Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Halima Abdallah Bulembo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HALIMA A. BULEMBO (K.n.y. MHE. ZUBEDA H. SAKURU) aliuliza:- Kumekuwa na ongezeko kubwa la matukio ya kihalifu nchini yanayohusishwa pia na upatikanaji wa hati za kusafiria zaidi ya moja zinazotolewa hapa Tanzania kwa baadhi ya wahalifu kiholela:- Je, Serikali inachukua hatua gani katika udhibiti wa utoaji hati za kusafiria kiholela?

Supplementary Question 1

MHE. HALIMA A. BULEMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kuna raia wa kigeni ambao wamekuwa wakitumia udhaifu wa mfumo wa hati za kusafiria na kuwawezesha kusafiri kinyume cha utaratibu na kuwawezesha kutenda makosa kwa kigezo cha Utanzania. Mheshimiwa Waziri amekiri kwamba wanapatikana lakini hatujajua wala hatujawahi kusikia ni hatua gani ambazo zimekuwa zikichukuliwa. Je, Serikali imewachukulia hatua gani maofisa hawa wanaojihusisha na utoaji wa hati hizo?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na Maafisa Uhamiaji ambao wanajihusisha na ukiukwaji wa taratibu wamekuwa wakichukuliwa hatua mbalimbali. Miongoni mwa hatua hizo ni kuwafukuza kazi pamoja na kuwashtaki. Hata hivyo, naomba nichukue fursa hii kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba tupo katika hatua za mwisho za ukamilishwaji wa uanzishwaji wa Mahakama ya Kijeshi katika Idara ya Uhamiaji kama ilivyo katika majeshi mengine ikiwemo Polisi ili kuweza kuwa na utaratibu wa uchukuaji wa hatua hizo kwa haraka.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naamini kabisa pale mchakato huo utakapokuwa umekamilika, basi tutaweza kufanya kazi hiyo kwa ufanisi zaidi. Kwa wale ambao tumekuwa tukiona mazingira tu yanaashiria utendaji mbovu au ukiukwaji wa sheria ikiwemo rushwa bila ya kupata ushahidi tumekuwa tukichukua hatua mbalimbali ikiwemo kuwahamisha katika vituo vyao vya kazi.

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. HALIMA A. BULEMBO (K.n.y. MHE. ZUBEDA H. SAKURU) aliuliza:- Kumekuwa na ongezeko kubwa la matukio ya kihalifu nchini yanayohusishwa pia na upatikanaji wa hati za kusafiria zaidi ya moja zinazotolewa hapa Tanzania kwa baadhi ya wahalifu kiholela:- Je, Serikali inachukua hatua gani katika udhibiti wa utoaji hati za kusafiria kiholela?

Supplementary Question 2

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa kwa siku hizi za karibuni Watanzania wameshuhudia mauaji ya kutisha katika Mikoa ya Mwanza na Tanga. Je, Serikali ina mkakati gani wa dhati wa kuzuia mauaji haya?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili lina majibu mapana sana kwa sababu linagusa vyombo kadhaa vilivyo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani na hususan Jeshi la Polisi. Kwa sababu swali la msingi linahusu Idara ya Uhamiaji, naomba nilijibu kwa mtazamo wa Idara ya Uhamiaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Idara ya Uhamiaji suala la udhibiti wa uhalifu nchini inajikita zaidi katika kuhakikisha tunadhibiti uingiaji wa wahamiaji haramu nchini ambao mara nyingi wamekuwa wakihusishwa na kuongeza wimbi la uhalifu katika nchi yetu kwa kuingiza silaha pamoja na kujihusisha na vitendo mbalimbali vya uhalifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kufanya hivyo, tumeandaa mkakati kabambe ambao utahakikisha kwamba unadhibiti vipenyo vyote vilivyopo mipakani. Mpaka sasa hivi tumefanya uhakiki katika baadhi ya mikoa na kubaini zaidi ya vipenyo 280 na bado tunaendelea katika baadhi ya mikoa ambayo hatujakamilisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunatafuta fedha ili tuweze kufanya hiyo kazi ya kudhibiti mipaka yetu ili tuweze kuzuia hawa wahamiaji haramu wasiweze kuingia katika nchi yetu. Hata hivyo, tumekuwa tukifanya kazi kubwa sana ya kuhakikisha kwamba tunawakamata wahamiaji haramu na kuwachukulia hatua zinazostahiki kwa kufanya misako katika maeneo mbalimbali nchini. Tumefanya kazi hiyo kwa mafanikio makubwa sana na wahamiaji haramu wengi tayari wameshakamatwa na wameshachukuliwa hatua za kisheria kwa kipindi kifupi tangu Serikali ya Awamu ya Tano ilivyoingia madarakani.