Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Asha Abdullah Juma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ASHA ABDALLAH JUMA (K.n.y. MHE. KHADIJA NASSIR ALI) aliuliza:- Sera yetu ya Elimu inatueleza kuwa elimu ya msingi ni hadi kidato cha nne. Je, ni lini Serikali itaboresha kiwango hiki cha elimu ya msingi hadi kufika ngazi ya Ufundi Stadi yaani VETA?

Supplementary Question 1

MHE. ASHA ABDALLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, bado vijana wengi wanaomaliza darasa la saba wanakuwa hawajapata nafasi kwenye vyuo vya ufundi au kuendelea na masomo ya sekondari. Ni lini Serikali itaboresha elimu ya msingi kuhusisha mafunzo ya ufundi ndani yake ili kuwaasaidia wale wanaobaki?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mtaala wa VETA ni mmoja nchi nzima wakati mahitaji yanatofautiana sehemu na sehemu. Kwa mfano, mikoa yenye gesi wangefundishwa mambo yanayotokana na gesi, mikoa ya uvuvi wangefundishwa taaluma za uvuvi na mikoa ya madini vivyo hivyo. Sasa Serikali ina utaratibu gani kuhusu kuingiza component hiyo katika mitaala yake?

Name

Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Answer

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kuhusu suala la wanafunzi ambao wanamaliza darasa la saba lakini hawapati nafasi ya kuendelea na masomo ya sekondari, kama ambavyo nimesema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali inafanya kazi kubwa ya kuongeza nafasi za udahili kwenye vyuo vya ufundi kwa kujenga vyuo vipya vya ufundi pamoja na kuboresha Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niseme kwamba katika mtaala wa elimu ya msingi kuna somo la stadi za kazi ambalo limewekwa mahsusi kwa ajili ya kuwapatia vijana wetu angalau ujuzi ili hata yule anayemaliza elimu yake ya msingi awe tayari ana uwezo wa kufanya jambo katika mazingira yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusu mtaala wa VETA kwamba unafanana, kimsingi masuala ya ufundi yanatakiwa yaangalie mazingira halisi ya mahali ufundi unapofanyika. Kwa hiyo, suala la kuangalia masuala ya gesi au masuala ya uvuvi ndiyo jambo ambalo limekuwa likifanyika. Kwa hiyo, niendelee kutoa wito kwa wote wanaotoa mafunzo ya ufundi stadi wahakikishe kwamba mitaala yao inazingatia mazingira halisi ya pale ambapo wanatoa mafunzo ili kuwawezesha wananchi wa eneo husika kuongeza tija katika shughuli wanazozifanya.

Name

Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Primary Question

MHE. ASHA ABDALLAH JUMA (K.n.y. MHE. KHADIJA NASSIR ALI) aliuliza:- Sera yetu ya Elimu inatueleza kuwa elimu ya msingi ni hadi kidato cha nne. Je, ni lini Serikali itaboresha kiwango hiki cha elimu ya msingi hadi kufika ngazi ya Ufundi Stadi yaani VETA?

Supplementary Question 2

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa sasa wa kutumia VETA na vyuo vya FDC kutoa mafunzo ya ufundi stadi umekuwa ni wa polepole sana na idadi kubwa ya vijana wanamaliza shule za sekondari hawana ujuzi kabisa. Je, Serikali inaonaje sasa ikaanza kubadilisha baadhi ya shule za sekondari ambazo tumezijenga katika Halmashauri zetu kuwa shule za ufundi ili kusudi zisaidie vijana hawa kupata elimu ya ufundi?

