Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Victor Kilasile Mwambalaswa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupa

Primary Question

MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA (K.n.y MHE. FREDY A. MWAKIBETE) aliuliza:- Tanzania imebarikiwa kuwa na madini mbalimbali na Jimbo la Busokelo pia limebarikiwa kuwa na madini hayo. Je, ni lini Serikali itapeleka wawekezaji wa kiwanda cha marumaru katika Kata ya Lufilyo kwenye Mto Makalya?

Supplementary Question 1

MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri sana. Kwanza kabisa wananchi wa Busokelo Kata ya Lufilyo wanakupongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri na kukushukuru sana kwa utendaji wako. Ulienda Kata ya Lufilyo ukiwa Naibu Waziri wa Elimu, ulisaidia sana katika uanzishwaji wa ujenzi wa Kituo cha VETA pale kwenye kata hiyo. Wanakushukuru sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani hizo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza; la kwanza; madini ya granite ni mazito sana na ndiyo maana katika kuyabeba kutoka Lufilyo kwenda mpaka Mbeya inaharibu miundombinu hasa hasa ya barabara sababu ya uzito.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawezesha wawekezaji waweze kuweka mtambo wa kutengeneza madini hayo hapo hapo sehemu ya Lufilyo ili tusiharibu miundombinu? La kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, uwekezaji katika Kata ya Lufilyo na Jimbo la Busokelo unafanana kabisa na uwekezaji katika Wilaya ya Chunya. Mheshimiwa Waziri Mkuu alifanya ziara Chunya mwanzoni mwa mwaka huu na alishuhudia uchenjuaji wa tailings (makinikia) kwa wazawa na wageni na alifurahishwa sana na uchenjuaji huo uko Chunya. Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema kwamba sasa hivi Serikali iko kwenye mchakato wa kuweza kuweka mtambo wa kuchenjua makinikia hapa nchini na akapendekeza kwamba Chunya inaweza kuwa sehemu mojawapo ya kuweka mtambo huu wa kuchenjua makinikia (smelter). Je, mchakato huo wa kuweka smelters nchini hasa Chunya umefikia wapi? (Makofi)

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.
Kwanza kabisa nimjibu Mheshimiwa Mbunge kwamba kweli granite zina uzito mkubwa, lakini katika hatua za ku- process ni mwekezaji mwenyewe ndiye ana jukumu la kuangalia ni sehemu gani anaweza akaweka mtambo wa ku-process ili uweze kumtengenezea faida. Kwa hiyo, anatakiwa afanye cost benefit analysis kusafirisha na ku- process katika eneo husika na sisi kama Wizara ya Madini tunapendekeza mtu a-process madini katika eneo la uchimbaji ili atengeneze ajira katika eneo lile, hiyo moja.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili katika uchenjuaji wa tailings kwa manufaa ya Wabunge wote kufahamu kwanza tailings na makinikia ni vitu viwili tofauti. Tailings ni mabaki ya dhahabu katika udongo ambao umechenjuliwa katika hatua za awali yaani unapochenjua kwa kutumia mercury zinabaki tailings kwa ajili ya ku-process katika CAP yaani katika process ya aina nyingine. Sasa kutengeneza mtambo wa makinikia ni kweli kabisa Wizara ya Madini inashirikiana na makampuni makubwa kutoka nje kuweza kuwekeza katika mitambo mikubwa ya kuweza kufanya smelting. Mpaka sasa hivi tuna kampuni 27 ambazo zimekuja kuonesha nia za kuwekeza, kuanzisha smelters pamoja na refineries na mpaka sasa hivi tayari tuna kampuni 10 zime-qualify, kwa hiyo, Serikali kwa kushirikiana na hizo kampuni za nje muda si mrefu tutaanzisha zile smelters hapa nchini. Ahsante.