Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Rose Cyprian Tweve

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza:- Imekuwa ni kawaida sasa kwa Askari wa Usalama barabarani kusimamisha magari ya usafiri wa Umma kama vile daladala na mabasi na kadhalika:- Je, ni lini Serikali itaandaa utaratibu wa kuwa na Vituo Maalum vya Ukaguzi huo ili kuokoa muda wa wasafiri?

Supplementary Question 1

MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, nakubaliana kabisa na maelezo ya Mheshimiwa Waziri kuwa pale Polisi anapokuta kuna umuhimu wa kusimamisha gari ambalo limevunja sheria ni muhimu wafanye hivyo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuwa tumekuwa na hivi vituo maalum vya ukaguzi, sasa hivi kumekuwa na changamoto kubwa hasa kwenye mabasi ya daladala. Kumekuwa na unnecessary stop na kusababisha ucheleweshaji wa wananchi kwenda kufanya shughuli zao. Nitakupa mfano, unakuta daladala imesimamishwa na Traffic yuko pembeni ana-argue na Konda kwa nini hana proper uniforms? Haya ilibidi yafanywe kabla huyu abiria hajaingia kwenye gari.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, nilitaka kujua sasa kama Serikali na Jeshi la Polisi tumejipanga vipi kuhakikisha sasa tunakuwa na hii mandatory car inspection tofauti na utoaji wa stika wa sasa ukizingatia hizi stika zimekuwa zinatolewa kwenye magari yasiyo na viwango na kusababisha ajali kubwa za barabarani. Nakushuru sana.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa maswali yake mazuri sana na ya msingi. Baada ya pongezi hizo sasa nitoe majibu ya maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mbali ya sheria ambayo nimeinukuu inayotoa mamlaka kwa Askari kusimamisha gari popote anapoitilia hitilafu, ambapo madhumuni ya sheria ile kimsingi inatokana na baadhi ya madereva wetu nchini ambao wamekuwa wakikiuka Sheria za Barabarani mara kwa mara, kwa mfano, utakuta mtu anaendesha gari kwa speed. Kwa hiyo, Askari akiona utaratibu wa uendeshaji kama huo, lazima achukue hatua.

Mheshimiwa Spika, kwanza nitoe wito kwa wananchi hasa madereva kutii Sheria za Barabarani ili kuepusha usumbufu. Pili, nataka nichukue fursa hii pia kutoa wito kwa Askari wetu wa usalama barabarani nchi nzima ambao kama wapo kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge najua atakuwa ame-experience hiyo, kama wapo ambao wanafanya utaratibu wa kusimamisha magari kiholela kwa kujifichia chini ya mwamvuli wa sheria hii bila kuwa na makosa yoyote, basi waache mara moja.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali lake la kuwa na utaratibu wa ukaguzi wa lazima, nataka nimwelezee Mheshimiwa Mbunge kwamba kama Serikali tumeshalitafakari kwa kina suala hilo na tunatambua kuwa na utaratibu wa ukaguzi wa lazima ni jambo ambalo ni muhimu na haliepukiki katika karne hii tuliyokuwa nayo, siyo tu kwamba litasaidia kutoa fursa kwa magari yetu kukaguliwa vizuri zaidi na hivyo kuwa na magari salama barabarani, lakini itasaidia kuiongezea mapato Serikali na hususani Jeshi la Polisi katika kukabiliana na changamoto mbalimbali ambazo tunazikabili. Kwa hiyo, kwa kutambua hilo tumekuja na mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza tunatamani kwamba katika mabadiliko ya sheria ambayo itakuja, utaratibu huo utakuwa unasimamiwa na baraza jipya la usalama barabarani ambalo tunatarajia lije na muundo mwingine. Kwa hiyo, ni Baraza Tendaji, lakini hata kama matamanio yetu hayo bado hayajafikiwa au yatakuwa yamechelewa kufikiwa, tumeshatoa maelekezo kwa Shirika la Jeshi la Polisi (Police Cooperation Soul) kuanza mchakato wa kuanzisha utaratibu huo wa ukaguzi lazima.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nichukue fursa hii vilevile kuwaelekeza Jeshi la Polisi kupitia Shirika hilo la Maendeleo kuharakisha huo mchakato ili uweze kuanza mapema ikiwezekana hata kabla ya Awamu hii ya Kwanza ya utawala wa Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli haijamaliza muda wake.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.

