Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:- Moja kati ya vigezo vya “Capital Development Grant Assessment”ni namna Halmashauri inavyoweza kutoa taarifa kwa wananchi juu ya mtiririko wa fedha ambazo Serikali imepeleka katika Halmashauri na miradi iliyokusudiwa kutekelezwa:- (a) Je, kwa nini mchakato huo ulisitishwa? (b) Je, Serikali haioni umuhimu wa kurejesha mchakato huo ambao utakuwa ukiongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali nchini?

Supplementary Question 1

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nilikuwa na maswali madogo mawili ya nyongeza. Ni hatua zipi zilizochukuliwa kwa Wakurugenzi walioshindwa kufikia malengo ya ukusanyaji mapato; kuchangia asilimia 40 katika miradi ya maendeleo; na kuchangia asilimia 10 kwa akina mama, watu wenye ulemavu na vijana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, katika nafasi za Wakuu wa Idara zilizo wazi Serikali imechukua hatua gani kuhakikisha zinajazwa na watumishi wenye sifa za kuwa Wakuu wa Idara ili kuwepo na uwajibikaji katika matumizi ya fedha za maendeleo ukizingatia Serikali inapeleka fedha nyingi sana katika miradi ya maendeleo?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mheshimiwa Leah Jeremia katika swali lake, anataka kujua ni hatua gani zimechukuliwa kwa Wakurugenzi na Watumishi wengine ambao wameshindwa kupeleka asilimia 40 na asilimia 10 kama ambavyo ndivyo ilivyo maelekezo ya Serikali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba hata hivi karibuni Mheshimiwa Waziri wa Nchi alitoa taarifa ya tathmini ya makusanyo ya Halmashauri mbalimbali na Halmashauri ya kwanza mpaka za mwisho zimetajwa na alitoa muda ambao Halmashauri watachukua hatua kurekebisha mapato hayo na kila Mkurugenzi amepaswa kujieleza na kuonesha mikakati hiyo. Kwa hiyo, hatua zinachukuliwa na wana maelekezo mahususi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ni kweli kwamba kuna fedha zimetengwa asilimia 40 ili ikaendeshe miradi ya Halmashauri. Tumetoa maelekezo, sisi viongozi wa Wizara hii, sisi Manaibu wenzake na Watendaji wengine, tukifanya ziara kwenye Halmashauri zetu, pamoja na kwenda kukagua fedha kutoka Serikali Kuu, ni lazima pia kila Halmashauri itupeleke kwenye mradi mmojawapo ambao ni own source; fedha ambazo wamekusanya kutoka kwa wananchi, zimefanya miradi? Hii ni ili tuwe na connection kati ya fedha ambayo inatolewa kama kodi, lakini pia na miradi ya maendeleo, kweli jambo linafanyika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni kweli kwamba kuna maeneo mengi wako Wakuu wa Idara na Vitengo wanakaimu na tumetoa maelekezo kufanyike utaratibu, wale ambao wana sifa wathibitishwe kazini na wale ambao hawana sifa waondolewe ili tuwe na watu ambao kimsingi wana uwezo wa kufanya maamuzi. Kwa sababu ni kweli kwamba kama mtu anakaimu, wakati mwingine amekaimishwa na Mkurugenzi, akipingana naye katika mambo fulani, anamwondoa anamweka mtu mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunataka watu wawe na uwezo, wakaelezee Idara, wawe na mipango na pia waweze kubuni kwa sababu ofisi ni ya kwake..

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.