Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SUSAN A. J. LYIMO aliuliza:- Vitabu ni nyenzo muhimu sana ya kujifunzia lakini kwa muda mrefu sasa wanafunzi hawana vitabu vya kiada:- Je, Serikali inawaambia nini Walimu na Wanafunzi wa Shule za Msingi?

Supplementary Question 1

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Ukiangalia kwenye majibu ya msingi ya swali langu Waziri anakiri kabisa kwamba bado mpaka sasa hivi wanasambaza vitabu vya darasa la nne na kimsingi darasa la nne wamefanya mtihani. Kwa hiyo ina maana kuna wanafunzi wamekosa vitabu na wamefanya mitihani na hawa watoto pia wanafanya mitihani ya kufanana. Je, Serikali haioni hili ni tatizo kubwa na kwamba ni lazima sasa watoto wapate vitabu kwa wakati kwa sababu tunajua Walimu nao wana matatizo yao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; mwaka 2016 Taasisi ya Elimu ilitayarisha vitabu na vitabu hivyo vikaondolewa kwa sababu vilikuwa vibovu sana, lakini mwaka 2018 wametengeneza tena vitabu na baadhi ya vitabu vina matatizo. Je, Serikali haioni kwamba Taasisi ya Elimu imeshindwa kazi yake kwa sababu vile vitabu vilikuwa zaidi ya bilioni 100 tulivyoambiwa na kwamba sasa Serikali haioni kuna haja ya kuwa na ushindani na Sekta Binafsi ili vipatikane vitabu ambavyo vitakuwa bora ili watoto wetu waweze kupata elimu bora? (Makofi)

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kumekuwepo na changamoto ya kuhakikisha kwamba vijana wetu wa darasa la nne wanapata vitabu kwa wakati. Hata hivyo, kama nilivyoeleza sasa tunaelekea kukamilisha zoezi la kusambaza vitabu hivyo nchi nzima. Kwa hiyo nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba changamoto hiyo sasa tuko mbioni kuachana nayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu hili la vitabu anavyosema vina makosa tulishatoa rai kwamba kama kuna yeyote mwenye kitabu kati ya vitabu hivi ambavyo tumechapisha ambaye ameona au anahisi vina makosa atuletee kwa sababu sisi ka Wizara na kama Serikali. Mchakato ambao tumeutumia kuja na vitabu vipya umetuhakikishia kwamba kuna ubora mkubwa sana katika vitabu vipya ambavyo vimetoka kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Mbunge na wengine wote ambao wao wana vitabu ambavyo wanafikiri vina makosa wavilete kwetu na tutaviangalia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu tayari kulikuwa na vikaragosi vinazungushwa mtaani kumbe vilikuwa ni vikaragosi vya vitabu vya Kenya. Kuna watu wengi ambao wanajaribu kuichafua Serikali na kuchafua mfumo wetu wa elimu. Kwa hiyo, naombeni mwenye chochote kile ambacho anafikiri ni makosa alete tuangalie kwa sababu sisi tunajiridhisha kuwa vitabu havina makosa.