Name

Catherine Valentine Magige

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza:- Imekuwa ni kawaida sasa kwa Askari wa Usalama barabarani kusimamisha magari ya usafiri wa Umma kama vile daladala na mabasi na kadhalika:- Je, ni lini Serikali itaandaa utaratibu wa kuwa na Vituo Maalum vya Ukaguzi huo ili kuokoa muda wa wasafiri?

Supplementary Question 2

MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa vituo hivi vya ukaguzi wa magari barabarani siyo tu muhimu kwa wananchi vilevile ni muhimu sana kwa Askari wetu. Tunatambua kazi kubwa wanayofanya Askari wa Barabarani, lakini Askari hawa mara nyingi wanapopata ajali kulipwa haki zao inachukua muda mrefu. Kwa mfano tu, katika Mkoa wangu wa Arusha kuna Askari wengi waliopata ajali wakiwa kazini, lakini mpaka sasa hivi hawajalipwa stahiki zao.

Je, ni lini Serikali italipa maaskari ambao wamepata ajali kazini haki yao?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza lazima nikiri kwamba kulikuwa na changamoto za baadhi ya malipo ya stahiki mbalimbali za Askari wetu nchi nzima ikiwemo hii ambayo Mheshimiwa Mbunge ameizungumza, lakini lazima nichukue fursa hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano, lazima tujipongeze kwa pale ambapo tutafanya vizuri.

Mheshimiwa Spika, sehemu kubwa ya malimbikizo haya yameanza kulipwa na tunaamini kwamba kama kutakuwa kuna maeneo ambayo bado hayajakamilika, kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amezungumza, hii fidia ya Askari ambao wanapata ajali barabarani, basi tutakamilisha pale michakato mingine ikiwemo uhakiki pamoja na bajeti itakapokaa sawa.

Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Mbunge, kama ana maombi mahususi ya Askari ambayo anafahamu, basi aweze kutupatia ili tufuatilie tujue ni tatizo gani lililosababisha mpaka leo wawe hawajapatiwa stahiki zao?

Name

Masoud Abdalla Salim

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtambile

Primary Question

MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza:- Imekuwa ni kawaida sasa kwa Askari wa Usalama barabarani kusimamisha magari ya usafiri wa Umma kama vile daladala na mabasi na kadhalika:- Je, ni lini Serikali itaandaa utaratibu wa kuwa na Vituo Maalum vya Ukaguzi huo ili kuokoa muda wa wasafiri?

Supplementary Question 3

MHE. MASOUD ABDALLAH SALIM: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nami kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza. Pamoja na mabadiliko ya Muswada wa Sheria ya Usalama Barabarani ambayo inatarajiwa kuletwa hapa Bungeni, kuna malalamiko kwa madereva mbalimbali kwamba kosa lolote linapotokea, basi hakuna onyo, hakuna karipio. Karipio kubwa ni shilingi 30,000/= kwa haraka sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, inaonekana kwamba Polisi kwa wakati huu wanakusanya zaidi fedha kwa njia ya mapato zaidi kuliko kutoa karipio au kutoa onyo. PGO inaelekeza nini pale ambapo dereva amefanya kosa dogo la kwanza juu ya tatizo hili?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza ni imani yetu na imani ya Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote waliomo humu ndani kwamba mtu yeyote ambaye amechukua chombo cha usafiri na kuingia barabarani, maana yake kwanza amepata mafunzo ya kutosha na ana leseni.

