Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza:- Matatizo ya wanafunzi kutojua kusoma na kuandika pamoja na kutofanya vizuri katika mitihani yao mara zote lawama zinakwenda kwa Walimu. Je, Serikali imefanya utafiti wa kina na kuona kama Mwalimu peke yake ndiye anayeweza kumfanya mwanafuzi aweze kufanikiwa katika masomo yake?

Supplementary Question 1

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa majibu ya Serikali yanaeleza wazi kuwa kufaulu kwa mtoto kunategemea mwanafunzi mwenyewe, Mwalimu, mazingira ya kufundishia pamoja na wazazi. Sasa, je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kwamba mazingira ya kufundisha na kufundishia yanakuwa bora na pia kutoa elimu bora kwa wazazi kwamba wao ni wajibu wao pia kuwasimamia watoto wao?
Swali la pili, kwa kuwa hakuna Mwalimu anayefanya kazi kubwa kama Mwalimu ya KKK wa darasa la kwanza na la pili kwani yeye ndiye anayetoa msingi wa elimu au mwelekeo wa mtoto wa maendeleo yake ya baadaye. Je, Serikali imejipanga vipi kuwapa motisha Walimu wa KKK kutokana na kazi kubwa wanayoifanya?

Name

Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Answer

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mariam Nasoro Kisangi kwa ufuatiliaji mzuri. Anawajali sana Walimu na ndiyo maana maswali yake kila siku yanalenga katika kuangalia Walimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikiendelea kuboresha mazingira ya kufundishia na kujifunzia na ndiyo maana katika majibu yangu ya msingi nimeeleza kabisa kwamba, Serikali imekuwa inatoa mafunzo kwa walimu kazini na tumetoa mafunzo kwa walimu 22,697 kwa stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu, hii yote ni katika kujenga mazingira mazuri na kumwezesha mwalimu. Vilevile Serikali imeandaa vitabu na iko inasambaza vitabu katika kuimarisha stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kwamba Serikali inafanya nini ili wazazi waweze kutambua wajibu wao. Serikali imekuwa ikihamasisha wazazi na ndiyo maana hata kupitia Bunge lako naomba pia Waheshimiwa Wabunge mtuunge mkono katika maeneo yenu tuhamasishe wazazi ili watambue kwamba elimu ndiyo kila kitu katika maisha ya watoto wao na hivyo Serikali itaendelea kutoa uhamasishaji kwa wazazi ili waendelee kutambua wajibu wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la mwisho la nyongeza anauliza kwamba, Serikali imejipanga vipi kutoa motisha kwa walimu wa darasa la kwanza na la pili ambao wanakuwa na mzigo mkubwa wa kufundisha watoto. Serikali inatambua mchango wa walimu na ndiyo maana nasema ukiangalia vipaumbele vyetu katika mafunzo kwa Walimu kazini tumejikita zaidi kwa Walimu hao kwa sababu tunatambua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nitumie nafasi hii kusema kwamba tunakusudia na kesho nitasimama hapa mbele yenu kueleza mipango yetu ijayo lakini tunakusudia kuweka utaratibu wa kuweza pia kuwatambua Walimu wa darasa la kwanza na la pili wanaofanya vizuri kwa sababu tumekuwa na utamaduni wa kuwatambua kwenye darasa la saba, kidato cha nne, lakini tunaweka utaratibu mahsusi wa kuweza pia kuwatambua kwa sababu nayo pia ni motisha.

Name

Ester Michael Mmasi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza:- Matatizo ya wanafunzi kutojua kusoma na kuandika pamoja na kutofanya vizuri katika mitihani yao mara zote lawama zinakwenda kwa Walimu. Je, Serikali imefanya utafiti wa kina na kuona kama Mwalimu peke yake ndiye anayeweza kumfanya mwanafuzi aweze kufanikiwa katika masomo yake?

Supplementary Question 2

MHE. ESTER M. MMASI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na uwepo wa Tume ya Vyuo Vikuu yaani TCU (Tanzania Commission for Universities), lakini tumekuwa na changamoto kubwa sana ya kuzalisha wahitimu wasiokuwa na uwezo wa kutosha katika mustakabali wa ujenzi wa uchumi wa nchi ya Tanzania. Swali, je, Serikali imejipangaje katika suala zima la kuzalisha wahitimu wenye uwezo, weledi wenye tija na maarifa kazini? Ahsante sana.

Name

Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Answer

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba Serikali imejipanga vizuri kabisa kuhakikisha kwamba watu wasiokuwa na uwezo wanachukuliwa hatua stahiki na katika hili niseme tu wazi kwamba, Serikali itafanya uhakiki wa wanafunzi au tunaangalia upya vigezo vya wanafunzi kujiunga na vyuo vikuu ili tuweze kuchukua hatua mahsusi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kesho nitakuwa nawasilisha hotuba yangu, haya yote nitayaeleza kwa kina, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Ester upokee hili jibu lakini tumejipanga vizuri na mikakati yote nitakuja kuieleza hapa kesho.