Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Joseph Kasheku Musukuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:- Je, ni lini Mgodi wa GGM utawasilisha bajeti yake ya kuhudumia jamii katika Baraza la Madiwani la Geita ili tuweze kuangalia kipaumbele chao na kuwapa vipaumbele vya Halmashauri ya Geita?

Supplementary Question 1

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, nimpongeze Waziri kwa majibu mazuri, lakini naona majibu yake hayajitoshelezi.
Mheshimiwa Spika, kwa kifungu cha 105(3) kama alivyoainisha Mheshimiwa Naibu Waziri, ni kwamba mgodi utapokea maelekezo kutoka kwenye mabaraza mawili maana yake Geita Mjini na Vijijini, na mgodi utatulipa kama shilingi bilioni 9.1. Lakini kwa mchanganuo wa Halmashauri zetu, Halmashauri ya Geita Vijijini inapata asilimia 46, asilimia 54 zinabaki Geita Mjini. Sasa kwa maelezo na mchanganuo aliyoutoa Waziri CSR ya Halmashauri ya Geita inaingiaje kwenye Chato, Bukombe na Mbogwe? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; Geita Vijijini na Mjini tuna mgogoro na Mgodi wa GGM, tunawadai dola bilioni 12 wewe mwenyewe unafahamu na mlishauri watulipe kwanza dola laki nane mwezi wa kwanza, leo ni mwezi wa tano hatuoni majibu na hawatusikilizi, tumeshapeleka demand, sasa tunataka kupelekana mahakamani na Mgodi wa Geita unazidi kusafirisha dhahabu Jumanne na Ijumaa, na ili kibali cha kusafirisha dhahabu kitoke lazima walipe kodi za Serikali ninyi Wizara ndio mtoe kibali cha kusafirisha.
Mheshimiwa Spika, kwa nini Wizara isichukue action ya kutusaidia kuwanyima kibali ili waweze kutulipa hata kesho hizo dola laki nane? (Makofi)

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO): Mheshimiwa Spika, katika swali la kwanza, ni kwamba mgawanyo wa fedha katika Halmashauri ya Mji na Halmashauri ya Geita Vijijini, haya ni makubaliano ambayo wao wenyewe walifikia na Baraza la Madiwani na Mheshimiwa Mbunge naye ni Mjumbe, kwa hiyo, walifikia maamuzi haya na huu ndiyo msimamo wa Halmashauri na hivyo ndivyo mgawanyo utakavyokuwa.
Mheshimiwa Spika, kuhusu shilingi hizo bilioni alizozitaja ambazo ni sawasawa na dola laki nane ambazo walisema kwamba wanatakiwa wapewe na Mgodi wa GGM, ni kwamba mpaka sasa hivi GGM wako tayari kutoa hizo fedha. Mgogoro uliokuwepo ilikuwa ni Halmashauri ipi au akaunti ya Halmashauri ipi ipewe fedha hizo, na mpaka hapa ninapozungumza ni kwamba tayari Mkuu wa Mkoa kesho kutwa, siku ya tarehe 10 Mei, anakaa na hizi Halmashauri mbili, anakaa na hiyo GGM waelewane kwa pamoja ni Halmashauri ipi akaunti yake iweze kupewa fedha hizo na wao waweze kutafuta utaratibu wa kuweza kugawana fedha hizo.
Mheshimiwa Spika, la mwisho kwa kuongezea, suala la Halmashauri ya Mbogwe na halmashauri nyingine, Chato na maeneo mengine, napenda kumwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba waendelee kushiriki vile vikao vya Halmashauri ili waweze kuelewana vizuri kupitia Sekretarieti ya Mkoa waangalie ni namna gani ya kugawanya hizo fedha, sisi kama Wizara tutasimamia tu kuhakikisha GGM wameweza kutoa fedha za CSR. Ahsante sana. (Makofi)

Name

Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:- Je, ni lini Mgodi wa GGM utawasilisha bajeti yake ya kuhudumia jamii katika Baraza la Madiwani la Geita ili tuweze kuangalia kipaumbele chao na kuwapa vipaumbele vya Halmashauri ya Geita?

Supplementary Question 2

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa maelezo mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, Wilaya yetu ya Mbogwe kuna madini ya dhahabu na kumekuwa na mgogoro kati ya wananchi wa Nyakafuru pamoja na wawekezaji ambao wamekuja hapo. Sasa ninataka kujua msimamo wa Wizara uko vipi katika kuhakikisha kwamba leseni inatolewa kwa ajili ya wachimbaji wadogo wadogo wa Wilaya ya Mbogwe?

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO): Mheshimiwa Spika, wachimbaji wadogo wanaochimba Nyakafuru wanachimba chini ya leseni ya mtu mwingine, wanachimba bila kuwa na leseni, ni kama vile wachimbaji waliovamia leseni ya mtu mwingine. Sisi kama Wizara hatuchochei wachimbaji wadogo kwenda kuvamia leseni ya mtu mwingine, huo siyo utaratibu. Lakini sisi kama Wizara ya Madini tuna mpango na mkakati wa kutenga maeneo maalum kwa ajili ya wachimbaji wadogo.
Mheshimiwa Spika, tuna maeneo zaidi ya 44, tuna heka zaidi ya 238,000 kwa ajili ya wachimbaji wadogo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tunaomba ushirikiane na wananchi wako kwa kuwapa elimu ya kutosha kwamba tunakwenda kuwagawia maeneo ambayo ni halali, wachimbaji wadogo wachimbe kwa uhalali ili waweze kujipatia kipato chao, lakini wasiendelee kuvamia leseni za watu wengine. Ahsante.