Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Primary Question

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA III katika Kijiji cha Hemsambia na Vitongoji vyake vyote?

Supplementary Question 1

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, pamoja na majibu mazuri ya Wizara ambayo yanatupa matumaini, nina maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa survey iliyofanyika Hemsambia ilifanyika kwa vitongoji viwili na kuacha vitongoji vingine vitano. Je, Waziri anatuthibitishia kwamba, kwa azma ile ya kuhakikisha kwamba, kila kijiji kinapofikiwa lazima kijiji chote kipate umeme; Je, vitongoji hivi vitajumuishwa kwenye kupatiwa umeme?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, wakati tunapeleka umeme kwenye Kata ya Bosha maeneo ya Vitongoji vya Miyongwe, Kwemsakazi, Kwashemwaondwa na Kibago B yalirukwa, lini maeneo haya yatapatiwa umeme?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya swali la msingi la Mheshimiwa Kitandula, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Luka Kitandula, Mbunge wa Mkinga na pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, katika maswali yake mawili ya nyongeza kwanza ni kweli, kwenye Kijiji cha Hemsambia tulifanya survey vitongoji viwili na tukabakiza vitongoji vitano ambavyo tayari wakandarasi tumeshaviingiza kwenye
marekebisho na yanafanyiwa kazi. Na hivi sasa Mheshimiwa Mbunge, pamoja na kupongeza, tulipokuwa katika jimbo lako wiki iliyopita tulitoa maelekezo na wakandarasi wameshaanza kuyafanyia kazi. Kwa hiyo, niwape taarifa tu Wananchi wa vitongoji vitano vya Kijiji cha Msambia kwamba, vitongoji vyote katika kijiji hicho vitafanyiwa kazi na vitakamilika mwezi Septemba mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, katika swali la msingi la pili la Mheshimiwa Mbunge, ni kweli tunazo kata tano muhimu sana kwa Mheshimiwa Mbunge, lakini Kata ya Bosha yenye vijiji vinne vikiwemo Kijiji cha Kwashemhonda, pamoja na Kwesekazi, pamoja na Kibango vimeshaanza kufanyiwa kazi na Shirika la Umeme – TANESCO kwa sababu, sasa hivi bei ni ileile 27,000/=. Na jana tumewasiliana na Mheshimiwa Mbunge alikuwa kufuatilia na TANESCO pamoja na wataalamu wameshaingia site kuanzia leo. Kwa hiyo, ni matumaini yetu Mheshimiwa Mbunge na Wananchi wa Mkinga muwe na matumaini kwamba, Kata na Vijiji vyote vya Bosha vinakwenda kupatiwa umeme mwisho wa mwezi Disemba mwaka huu.

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA III katika Kijiji cha Hemsambia na Vitongoji vyake vyote?

Supplementary Question 2

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, Mji wa Tarime kwa hadhi ya kuwa mji ulitakiwa kuwa na umeme kwa zaidi ya asilimia 90, lakini maeneo yenye umeme ni chini ya asilimia 40. Na kwa sababu, Waziri wakati anajibu baadhi ya maswali hapa amehakikisha kwamba, na akatoa instructions kwamba, vituo vya afya, zahanati, shule kama sekondari vihakikishwe vinapewa umeme.

Mheshimiwa Spika, kwenye Jimbo langu Kata ya Nkende kuna kituo cha afya, kuna sekondari na kuna shule za msingi, lakini hazina umeme. Kata ya Kenyamanyori ina shule ya sejkondari, ina shule za msingi, ina kituo cha afya hakina umeme na Kata ya Kitale kuna Sekondari ya nkongole na Mogabili na vituo vya afya pale, zahanati hazina umeme, vilevile na Kata ya Nyandoto.

Mheshimiwa Spika, ningependa kujua sasa ni lini, na nimekuwa nikiuliza haya maswali, ni lini huu umeme wa REA utaweza kufika kwenye hayo maeneo ambayo hayana umeme kabisa, ili sasa hizo zahanati, vituo vya afya, sekondari na shule za msingi ziweze kupata umeme, pamoja na Wananchi? Ahsante.

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza pamoja na kuwapongeza Wananchi wa Tarime kwa kupelekewa umeme katika vijiji vyote iko changamoto katika kata ambazo amezitaja, hasa Kata ya Nkende pamoja na Kenyamanyori na Kitale. Nimeshazungumza mpaka na Mkurugenzi alipie zahanati na shule zipelekewe umeme kwa sababu, vijiji na vitongoji vya maeneo hayo vina umeme. Kwa hiyo, nikupongeze Mheshimiwa kwa kufuatilia, lakini nikuombe uwasiliane na Mheshimiwa Mkurugenzi na Halmashauri ya Kijiji cha Nkende pamoja na Kijiji cha Kitale na Kenyamanyori waweze kulipia ili shule na zahanati zipelekewe umeme.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili, nyongeza ya hilo, nitapenda nitembelee mimi mwenyewe ili nikatoe maelekezo kwa wakurugenzi waweze kulipia. Mheshimiwa Esther hata akibaki nitakwenda mwenyewe ili kusudi maeneo hayo na zahanati ziweze kupatiwa umeme, ahsante sana. (Makofi)

Name

Hussein Nassor Amar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyang'hwale

Primary Question

MHE. DUNSTAN L. KITANDULA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA III katika Kijiji cha Hemsambia na Vitongoji vyake vyote?

Supplementary Question 3

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Nyanghwale ina vijiji 62 na mpaka kufikia leo hii ni vijiji saba tu ambavyo vimeshawashwa umeme na vijiji 13 tayari nguzo zimeshasimama. Nimeongea na mkandarasi kwa nini hajawasha vile vijiji 12 akadai kwamba, kuna upungufu wa nyaya.

Je, Waziri anatuambia nini kuhusu upungufu huo wa nyaya?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza kwa taarifa hiyo nashukuru kuipokea, kwanza umenipa jukumu la kufuatilia, nikuhakikishie nitalifuatilia hilo.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusiana na upungufu wa nyaya naomba nitoe taarifa kupitia Bunge lako Tukufu na kwa Watanzania hivi sasa hapa nchini hatuna shida na nyaya wala nguzo wala mita, changamoto inaweza ikawa ni utaratibu wa wakandarasi wenyewe namna ya kuhifadhi hivyo vifaa.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii Mheshimiwa Mbunge nimfuatilie mkandarasi tumfuatilie tujue changamoto ni nini, lakini tunachomuagiza kupitia Bunge lako Tukufu, napenda nichukue nafasi hii kumuagiza Mkandarasi wa White City anayetekeleza Mradi wa REA katika Mkoa mzima wa Geita, ikiwemo na Nyanghwale, achukue hatua za kuhakikisha vifaa vyote vinapatikana site na kazi ikamilike ndani ya wakati.