Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Victor Kilasile Mwambalaswa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupa

Primary Question

MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:- Mheshimiwa Spika, Serikali imeamua kujenga Vyuo vya VETA kwa Wilaya zote nchini na Chunya ni kati ya Wilaya 10 za mwanzo kupata chuo hicho:- Je, Serikali ina mpango gani wa kutumia majengo yaliyokuwa kambi ya ujenzi wa barabara ya lami pale Chalangwa kwa ajili ya Chuo cha VETA, ili kuokoa gharama kubwa za ujenzi wa majengo mapya.

Supplementary Question 1

MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri sana yameniridhisha sana, lakini pamoja na hayo nina maswali mawili ya nyongeza. Serikali mwaka juzi ilitangaza kwamba itaweka vyuo vya VETA kwenye Wilaya zote nchi, lakini itaanza na Wilaya 10 ambapo Wilaya ya Chunya ni mojawapo naishukuru sana Serikali kwa kuiweka Chunya katika moja ya Wilaya 10 za kuweka Vyuo vya VETA.
Mheshimiwa Spika, bahati nzuri sana tena Wilaya ya Chunya inagawanyika kuwa Wilaya mbili, Wilaya ya Chunya na Wilaya ya Mkwajuni Wilaya ya Songwe ambako sasa ndiyo kuna heka kumi zimetengwa za kujenga Chuo cha VETA. Sasa swali, kama Serikali ilisema inaipa Chunya Chuo cha VETA, Chunya imegawanyika ziko Wilaya mbili siyo bora tu zote Wilaya zote mbili Chunya na Songwe zipate Chuo cha VETA? Hilo la kwanza na naona Mheshimiwa Mulugo ambaye ni wa Wilaya ya Songwe amefurahi sana. (Kicheko)
Mheshimiwa Spika, la pili, pale kwenye kambi ya ujenzi wa barabara ya Mbeya - Chunya kwa kiwango cha lami Serikali imesema majengo yale ni ya muda siyo ya kudumu. Je, kwa kuwa, eneo lililotengwa ni heka 25 haiwezi ikaanzia kwa majengo hayo ambayo siyo ya kudumu lakini ikajenga Chuo cha VETA kwa eneo kubwa ambalo limebaki?

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimwa Spika, ahsante sana. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mwambalaswa Mbunge wa Lupa kwa jinsi ambavyo amelifuatilia sana jambo hili. Pia niseme tu kwamba, kwa mujibu wa sera tuliyojipangia na mpango tuliojipangia Wizara yetu imedhamiria kuanza kujenga Vyuo vya VETA katika Wilaya zote ambazo hazina kabisa Chuo chochote cha Ufundi au VETA kwa ujumla. Kwa hali hiyo, kwa sababu ya bajeti ambayo kimsingi inahitajika katika maeneo mengi siyo rahisi kuvijenga vyuo vyote kwa siku moja.
Mheshimiwa Spika, nikuombe Mheshimiwa Mbunge kushirikiana Halmashauri yako hilo eneo ambalo umeliangalia ni vema likatengwa na likapimwa na hati zake zikawasilishwa katika Wizara yetu ili liwe katika mpango.
Mheshimiwa Spika, pia nitoe wito kwa Waheshimiwa Wabunge wote, Wizara yangu inapata tatizo kubwa sana inapofikia kuanza mipango ya maandalizi ya ujenzi wa vyuo hivyo kutokana na ardhi hizo kutokupatikana na kupimwa, ni vema Halmashauri zote ambazo ziko katika mpango huu zihakikishe zinatenga maeneo hayo ili isiwe ni kikwazo tunapofikia kufanya hivyo.
Mheshimiwa Spika, pili, nadhani nimejibu yote kwa pamoja kama ambavyo nimeelekeza kwamba ukishapima tutafanya hivyo kwa kuwa sasa Wilaya ya Songwe inajitegemea, lakini itakuwa ni baada ya kumaliza zile ambazo tumeanza nazo. Ahsante sana.