Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Faida Mohammed Bakar

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FAIDA MOHAMED BAKAR (K.n.y. MHE. KHATIB SAID HAJI) aliuliza:- Serikali imekuwa ikitoa huduma za dawa bila malipo kwa baadhi ya maradhi kama vile UKIMWI, TB na kadhalika:- (a) Je, ni maradhi ya aina gani yaliyo katika orodha ya kupatiwa dawa bila malipo? (b) Je, ni kwa kiasi gani Serikali imefanikiwa kufikia malengo katika mpango huo wa kusaidia wananchi kupata dawa hizo?

Supplementary Question 1

MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa kunipatia nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza baada ya majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi juzi tu, gazeti moja la Mwananchi lilitoa habari kuwa, huduma za dawa zitatolewa yaani kwa kununuliwa katika hospitali kuu ya Muhimbili. Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na habari hizo?
Swali la pili, kwa kuwa ajali ni jambo baya sana, na ajali huweza kutokea kwa mtu yeyote na wakati wowote ule, na kwa kuwa watu wanaopata ajali huwa wanalipishwa dawa hata kama ni kwa baadae. Je, Serikali itakubaliana nami kwamba sasa ni wakati muafaka wa kuingiza katika mfumo kwa hao watu wanaopata ajali, kutolipa malipo ya huduma na dawa? (Makofi)

Name

Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NAWATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya MheshimiwaFaida Mohammed Bakar, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kuhusu taarifa za Hospitali ya Taifa ya Muhimbili imetoa tamko kwamba itaanza ku-charge dawa zote; naomba nirejee maelezo niliyoyatoa hapa juzi, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Mrisho Kikwete, Mbunge wa Chalinze. Kuhusu jambo hilo hilo ambalo leo tena Mheshimiwa Faida Mohammed Bakar analiuliza,kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, haijafanya mabadiliko yake kwenye Sera ya Taifa ya Afya ya mwaka 2007; na nimeeleza kwenye majibu yangu ya msingi kwamba kuna magonjwa ambayo yanapewa msamaha kwa mujibu wa sera hiyo, kwenye ile Ibara ya 5.4.8.3 cha sera hiyo ambapo tunaelezea makundi ambayo yanapaswa kupata huduma za afya kwa msamaha.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitarudia tena kuyataja kwa faida ya Wabunge lakini pia kwa faida ya watanzania wote. Kwamba wagonjwa wote wanaoumwa magonjwa ya muda mrefu, yaani chronic illnesses, wanapewa msamaha na Sera ya Taifa ya Afya; na kwa kutaja machache tu nitasema kuna magonjwa ya moyo, magonjwa yote ya akili, magonjwa ya saratani, kifua kikuu, ukoma, UKIMWI, pumu, sickle cell, magonjwa yote haya yanapewa msamaha kwa mujibu wa Sera ya Afya. Lakini pia kuna makundi maalum machache nayo yanapewa msamaha na Sera ya Afya na makundi hayo ni makundi ya wazee wenye umri wa miaka zaidi ya 60, watoto wenye umri chini ya miaka mitano, akina mama wajawazito na watu wenye uwezo mdogo wa kifedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama kuna gazeti liliandika taarifa hizo, basi gazeti hilo linapotosha na taarifa hizo haziwezi kuwa sahihi, na mimi kama Naibu Waziri mwenye dhamana ya kusimamia utekelezaji wa sera ya afya hapa nchini, ninarejea tena kutoa msimamo wa Serikali kwamba sera yetu haijabadilika na kwa maana hiyo makundi haya ambayo yanapewa msamaha na Serikali kwa mujibu wa sera yataendelea kupata msamaha huo kwa mujibu wa sera yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, kuhusu ajali. Matibabu yote ya dharula kwa mujibu wa Sera ya Afya hapa nchini ni bure, mtu akiugua ghafla achilia mbali kupata ajali; akiugua tu ghafla, akaanguka, jambo la kwanza akifika hospitalini atapewa tiba hiyo bure bila kuulizwa gharama yoyote ile. Huo ndio utaratibu na ikitokewa mahala mtu akawa-charged naomba azifikishe taarifa hizo kwangu na mimi nitachukua hatua hapo hapo.