Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Name
Dr. Pudenciana Wilfred Kikwembe
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Kavuu
Primary Question
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE aliuliza:- Serikali imekuwa ikiwahimiza wananchi wajiunge kwenye vikundi ili waweze kupata mikopo ya kuwasaidia kuendesha shughuli zao:- Je, Serikali haoni kuwa sharti hilo linawakosesha fursa baadhi ya wananchi ambao pengine wanahitaji huduma hiyo?
Supplementary Question 1
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kumuuliza Mheshimiwa Waziri pamoja na majibu mazuri ya Serikali, kwa kweli leo nimefurahi kidogo. Naomba nimshukuru Mheshimiwa Waziri amenijibu vizuri. Naomba nimuulize maswali mawili madogo ya nyongeza:
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, sera hii inalenga kutatua changamoto inayowapata wananchi kuhusu mitazamo mbalimbali lakini umesema pia sera hii inalenga kuwakopesha wanavikundi na mtu mmoja mmoja, swali langu ni kwamba; ni kwa nini sasa Halmashauri nyingi zimekuwa zikiwalazimisha wananchi wakope wakiwa kwenye vikundi vya watu watano na kuendelea, jambo ambalo kimsingi linamnyima mkopaji mmoja mmoja mwenye uwezo wa kukopa ambaye anaweza akajidhamini ili aweze kujiendeleza katika maisha yake?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, naishukuru Serikali yangu kwa sababu imeweza kuondoa riba katika hii mikopo ambayo imekuwa ikitolewa na Halmashauri asilimia kumi, lakini, ni kwa nini sasa, bado tunasema kwamba, kwa mfano kwenye Mifuko ya Akinamama na Vijana, wazee na wanaume hawapati mikopo hii, jambo ambalo tunaweza tukawakopesha na wakaweza kuendeleza mifuko hiyo?
Name
Josephat Sinkamba Kandege
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kalambo
Answer
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE):
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza kipengele cha kwanza alichouliza Mheshimiwa Pudenciana Kikwembe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, katika swali lake anapendekeza ingefaa tukaanza kum-address mtu mmoja mmoja badala ya vikundi ambalo kimsingi na yeye mwenyewe atakubaliana na mimi na hata ukienda kule kwake, vikundi kwa maana ya ushirika ndiyo hasa njia ya kuweza kututoa sisi wanyonge. Naomba nimsihi Mheshimiwa Mbunge kuwa vyovyote, yule ambaye ana uwezo wa kuweza ku-access mabenki, window hiyo ipo, lakini katika hii pesa ambayo inatolewa na Serikali ni vizuri kwanza tukajikita katika vikundi maana tukisaidia vikundi tunasaidia watu walio wengi zaidi.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA NA AJIRA: Mheshimiwa Spika, katika utaratibu wa uwezeshaji wananchi kiuchumi, Serikali inachokifanya ni kuona namna ya kuweza kuyagusa makundi yote kwa wakati mmoja. Ndiyo maana pamoja na kwamba tunayo Mifuko ya Uwezeshaji wa Wananchi Kiuchumi lakini pia tunayo mifuko maalum kwa ajili ya akinamama na vijana, lakini kundi la wazee na watu wengine ambao hawadondokei katika sifa hizo, wenyewe pia kupitia Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi wanayo fursa ya kwenda kukopeshwa mtu mmoja mmoja au kupitia vikundi pia.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimwuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ya kwamba bado hata kama kuna mzee na mtu mwingine yeyote ambaye anahitaji kupata mikopo hii, hata kama hadondokei katika kundi la vijana na akinamama lakini fursa hiyo ipo kupitia Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ambayo ipo 19 na imekuwa ikifanya kazi hiyo kuwawezesha wananchi kiuchumi.
Name
Kemirembe Rose Julius Lwota
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Special Seats
Primary Question
MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE aliuliza:- Serikali imekuwa ikiwahimiza wananchi wajiunge kwenye vikundi ili waweze kupata mikopo ya kuwasaidia kuendesha shughuli zao:- Je, Serikali haoni kuwa sharti hilo linawakosesha fursa baadhi ya wananchi ambao pengine wanahitaji huduma hiyo?
Supplementary Question 2
MHE. KEMILEMBE J. LWOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kumekuwa kuna hamasa ya uhamasishaji mkubwa sana kwa wananchi wetu kujiunga na vikundi hivi ili waweze kupata mikopo hii asilimia 10 kutoka kwenye Halmashauri zetu, lakini kiuhalisia Halmashauri nyingi mikopo hii haitoki. Nataka kujua, Serikali ina mpango gani wa kuwezesha Halmashauri zetu ili mikopo hii iweze kutoka na akinamama, wazee na watoto waweze kupata mikopo hii kama inavyoonekana? Mheshimiwa Spika, ahsante.
Name
Josephat Sinkamba Kandege
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Kalambo
Answer
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, swali hili limekuwa likijirudia mara kwa mara na majibu ambayo tumekuwa tukitoa, tumekuwa tukielekeza kwamba wakati tunakuja kuhitimisha bajeti kuna kipengele ambacho kitaingizwa katika Finance Bill ambacho kitamlazimisha kila Mkurugenzi kuhakikisha kwamba pesa hizi zinatengwa na zisipotengwa sheria zitachukuliwa ili kutoa adhabu kwa wale wote ambao hawatatimiza takwa hili la kisheria. Kwa sasa hivi, imekuwa ni kama option lakini tutakuja na kipengele ambacho kitamlazimisha kila Mkurugenzi a-make sure kwamba pesa hizi zinatengwa.
Copyright © Bunge Polis 2024. All Rights Reserved