Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Faida Mohammed Bakar

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR aliuliza:- Je, ni lini Benki ya Wanawake itaanza kutoa huduma zake Zanzibar?

Supplementary Question 1

MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri Kigwangalla, kwa niaba ya wananchi na wanawake wa Zanzibar, tunapenda kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuridhia kufungua Benki ya Wanawake, Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kumshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kukubali kutoa ofisi yake. Ahsante sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa baadhi ya Wabunge wanawake wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tulikuwa ni miongoni mwa waanzilishi wa benki hii kwa kutoa hela zetu kuweka hisa, lakini mpaka hii leo hatujui chochote kinachoendelea na hatujapatiwa gawio la hisa kutokana na Benki hii ya Wanawake.
Je, Serikali itaanza lini au inasema nini kuhusu gawio letu la hisa la wananchi wote, sio lazima Wabunge tu na wananchi wote? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)

Name

Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote kabla sijajibu swali lake, nitumie nafasi hii kwa namna ya kipekee kumpongeza sana aliyekuwa Waziri wa Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Mheshimiwa Sophia Mnyambi Simba, kwa chachu ya kuanzisha benki hii. Pia nimpongeze aliyekuwa Naibu Waziri wa Wizara hiyo ambaye sasa ni bosi wangu, Mheshimiwa Ummy Ally Mwalimu, kwa kutia chachu ya kukua kwa kasi ya benki hii. Zaidi nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, kwa kujitolea kufanya uamuzi makini wa kuchangia mtaji kwenye benki hii wa shilingi bilioni mbili kila mwaka. Naamini Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ataendelea kuipa uwezo benki hii kwa kuendelea kutekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwapongeze Wabunge wote wa Viti Maalum ambao nao kwa dhati kabisa waliamua kujitolea michango kwa kununua hisa kwenye benki hii. Kilichokwamisha wao kupata hisa hizi rasmi kwa maana ya utaratibu wa kisheria ni kwamba wakati benki inaanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Makampuni ya mwaka 2002, Cap. 212, ilikuwa imesajiliwa kama Private Limited Company. Kwa maana hiyo ilikuwa na benki binafsi ya wanahisa binafsi ambao walikuwa wameteuliwa kuianzisha benki hiyo na Mheshimiwa Rais wa wakati huo na kwa maana hiyo Wabunge walipochangia michango ile kwa maana ya kununua hisa kwa ajili ya kujiunga kwenye benki hii haikuweza kurasimishwa kwa haraka kwa sababu ya utaratibu wa kisheria.
Mheshimiwa Naibu Spika, kumbukumbu za Wabunge wote walionunua hisa pale awali wakati benki inaanzishwa zipo. Machi, 2012 baada ya kutambua michango hii ya Waheshimiwa Wabunge wote wa Viti Maalumu bila kujali itikadi zao, ilionekana kwamba usajili wa benki kwa mujibu wa sheria ubadilike, badala ya kuwa private sasa iwe public kwa maana ya kuwa Public Limited Campany ambapo kwa mujibu wa sheria sasa inaruhusiwa kuongeza wanahisa wengi zaidi. Lakini benki imeenda mbele, sasa hivi itakuwa benki ya wananchi wote kwa maana ya kwamba tuna mkakati wa ku-issue IPO, kufanya Initial Public Offering kwenye Soko la Hisa ili wananchi wengi zaidi wanunue hisa na iweze kuwa na mtaji mkubwa na kufika kwa wananchi wengi zaidi. Kwa maana hiyo, wale Wabunge walionunua hisa wakati huo, watapewa hati rasmi za hisa zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kupewa hati rasmi za hisa na wananchi wengine watakaonunua hisa nao pia watapewa hati za hisa hizo. Sasa benki kwa kuwa imeanza kupata faida kuanzia mwaka jana na mwaka huu, itaweza kutoa gawio. Huo ulikuwa ni utaratibu wa kisheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakusukuru kwa kunipa nafasi hii.