Name

Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Answer

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwalongo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme kwamba Serikali tayari imeshaona hiyo changamoto na ndiyo maana zile shule za ufundi ambazo awali zilikuwa zimebadilishwa mafunzo ya ufundi yaliondolewa tayari Serikali imeshachukua jukumu la kuzikarabati zile shule saba za ufundi za Kitaifa na kuziimarishia vifaa vya kufundishia na karakana zake zote zimeimarishwa. Nitoe wito kama alivyosema Mheshimiwa Mwalongo, Serikali itafurahi sana kama kuna Halmashauri ambayo ina shule na wanaona kwamba inakidhi vile vigezo vya kutoa mafunzo ya ufundi tuko tayari watuambie ili twende kuikagua na tutapenda tu kuongezea idadi ya wanaofanya mafunzo ya ufundi.

Name

Fatma Hassan Toufiq

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ASHA ABDALLAH JUMA (K.n.y. MHE. KHADIJA NASSIR ALI) aliuliza:- Sera yetu ya Elimu inatueleza kuwa elimu ya msingi ni hadi kidato cha nne. Je, ni lini Serikali itaboresha kiwango hiki cha elimu ya msingi hadi kufika ngazi ya Ufundi Stadi yaani VETA?

Supplementary Question 3

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa baadhi ya shule za msingi zina vituo vya ufundi stadi, mfano, katika Wilaya ya Chamwino, vituo hivyo viko katika Shule ya Msingi Mvumi Mission na Shule ya Msingi Chamwino lakini hakuna vifaa wala walimu wa kutosha. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuvifufua vituo hivyo siyo kwa Wilaya ya Chamwino tu lakini katika shule zote za msingi ambazo ziko Tanzania hii? Ahsante.

Name

Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Answer

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLIJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la dada yangu Mheshimiwa Fatma Toufiq, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru kwa swali lake zuri kwa sababu ni kweli zile shule zipo lakini kwa kweli hali yake haijakaa vizuri, niliona nilipozitembelea. Kwa hiyo, tayari Serikali imeliona na kwa kupitia Mradi wa Kukuza Ujuzi hapa Nchini (ESPJ) ambao Wizara yangu inautekeleza kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, tutafanya tathmini ya shule hizo na kwa awamu tutaanza kuzifanyia maboresho kwa kuzipelekea vifaa.

Name

Salma Rashid Kikwete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mchinga

Primary Question

MHE. ASHA ABDALLAH JUMA (K.n.y. MHE. KHADIJA NASSIR ALI) aliuliza:- Sera yetu ya Elimu inatueleza kuwa elimu ya msingi ni hadi kidato cha nne. Je, ni lini Serikali itaboresha kiwango hiki cha elimu ya msingi hadi kufika ngazi ya Ufundi Stadi yaani VETA?

Supplementary Question 4

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Tunaamini na tunajua kwamba elimu ndiyo msingi wa kila kitu katika maisha ya mwanadamu na mafanikio ya elimu ni pamoja na kuwa na zana za kufundishia pamoja na kujifunzia. Kwa kuwa, vitabu vyetu vya kiada huchapishwa nje ya nchi yetu na tukiamini kwamba elimu ni jambo tete katika ustawi wa Taifa letu, je, ni lini vitabu hivi vya kiada vitachapishwa hapa nchini ukizingatia Serikali yetu ni ya viwanda? (Makofi)

Name

Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Answer

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mama Salma Kikwete, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimshukuru sana kwa kuleta swali hili hapa Bungeni na nitumie nafasi hii kuonyesha masikitiko yangu makubwa sana kwa makampuni ya Kitanzania ambayo yanafanya kazi ya uchapishaji. Haya Makampuni yametuangusha kweli kweli, tumelazimika kwenda kuchapa vitabu nje kwa sababu unapoyapa makampuni ya Kitanzania kwanza kuna mengine ambayo yamekuwa yanachapa vitabu, kitabu kimekaa kama sambusa yaani wanakata hovyo hovyo lakini pia wanatumia muda mrefu kuvichapa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuhusu swali lake kwamba Serikali ina mpango gani, kutokana na changamoto hiyo, Serikali imeamua kununua mashine ya uchapaji na hapa tunapoongea tayari tumekwishaiagiza. Kwa hiyo, tunategemea hilo suala sasa tutakuwa tunalifanya wenyewe.