Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Edwin Mgante Sannda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Primary Question

MHE. EDWIN M. SANNDA aliuliza:- Halmashauri ya Mji wa Kondoa imepata eneo la iliyokuwa kambi ya ujenzi wa barabara ya Mela – Bonga pale Kolo kwa ajili ya uanzishwaji wa Chuo cha VETA:- Je, ni lini Serikali itatekeleza azma hiyo?

Supplementary Question 1

MHE. EDWIN M. SANNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nachukua fursa hii kushukuru na kupongeza majibu mazuri ya Serikali. Pia niseme tu kwamba ushauri wa kuendelea kutumia Chuo cha Munguri kilichopo sasa tumeupokea na tunaendelea kuutumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu, uwepo wa VETA utaongeza sana na kupanua wigo wa fursa za elimu ya ufundi ili kuendeleza azma yetu ya viwanda. Siyo hivyo tu, lakini pia kuongeza ajira kwa vijana. Swali; je, Serikali imejipangaje kuhakikisha kwamba maboresho haya mliyoyasema yanaingizwa kwenye Mpango na Bajeti ya VETA ili azma hii itekelezwe kwa haraka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, naelekea huko mzee, swali la pili, azma ya kuwa na VETA ina maslahi mapana sana kwa wanachi, siyo tu kwa wananchi wa Jimbo la Kondoa Mjini, lakini kwa Kondoa nzima kama Wilaya. Pia uwepo wa Taasisi ya kitaifa kama hii yenye hadhi ya VETA na sasa Kondoa ni Halmashauri ya Mji, itaongeza tija kubwa sana kwenye kuchangamsha uchumi wa Kondoa. Swali je, Serikali inatupa commitment gani ya kuhakikisha inaharakisha mchakato huu mara tu baada ya kupokea hiyo barua kutoka Kondoa?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kweli amekuwa akifuatilia kuhakikisha kwamba majengo yale yanatumiwa kwa ajili ya VETA. Naomba nimhakikishie kwamba kwa sababu Serikali ina azma na imedhamiria kujenga VETA kila Wilaya na kila mkoa, sisi tukikuta kwamba kuna majengo ambayo yamekuwa tayari tunakimbilia kwa sababu gharama ni ndogo kwa sababu tunataka tuweze kuwaletea wananchi maendeleo na kupata ile elimu ya ufundi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimhakikishie mbele yako kwamba pindi sisi tutakapopata barua ya kutuhurusu tutumie yale majengo tutaendelea na utaratibu wa kukarabati ili wananchi wa Kondoa waweze kupata ile huduma. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Wizara yetu hatuwezi tukawa kikwazo cha yeye kufanikiwa lengo lake hilo kwa ajili ya wananchi wake. Kwa hiyo naomba nimshauri wakakae na halmashauri yake watupatie barua, wakinipa kesho mimi niko tayari hata mwenyewe kwenda kukagua eneo lile ili tuweze kuendelea na taratibu zinazofuata.