Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Augustine Vuma Holle

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kasulu Vijijini

Primary Question

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE aliuliza:- World Vision wamejenga Chuo cha Ufundi katika Kata ya Nyamidaho na kukikabidhi kwa Halmashauri ya Kasulu DC:- Je, kwa nini Serikali isimalizie ujenzi wa miundombinu midogomidogo na hatimaye kukifanya kuwa Chuo cha Ufundi cha Serikali?

Supplementary Question 1

MHE. AUGUSTINE V. HOLLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nishukuru kwa majibu mazuri na niishukuru Serikali kwa shilingi milioni 500 ambayo mmetuletea kwenye Chuo cha Nyamidaho, naamini kwamba mwakani kinaanza kufanya kazi kama alivyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, ni dhahiri kwamba hata baada ya kupokea fedha hizo, ujenzi utakapokuwa umekamilika, bado tutakuwa na uhitaji wa jiko, bwalo la kulia chakula, bweni la wanafunzi wa kiume pamoja na uzio kwa ajili ya usalama wa wanafunzi ambao watakuwa wanasoma kwenye chuo kile pamoja na nyumba za watumishi, maana hakuna mpango wa kujenga nyumba hata moja ya watumishi. Je, Serikali ina kauli gani kuhusu haya mahitaji ambayo yatakuwa yamebakia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Waziri yuko tayari kuongozana na mimi kwenda kuona mazingira jinsi yalivyo ili iweze kutoa msukumo katika kumalizia mambo haya na kuweka mazingira mazuri kwa ajili ya watoto kusoma kwenye Chuo cha Nyamidaho?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Vuma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utaniruhusu, kabla ya kujibu maswali hayo, naomba nitumie nafasi hii kwa msisitizo mkubwa kueleza ni namna gani Mheshimiwa Mbunge amehusika katika kupatikana kwa chuo hiki. Kwa kweli lazima niseme, kama isingekuwa yeye, kwa namna alivyokuwa anatusumbua, mpaka pale ofisini anafahamika kama king’ang’anizi, chuo hicho kisingepatikana. Naomba nitumie nafasi hii kumpongeza na nimuombe Mungu wapiga kura wake wasikie kwamba kwa kweli amejitahidi na napenda kumpongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kama Serikali iko tayari kuongeza majengo na miundombinu mingine ambayo bado kuna upungufu, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba punde chuo kitakapoanza mwaka 2020 kama tunavyotarajia, tutaangalia upungufu uliopo na kuendelea kuboresha na kuongeza kadri uwezo wa fedha utakavyoruhusu. Kwa hiyo, naomba nihamhakikishie kwamba hatutaishia hapa, tutaendelea kukiboresha chuo kile ili Wanakasulu na Watanzania wengine waweze kusoma katika mazingira mazuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuandamana naye, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba niko tayari kuandamana naye. Pia najua kwenye mkoa wake wapo vilevile Wabunge wa Viti Maalum ambao nao vilevile wamekuwa wakisaidia kusukuma ujenzi wa vyuo hivi, nao vilevile wakiwepo itasaidia tutaandamana kwenda kuangalia chuo hicho. Nashukuru sana.