Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Juma Kombo Hamad

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wingwi

Primary Question

MHE. JUMA KOMBO HAMAD aliuliza:- Ni muda mrefu Serikali ilikuwepo kwenye mchakato wa kupata Vazi la Taifa. (a) Je, Serikali imefikia hatua gani ya mchakato huo? (b) Je, ni lini Watanzania wategemee kuwa na Vazi la Taifa?

Supplementary Question 1

MHE. JUMA KOMBO HAMAD:Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, nina maswali mawili madogo sana ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa jibu la Mheshimiwa Naibu Waziri, ni kusema kwamba Serikali imeshindwa kuwapatia watanzania Vazi la Taifa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali namba mbili, nilitaka kujua tu, Serikali katika mchakato huu ambao kwa mujibu wa Mheshimiwa Naibu Waziri amesema ulianza mwaka 2011, ni muda mrefu kidogo na ni mchakato ambao ulichukua muda. Anaweza kutueleza ni fedha kiasi gani za Watanzania ambazo zilitumika katika mchakato huo ambao hadi sasa haukukamilika na ile ndoto ya Watanzania kuwapatia vazi la taifa sasa imepotea? Nashukuru.

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la kwanza amezungumza kwamba Serikali imeshindwa kukamilisha mchakato wa kupata Vazi la Taifa. Napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba Serikali haijashindwa na Serikali haijawahi kushindwa na jambo lolote, hususan Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo, kitu ambacho tunakifanya, kama ambavyo nimejibu yangu ya msingi kwamba kwa sasa hivi tumeshaufufua upya huo mchakato na nikuhakikishie kwamba Mheshimiwa Mbunge kwamba mchakato huo, muda si mrefu utaenda kukamilika.

Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuweza kutoa wito kwa Maafisa Utamaduni wote wa Mikoa yote ya Tanzania, lakini vilevile kwa Makatibu Tawala wote wa Mikoa ambao ndiyo tumewakabidhi hilo jukumu, ili Vazi la Taifa liweze kupatikana kuhakikisha kwamba wanasimamia huo mchakato uweze kukamilika kwa haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nikija kwenye swali lake la pili, kwa sababu ametaka kujua kuhusiana na fedha ambazo zimetumika kuanzia mchakato ulipoanza mwaka 2011. Niseme kwamba kwa sababu ni suala la kitakwimu, naomba baada ya hapa Mheshimiwa Mbunge tuweze kuonana ili niweze kukupatia hiyo takwimu. Ahsante.

Name

Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Primary Question

MHE. JUMA KOMBO HAMAD aliuliza:- Ni muda mrefu Serikali ilikuwepo kwenye mchakato wa kupata Vazi la Taifa. (a) Je, Serikali imefikia hatua gani ya mchakato huo? (b) Je, ni lini Watanzania wategemee kuwa na Vazi la Taifa?

Supplementary Question 2

MHE. MWIGULU L. NCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika,kwa kuwa Watanzania wanapokwenda nje ya nchi sasa hivi wanatumia scarf, t-shirt za bendera za Taifa na tai kama hizi, ile Mwigulu style na wanatambuliwa kuwa ni Watanzania.

Kwa nini Serikali isiidhinishe tu kwamba scarf, tai za Taifa na bendera za Taifa ndiyo itakuwa vazi la taifa kwa sababu nchi hii hawawezi wakavaa uniform ili kutambulisha kwamba lile ndiyo Vazi la Taifa? (Makofi)

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Mbunge, kwa sababu yeye amekuwa mzalendo kwelikweli katika kuhamasisha masuala ya utamaduni nchini Tanzania, lakini vilevile kama amabvyo ametaka kujua kwamba vazi ambalo amekuwa akilitumia yeye binafsi mara nyingi, kwa maana ya vazi la tai ambayo ina bendera ya Taifa, kwanini sisi kama Wizara tusilirasimishe rasmi liweze kuwa Vazi la Taifa.

Niseme kwamba kwa sababu kwa sasa hivi kuna mchakato ambao tumeshauanzisha na tumeshaufufua ambao ni mchakato mpya, lakini pia niseme kwamba maoni ambayo ameyatoa tunayachukua na tutayafanyia kazi ili tuangalie kama kuna huo uwezekano. Ahsante sana.