Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:- Hospitali ya Mji wa Tarime hutoa huduma kwa wananchi wa Wilaya za Tarime, Rorya, Serengeti na nchi jirani ya Kenya na kwamba hospitali hii ina ukosefu mkubwa wa madawa na vifaa tiba:- Je, Serikali ina mpango mkakati gani wa kuhakikisha hospitali hii inakuwa na madawa pamoja na vifaa tiba vya kutosha kutoka MSD?

Supplementary Question 1

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwenye swali langu la msingi nimeelezea dhahiri kwamba hospitali ya Mji wa Tarime inatoa huduma kwa Wilaya nzima ya Tarime na baadhi ya wananchi wa Serengeti na Wilaya ya Rorya. Serikali imekuwa ikileta fedha za OC na bajeti ya dawa, kwa kufuata population ya Mji wa Tarime ambayo ni watu 78,000. Ppia imekuwa ikileta, fedha la kapu la pamoja kwa maana ya basket fund, milioni 106 tu ambayo haikidhi haja na zamani tulikuwa tukipokea zaidi ya milioni 500 bado huduma za afya zilikuwa siyo dhahiri.
Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwa nini Serikali sasa, isiweze kuleta fedha za OC na za basket fund kwa kufuata population walau ya Tarime Rorya na siyo ya Mji wa Tarime, ukizingatia kwamba tunatoa huduma kote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi wanaopata huduma ya afya kwenye hospitali ya Mji wa Tarime, wamekuwa wakitozwa sh. 6,000 lakini wakifika ndani hawapati madawa, hawapati huduma zinazostahili, ni kwa nini sasa Serikali kwa maana katika Hospitali ya Mji wa Tarime tayari tuna jengo ambalo liko tayari, kuweza kufungua duka la dawa kwa maana ya MSD ni kwa nini sasa Serikali isiweze kuja na kufungua hilo duka pale kwenye hospitali ya Mji wa Tarime ili wananchi waweze kupata huduma ya madawa wanavyoenda kutibiwa pale kuliko kuhangaika tena wanatoa sh. 6,000 halafu akitoka nje anaambiwa hamna dawa? Ahsante.

Name

Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, swali la kwanza ni kwa nini Serikali, isichukulie takwimu kwamba Hospitali hii ya Mji wa Tarime inatibu pia wateja kutoka Rorya na maeneo mengine ya jirani. Jibu ni kwamba Serikali siku zote inapopanga Mpango wake wa Bajeti kwa ajili ya kuzihudumia hospitali zote nchini ina formula maalum ambayo inazingatia kigezo anachokisema cha idadi ya watu wanaohudumiwa katika hospitali. Pia, pesa zote zinazotoka kwa wafadhili zinapangwa kwenye bajeti kutokana na burden of desease, mzigo wa magonjwa ambao unahudumiwa katika eneo la kijiographia ambapo hospitali hiyo inatoa huduma.
Kwa hivyo, watu wote wanaofanya planning kwenye sekta ya afya, wanazingatia kigezo cha idadi ya watu, lakini pia mzigo ambao hospitali husika inaubeba kwa maana ya kutoa huduma zake. Kwa maana hiyo, niseme tu maelezo ya ziada hapa kwa Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Spika, kwamba changamoto ya kuwahudumia Watanzania kwenye eneo hili la dawa, vifaa na vifaa tiba ni kubwa sana, kwa maana ya mzigo wa kibajeti ambapo Sekta ya Afya inabeba. Changamoto hiyo itaweza kutatuliwa kwa jitihada ambazo tunazifanya sasa hivi za kuhakikisha Watanzania wote wanakuwa na bima ya afya, hili ni jambo ambalo lipo kwenye Ilani ya Uchaguzi pesa tulizonazo sasa ni ndogo haziwezi kubeba mzigo wa kutibu Watanzania wote kama ambavyo tunatamani iwe, sasa tunakuja na jitihada mpya ya kuhakikisha Watanzania wote wanaingia kwenye Mfuko wa Bima ya Afya ili hospitali zenyewe ziweze kukidhi mahitaji ya madawa, vifaa tiba na vitendanishi kama ambavyo zinajipangia.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, kuhusu duka la dawa la MSD. Nimpongeze Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko na wataalam wetu wa sekta ya afya kwenye hospitali ya Mji wa Tarime, kwa kuandaa eneo kwa ajili ya kuanzisha duka la MSD. Kwanza nitumie nafasi hii kwa namna ya kipekee kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli. Kwa kuanzisha mkakati, wa kufungua maduka ya MSD yaani MSD Community outlets.
Maduka haya kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais yanatoa huduma kwenye hospitali ya Taifa na hospitali za Kanda kwa maelekezo yake, lakini kwa kuzingatia mahitaji ya Mikoa na Wilaya zote nchini kwamba wangependa kuwa na maduka ya MSD, ili waweze kuhakikisha wananchi wanapata dawa kwa ukaribu na kwa gharama nafuu zaidi, ndani ya hospitali kuliko kuzifuata nje ya hospitali. Wizara yetu imewaelekeza MSD waandae Mpango Mkakati wa kutoa utaalam wa kiufundi wa namna ya kuanzisha maduka ya dawa, katika mfumo huu wa MSD community outlets. Taasisi yetu ya MSD, imejipanga kuwasaidia Milkoa.
Pia Taasisi yetu ya NHIF imejipanga kuingia kwenye mkakati wa kuwakopesha hospitali yoyote ile iwe ya Mkoa ama ya Wilaya, fedha kwa ajili ya kuanzisha maduka haya na MSD itatoa technical support, ikiwepo mifumo ya kuendeshea maduka haya kama mifumo ya computer ili kuweza kuyaendesha kisasa zaidi na katika mtindo ule ule ambapo maduka yetu ya MSD community outlets yanaendeshwa.