Mheshimiwa Spika, hiyo ni moja, lakini la pili nina hakika Mheshimiwa Masoud anatambua kwamba tumekuwa tukifanya kazi kubwa sana ya kutoa elimu kuhusiana na usalama barabarani kwa kutumia njia mbalimbali ili kuwakumbusha wale madereva ambao wamekuwa wakighafirika katika kufuata Sheria za Usalama Barabara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa kuzingatia hayo mawili ni imani yetu kwamba mtu yoyote ambaye yuko barabarani anaendesha gari, anatambua wajibu wake na hivyo basi, sidhani kama ni jukumu la Jeshi la Polisi kuanza sasa kutoa elimu barabarani wakati mtu anahatarisha uhai wa raia wengine. Kwa hiyo, niendelee kusisitiza kwamba, ni vizuri kila mmoja ambaye anaendesha gari barabarani ajue kwamba kuna sheria na afuate sheria hizo.

Mheshimiwa Spika, jukumu la Jeshi la Polisi ni kuhakikisha kwamba wale ambao hawafuati sheria basi wanachukuliwa hatua kwa mujibu wa Sheria ikiwemo kutozwa faini. Hata hivyo, kuna baadhi ya changamoto ambazo tumekuwa tukizizungumza kila siku zinahitaji busara katika kuzikabili na niendelee kutoa wito kwa Askari Polisi kuzingatia busara wakati mwingine pale ambapo kuna matatizo ambayo yanaweza kuepukwa. Kwa mfano, kama ambavyo hata Mheshimiwa Waziri amekuwa akizungumza mara zote, unakamatwa mtu kwa kosa moja linazalisha makosa mengi, mtu anashtakiwa kwa makosa zaidi ya matano au sita. Kwa hiyo, mambo kama haya na mambo mengine ambayo yamekuwa kero kwa wananchi, hayo tumekuwa tukitoa maelekezo kwa Jeshi la Polisi litumie busara katika kuyakabili. Hata hivyo, tunataka kusisitiza umuhimu wa kutii sheria bila shuruti ili kuepusha ajali na kuokoa maisha ya Watanzania ambao wamekuwa wakipoteza maisha yao na kupoteza vyombo vyao kila siku.

Name

Joseph Osmund Mbilinyi

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mbeya Mjini

Primary Question

MHE. ROSE C. TWEVE aliuliza:- Imekuwa ni kawaida sasa kwa Askari wa Usalama barabarani kusimamisha magari ya usafiri wa Umma kama vile daladala na mabasi na kadhalika:- Je, ni lini Serikali itaandaa utaratibu wa kuwa na Vituo Maalum vya Ukaguzi huo ili kuokoa muda wa wasafiri?

Supplementary Question 4

MHE. JOSEPH O. MBILINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwenye barabara kuu ya Dar es Salaam - Morogoro tumeona sasa hivi wamefunga cameras. Sasa kwa nini camera zile zisifungwe nchi nzima ili sasa baada ya kufungwa zile camera Askari wanaokaa barabarani warudi vituoni, waende wakashughulike na masuala mengine ya wahalifu, kwa sababu msingi wao wa kukaa barabarani mkubwa ni speed. Sasa kwa kuwa zinafungwa camera ambazo zitakuwa zinachukua picha, zinatuma report kwenye database, wherever halafu zile report zinafuatiliwa hata baada ya wiki mbili, mwezi mmoja mtu anapelekea tiketi kwa mujibu wa details za gari lake. Ahsante sana.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMB0 YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Mbilinyi, Mbunge wa Mbeya Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, huu ndiyo mwelekeo wa Serikali yetu. Ni imani yetu kwamba, mambo yatakapokuwa yamekaa vizuri kibajeti tutafunga camera katika Miji mikuu yote na maeneo mengine nchi nzima. Kwa hiyo ni suala tu la kuvuta subira na kazi hiyo itafanyika hatua kwa hatua kadri ya hali ya fedha itakapokuwa inaruhusu.