Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Khatib Said Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Konde

Primary Question

MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:- FIFA inatoa misaada ya fedha kwa Tanzania kupitia TFF:- Je, ni kiasi gani cha fedha TFF imekuwa ikiipatia Zanzibar kupitia ZFA?

Supplementary Question 1

MHE. KHATIB SAID HAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Swali langu nililomwuliza, ni kiasi gani cha mgawo wa fedha hizi za FIFA wamewahi kuipatia Zanzibar? Jibu lake, anakuja kusema kwamba kuanzia mwaka huu tutapata 1.25. Kwa hiyo, amekwepa kabisa kunijibu swali langu nililomwuliza. Nataka kujua: Je, mmewahi kuipatia mgawo wowote Zanzibar kutokana na misaada hii inayotoka FIFA?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Nataka nijue, kwa kuwa TFF siyo chombo cha Muungano, Mheshimiwa Waziri wa Michezo sio Waziri wa Muungano na Wizara ya Michezo siyo Wizara ya Muungano; kwa hiyo, anaposema sasa kwamba kuanzia msaada huu unaokuja, mgawo utaenda kwa ZFA na TFF, nataka nijue, mtatumia formula ipi wakati mkijua kwamba masuala ya michezo Zanzibar wana Wizara yao na Tanzania Bara wana Wizara yao: Je, hamwoni hapa kwamba kuna mkorogano ambao kwa miaka yote na ndio maana Zanzibar tunakosa msaada huu wa FIFA?

Name

Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikianza na swali lake la kwanza, ametaka kujua kwamba, ni kiasi gani? TFF imekuwa ikitoa misaada mbalimbali kwa Chama cha ZFA ambacho ni cha Zanzibar. Moja ya miradi ambayo tayari imeshapelekwa ZFA ni ujenzi na ukarabati wa Uwanja wa Gombani ambao uko Pemba. Kwa hiyo, siyo kweli kwamba TFF imekuwa haipeleki msaada Zanzibar, hapana.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili ambapo ameelezea kwamba suala la michezo siyo la Muungano, nadhani Mheshimiwa Mbunge alikuwa hajaelewa jibu langu la msingi ambalo nimelitoa. Ni kwamba, ZFA ni sehemu ya TFF. Kwa tafsiri hiyo basi, maana yake fedha ambazo zinaletwa TFF zinagawiwa kwa mashirikisho yote ikiwepo ZFA ya Zanzibar, lakini si kwamba, ZFA inaletewa fungu lake peke yake, hapana, kwa sababu, ZFA siyo mwanachama wa CAF, lakini ZFA vilevile siyo mwanachama wa FIFA. ZFA iko chini ya TFF.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)