Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Omari Mohamed Kigua

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilindi

Primary Question

MHE. OMARI M. KIGUA (K.n.y. MHE. MENDRAD L. KIGOLA) aliuliza:- Sekondari za Jimbo la Mufindi Kusini zinakabiliwa na tatizo la hosteli kwa ajili ya wanafunzi wanaotoka mbali:- Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga hosteli kwa kila sekondari katika Jimbo la Mufindi Kusini?

Supplementary Question 1

MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini nina maswali mawili, kama ifutavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, changamoto ya hosteli ambayo imejitokeza katika Jimbo la Mufundi Kusini haitofautiani sana na hali iliyopo katika Jimbo la Wilaya ya Kilindi. Ni ukweli usiopingika kwamba suala la hosteli ni kitu muhimu sana kwa sababu linachangia katika ufaulu wa watoto wetu. Je, Serikali iko tayari sasa kuhakikisha kwamba shule zote za vijijini ambazo watoto wanatembea kwa umbali mrefu zinakuwa na hosteli?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni kwamba katika Jimbo la Kilindi ipo Shule ya Kwamkalakala ambayo ni miongoni mwa shule kumi za mwisho ambazo zimefanya vibaya kutokana na kutokuwa na hosteli. Je, Serikali ipo tayari kutoa msaada maalum kuhakikisha kwamba shule ile inajengewa hoteli? Ahsante sana.

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge wa Kilindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza anataka kujua kama Serikali iko tayari kujenga hosteli kwenye shule zote za sekondari. Ni ukweli usiopingika kwamba hakuna mtu ambaye anapinga kutokuwa na hosteli katika shule zetu, zimeonesha tija na hasa kusaidia watoto wa kike waweze kupata muda mwingi wa kujisomea na kuweza kufanya vizuri katika masomo yao ambao pia wamekuwa wakifanya vizuri wale ambao wamebahatika kusoma vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao mpango kupitia EPforR, tumepeleka fedha katika hosteli zetu na Kilindi wamepata hosteli moja ambayo nilienda kuitembelea. Tutaendelea kufanya hivyo kwa mwaka wa fedha huu ambao tumeleta bajeti leo mezani kwenu, Waheshimiwa Wabunge watuunge mkono ikishapita tutaangalia namna ya kuboresha.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tunawaomba wadau wote na Watanzania popote walipo hili jambo la kujenga hosteli za watoto wa kike katika shule zetu ni jambo shirikishi. Sisi Wabunge tushirikiane na wananchi wengine na Serikali tutasaidia kadri tutakavyokuwa na uwezo wa fedha wa kufanya jambo hilo.