Name

Rev. Peter Simon Msigwa

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Iringa Mjini

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:- Hospitali ya Mji wa Tarime hutoa huduma kwa wananchi wa Wilaya za Tarime, Rorya, Serengeti na nchi jirani ya Kenya na kwamba hospitali hii ina ukosefu mkubwa wa madawa na vifaa tiba:- Je, Serikali ina mpango mkakati gani wa kuhakikisha hospitali hii inakuwa na madawa pamoja na vifaa tiba vya kutosha kutoka MSD?

Supplementary Question 2

MHE. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Kwa kuwa tatizo hili la Rorya linafanana na tatizo la Iringa Mjini, baada ya kujua tatizo la hospitali ya Rufaa ya Iringa Mjini, Manispaa tumejenga hospitali ambayo inafanya kazi. Hata hivyo, tuna tatizo la vifaa tiba kwa mfano, akinamama wanavyofanyiwa operation wanahitaji wapange foleni kusubiri yale mashuka yakaoshwe kwenye hospitali ya Rufaa, ni lini sasa Serikali itatatua tatizo hili ambalo akinimama kwa kweli wanapata matatizo?

Name

Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Peter Msigwa, Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini kwa swali lake na majibu ya Serikali ni kwamba yeye ni Mjumbe kwenye Halmashauri ya Mji wa Iringa Mjini. Kwa maana hiyo, anashiriki kikamilifu katika uendeshaji kuanzia kwenye kupanga na hata kusimamia utekelezaji wa sera ya afya na sera ya maendeleo ya jamii kwenye eneo lake.
Namshauri ashirikiane vizuri na Halmashauri yake waweze kupanga bajeti kwa ajili ya kununua mashine za kufulia nguo hizo, ambapo zinakosekana kwenye hospitali moja ili aweze kutoa hiyo huduma kwa ukaribu na kwa urahisi zaidi kwa wananchi wanaohitaji.
Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo naomba niseme tu kwamba. Uendeshaji wa hizi hospitali una changamoto kubwa ya kifedha, kama nilivyosema awali, na kwa maana hiyo, Waheshimiwa Wabunge wote wakitaka kutatua matatizo yanayozikabili hospitali zao ni lazima wawe makini kwenye kuelekeza mapato yanayotokana na own source collection za pale kwenye Halmashauri, kwenye eneo hili la huduma za afya.
Maana kila Mbunge sasa amekuwa anatuletea maswali sisi watu wa Wizara ya Afya wakati sisi kazi yetu ni kutoa technical support, kazi yetu ni kusimamia ubora na vitu vingine lakini wao wenyewe Wabunge, wakishirikiana na Madiwani na Halmashauri zao wana jukumu la kutoa huduma bora zaidi kwa Wananchi wanaowaongoza. (Makofi)