Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:- Watu wenye ulemavu wanapitia changamoto nyingi sana katika safari zao za kimaisha na mojawapo ni miundombinu isiyo rafiki kwa ajili ya kupata elimu:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua matatizo hayo ili kuwawezesha watu wenye ulemavu kufurahia matunda ya elimu kwa kuweka mazingira mazuri yatakayowasaidia kupata elimu?

Supplementary Question 1

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Vilevile, naipongeza Serikali kwa jitihada za kutatua matatizo hasa changamoto zinazowakabili watoto wenye ulemavu. Nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Lugha ya alama ni changamoto kwa watoto viziwi ambao wengi wao huishia elimu ya sekondari na kushindwa kuendelea na elimu ya juu kutokana na Wahadhiri wengi kutokujua lugha ya alama. Je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa wa kuingiza lugha ya alama katika shule za msingi, sekondari na katika Vyuo vya Ualimu hapa nchini?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, ni Vyuo vingi hasa vyuo binafsi, mazingira yake sio rafiki kwa wanafunzi wenye ulemavu. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwepo mwongozo utakaoviongoza vyuo vyote kuzingatia mahitaji na hasa miundombinu kuwa rafiki kuwatimizia majukumu yao hasa watoto hawa wenye ulemavu ili waweze kusoma vizuri? Ahsante.

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ni kweli kabisa lipo hilo tatizo, kutokana na kwamba kama inavyojulikana kwa muda hawa watu wenye ulemavu wamejikuta hawapati elimu za aina mbalimbali kutokana na mahitaji yao. Sasa hivi Wizara inachofanya, kwanza imetambua hayo mahitaji maalum ya aina mbalimbali na kupitia bajeti hii, tumeshatenga fedha kwa ajili ya kuandaa mitaala kwa ajili ya kutoa mafunzo maalum kwa ajili ya Walimu pamoja na wanafunzi wenyewe katika shule husika, vile vile, kwa ajili ya kununua vifaa ambavyo vitatumika katika kufundishia.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili, juu ya miundombinu rafiki, niseme tu kwamba, hilo suala limekuwa likijitokeza. Ninayo mifano mingi ambayo nimeishuhudia mwenyewe kwamba, watu wanapojenga shule au taasisi maalum, wanasahau kabisa kwamba kuna siku wanaweza wakawa na mwanafunzi ambaye ni mlemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, unakuta hata mtu anapojenga iwe ni ghorofa, iwe ni choo, haangalii kama atakuja mwanafunzi mwenye wheel chair, atafika vipi huko au angalau kuwashusha wale wanafunzi badala ya kusoma ghorofani waweze kusoma katika madarasa ya chini ili nao waweze kupata hiyo fursa. Kwa hiyo nitoe wito, tujue kwamba, ulemavu siyo jambo la kujitakia bali ni mapenzi ya Mwenyezi Mungu katika kuonesha kazi za uumbaji wake. Ni vyema tuwafikirie na kuwajali watu wenye ulemavu.

Name

Fakharia Shomar Khamis

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:- Watu wenye ulemavu wanapitia changamoto nyingi sana katika safari zao za kimaisha na mojawapo ni miundombinu isiyo rafiki kwa ajili ya kupata elimu:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua matatizo hayo ili kuwawezesha watu wenye ulemavu kufurahia matunda ya elimu kwa kuweka mazingira mazuri yatakayowasaidia kupata elimu?

Supplementary Question 2

MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa elimu ndiyo ufunguo wa maisha, je, Wizara imechukua hatua gani kuwahamasisha wazazi wenye watoto walemavu kutoa kipaumbele kwa watoto hao kupata elimu?

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kweli Wizara yetu imekuwa ikizungumza katika nyakati mbalimbali kupitia vyombo vya habari, lakini pia kupitia Wizara nyeti sana hii ya Sera, Bunge, Watu wenye Ulemavu na mambo yote yaliyoko kule, kwamba tumekuwa tukishirikiana pamoja na Waheshimiwa Mawaziri wenzangu kuhakikisha kwamba tunahamasisha jamii kwa kupitia makongamano, mikutano na kupitia Bunge lako Tukufu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama hivi tunavyoona, kwamba tuna Waheshimiwa Wabunge wenye ulemavu, mtu anaanza kuona kwamba kumbe mwanangu nikimsomesha, kumbe nikimsaidia, kuna siku ataweza kuwa Mbunge, Waziri au kiongozi yeyote yule. Kwa hiyo, kwa hali hiyo niwaambie sana Waheshimiwa wazazi mlio huko, naomba muwatoe watoto wenu wenye ulemavu barabarani, msiwape kazi ya kuomba, hiyo sio kazi yao. Ninyi ndiyo kazi yenu mfanye kazi na hatimaye iweze kuwasaidia watoto hawa wenye ulemavu.

Name

Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Primary Question

MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:- Watu wenye ulemavu wanapitia changamoto nyingi sana katika safari zao za kimaisha na mojawapo ni miundombinu isiyo rafiki kwa ajili ya kupata elimu:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua matatizo hayo ili kuwawezesha watu wenye ulemavu kufurahia matunda ya elimu kwa kuweka mazingira mazuri yatakayowasaidia kupata elimu?

Supplementary Question 3

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu ina shule ya viziwi kule Dongobesh na pia ina Kitengo cha Elimu ya Watoto Walemavu katika Shule ya Msingi Endakkot na kwa kuwa kundi hili ni kubwa katika jamii; je, Serikali haioni umuhimu mkubwa wa kuweka Kitengo cha Elimu kwa Walemavu katika kila halmashauri kwa shule mojawapo ili kundi hili lililokosa nafasi wapate huduma stahiki?

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ni kweli kuna umuhimu mkubwa sana kwa kila halmashauri kuwa na shule yenye kitengo cha watu wenye ulemavu. Hata hivyo, niseme tu kwamba, kuwa na kitengo ni kitu kimojawapo, lakini kuangalia hivyo vitengo vikafanya kazi iliyokusudiwa ni hatua ya pili.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningetamani kuona kwamba, kwanza kila halmashauri iwatambue hawa watoto wenye ulemavu pamoja na mahitaji yao yanayohusika. Baada ya hapo, katika hizo shule zinazotengwa, naomba ziwasilishwe kwenye Wizara yetu pamoja na Wizara ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kuona kwamba vinawekwa vifaa vinavyohusika na kukidhi mahitaji yanayostahili, tukifanya hivyo tutakuwa tumetatua matatizo makubwa ya watu wenye ulemavu.