Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Susan Limbweni Kiwanga

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Mlimba

Primary Question

MHE. SUSAN L. KIWANGA (K.n.y. MHE. DEVOTHA M. MINJA) aliuliza:- Askari wa Jeshi la Polisi na Magereza wanaishi katika nyumba chakavu zisizokuwa na hadhi ikilinganishwa na kazi zao wanazofanya kwa jamii:- Je, Serikali ina mpango gani kuwaboreshea makazi?

Supplementary Question 1

MHE. SUSAN L. KIWANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ingawaje dah, Waziri kajibu kwa pozi kweli kweli mistari michache tu. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, anasema kwamba wanaendelea kujenga, hivi miaka 51 ya Uhuru upungufu nyumba 10,000 wapewe miaka mingapi ili wamalize hili tatizo katika nchi yetu? Magereza nimeshuhudia mwenyewe kwa mfano katika Wilaya yetu ya Kilombero kuna magereza mawili ya Idete na Kiberege wafungwa wanaenda kujenga nyumba za watu binafsi kwa nini msitumie nguvu kazi ya wafungwa hawa ili kwenda kujenga nyumba na Serikali muongeze hela kule juu kumalizia majengo haya? Hiyo nguvu kazi ya hawa wafungwa walioko magerezani mtafanya lini huo mpango? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la Polisi yaani kama kuna tatizo kubwa ndani ya Mkoa wa Morogoro ni suala la nyumba za Polisi hasa Wilaya ya Kilombero likiwemo na Jimbo la Mlimba. Kwanza Wilaya ya Kilombero pale Ifakara kulikuwa na majengo ya Kituo cha Polisi, Mlimba hakuna kabisa wanategemea TAZARA…
MWENYEKITI: Mheshimiwa naomba uulize swali tafadhali.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Na zile nyumba zimeuzwa ule mwaka zilizouzwa nyumba za Serikali.
MWENYEKITI: Mheshimiwa naomba uulize swali kwa ufupi.
MHE. SUSAN L. KIWANGA: Sasa hivi hawana nyumba kabisa. Je, Serikali katika huo mpango wao wana mpango gani wa kujenga nyumba na Vituo vya Polisi ndani ya Wilaya ya Kilombero, Ifakara na Jimbo la Mlimba ambapo wanakaa kwenye vituo vya TAZARA?

Name

Charles Muhangwa Kitwanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Misungwi

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu ni rafiki yangu sana. Ananiuliza tupewe miaka mingapi, yeye ana miaka mingapi? (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeeleza na nirudie tena tunafanya kila linalowezekana tuhakikishe askari wetu wanakuwa na mahali pazuri pa kukaa. Ndiyo jibu sahihi, tunafanya kila linalowezekana askari wetu wawe na mahali pazuri pa kukaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili nalo ni kwa sababu yeye ni rafiki yangu namjibu, mpango gani? Mpango nimeueleza kwenye jibu langu la msingi na nimhakikishie tu kwamba tutafanya kwa jinsi tulivyoeleza katika mpango wetu kuhakikisha kwamba askari wote wanapata nyumba nzuri na mahali pazuri pa kukaa.