Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Augustine Vuma Holle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kasulu Vijijini

Primary Question

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE Aliuliza: - Je, ni lini Mkoa wa Kigoma utaunganishwa na umeme wa Gridi ya Taifa?

Supplementary Question 1

MHE. VUMA A. HOLLE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, Wilaya ya Kasulu kuna mgao mkubwa sana wau meme. Yako maeneo hasa maeneo ya Makele, kila ikifika jioni lazima umeme ukatike na wananchi wanakosa huduma ya kuangalia tarifa ya habari, lakini na maeneo mengine mengi ya Wilaya ya Kasulu. Nataka kujua majibu ya Serikali nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba tena wa muda mfupi, kwamba unakomesha mgao huu?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Mkoa wa Kigoma, REA awamu ya III imeanza kwanza kwa kuchelewa lakini pili maeneo mengi hayajafikiwa na mradi, lakini pia mradi huo unasuasua. Je, Waziri yupo tayari kutuma wataalam wake au yeye mwenyewe kuja Mkoa wa Kigoma hasa Kasulu Vijijini ili kuhakikisha kwamba anakutana na wakandarasi ili waweze ku-speed up utekelezaji wa mradi? Nashukuru sana.

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri wangu, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Vuma, Mbunge wa Kasulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Vuma pamoja na Wabunge wengine wote kutoka Kigoma, kwa kazi kubwa walizofanya katika kufuatilia Mkoa wa Kigoma kupata Gridi ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kulikuwa na changamoto kubwa sana ya kiumeme katika Mkoa wa Kigoma na Mkoa wa Katavi, lakini kama ambavyo limejibiwa kwenye swali la msingi, Serikali imeanza kutekeleza mradi wa kupeleka umeme wa Gridi katika Mkoa wa Kigoma kutoka Tabora. Tumeanza kujenga toka mwaka jana mwezi Januari, kutokea Urambo, tunajenga sub-station na tumeshaanza kujenga na tumeshaanza kujenga sub-station ya pili tunajenga Nguruka na ujenzi unaendelea na sub-station ya tatu tunajenga Kidahwe Mjini Kigoma, nako ujenzi unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunajenga njia ya kusafirisha umeme mkubwa kilovoti 400 kutoka Kigoma na kusambaza maeneo yote ya Wilaya ya Kigoma ikiwemo, Kasulu, Kibondo, Kakonko na maeneo mengine na ujenzi umeshaanza. Naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Vuma, Mheshimiwa Profesa Ndalichako na Waheshimiwa Wabunge wengine wa Kigoma kwamba tunatarajia kukamilisha mwakani mwezi Desemba, shughuli zote na Gridi ya Taifa itakuwa imefika kwenye Mkoa wa Kigoma.

Pia kwa upande wa matumizi pia ya umeme Kigoma kwa sasa wanatumia mashine za mafuta ni vema nikawaambia Waheshimiwa Wabunge ili wajue, ingawa uendeshaji kwa kweli ni mkubwa na kwamba tunatambua mahitaji ya umeme, hatuna namna mbali na kuwalisha umeme kwa utaratibu huo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, mahitaji ya wananchi wa Kigoma kwa siku ni megawatt 5.2 pamoja na kwamba mashine tulizonazo pale ni megawatt 2.6 na tunazidisha mara nne zinafikisha kama megawatt 8 lakini kwa sababu ya njia kuwa ndefu na umeme unachotwa kwenye mafuta bado umeme ule unakuwa hauna nguvu. Ndio maana mnaona mara nyingi umeme unakatika sio mgao isipokuwa umeme unakatika kutokana na njia kuwa ndefu na source yake ni mafuta. Nimeona niliweke vizuri suala hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, maeneo ya REA yaliyobaki ni kweli katika Mkoa wa Kigoma na hasa Kasulu kwa Mheshimiwa Vuma, Mheshimiwa Vuma ana vijiji 61 na tumeshapeleka umeme kwenye vijijini 42 bado vijiji 19 na tulizindua pale Lusesa na Lusesa kazi inaendelea. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Vuma anavyofuatilia masuala haya na kwa sababu utekelezaji wa umeme katika vijiji vyote kama alivyoeleza Mheshimiwa Naibu Waziri unaanza tarehe 15 mwezi huu na tunarajia ndani ya miezi 18 kukamilisha vijiji vyote katika nchi yetu, vijiji vyote vya Mheshimiwa Vuma vitapata umeme mapema sana. Hata hapo Makere umeme unaokwenda kutoka pale mpaka mpakani mwa Rwanda na Burundi tutaunganisha na majirani zetu wa Rwanda na Burundi kupitia mradi wa Rusumo ili maeneo ya mipakani mwa Tanzania, Rwanda na Burundi nayo yapate umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)