo zitengwe. Kwa hali ilivyo sasa ni Madiwani na baadhi ya wadau wanahangaika na hili suala, lakini halmashauri zetu zitenge fungu chini ya Idara ya Elimu Msingi kwa ajili ya kuhakikisha michezo inadumishwa katika maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili alitaka kufahamu mkakati tulionao wa Wizara kuanzisha hizi combinations za michezo kwa A Level zimefikia hatua gani. naomba nimjulishe Mheshimiwa Vuma kwamba, Kamati ilishaundwa kati ya Wizara ya Elimu, Wizara ya Michezo pamoja na TAMISEMI na ipo site ikitembelea zile shule 56 za msingi na sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Kamati hiyo kuleta majibu maana yake tunaendelea na zile shule ambazo tumeshazitambua ikiwemo Shule za Kibiti, Mpwapwa na Makambako ili kuanzisha sasa hii combination na tupate network kuanzia msingi mpaka vyuo vikuu. Endapo kazi hii itakuwa imekamilika itasaidia sana kutoa mafunzo kwa vijana wetu kuhusu masuala ya michezo. Ahsante. (Makofi)