Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Joseph Kasheku Musukuma

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:- (a) Je, ni utafiti gani umefanyika katika Ziwa Victoria mpaka kufikia hatua ya kuzuia uvuvi wa aina yoyote kwa kisingizio cha uvuvi haramu? (b) Je, ni sheria gani inatumika kukamata nyavu na ndani ya dakika kumi zinachanwa bila ya kumpa mvuvi nafasi ya kujitetea?

Supplementary Question 1

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Dhana ya uvuvi haramu imeenea sana kwenye kauli za Mawaziri, lakini kule ziwani kuna aina za samaki kama 30 na samaki pia wana makuzi tofauti, ni kama binadamu. Ukichukua umri wa Musukuma ukachukua na umri wa Mwalongo, tuko sawa, lakini ukituangalia kwa maumbile tulivyo tuko tofauti na unapotupa nyavu ziwani inakuja na samaki za aina tofauti wakiwepo wenye tabia kama yangu na Mwalongo.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ukiwapima kwenye rula hawalingani lakini umri ni mmoja. Kwa kuwa sheria yenyewe ndiyo inajichanganya, ni lini Wizara itakuja na sheria ambayo itam-favour pia mvuvi anapokumbana na matatizo kama ya maumbile ya binadamu? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mheshimiwa Waziri wakati operesheni hii inapoendelea, kumekuwa na tabia ya kukamata nyavu saa nne na zinachomwa saa sita. Mfano mzuri ni kwenye Kisiwa cha Izumacheri kilichopo Jimbo la Geita Vijijini ambapo Maafisa Uvuvi walikamata nyavu ambazo siyo haramu lakini wakanyimwa rushwa, wakachoma nyavu dakika 15 zilizofuata na nyavu hizi ni halali. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kufuatana na mimi kwenda kusikiliza SACCOS hiyo na kutoa adhabu kwa wale waliohusika na suala hili? (Makofi)

Name

Abdallah Hamis Ulega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkuranga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la lini Serikali itakuja na sheria mpya itakayowasaidia wavuvi waweze kufanya shughuli zao kwa uzuri zaidi, hasa ikizingatiwa hili analolisema la kwamba samaki wako wa aina tofauti na ile nyavu inapoingia inakwenda kuzoa hata wengine wasiohusika.
Mheshimiwa Spika, Serikali tupo katika hatua ya mwisho ya maboresho ya Sheria yetu ya Uvuvi na itakapokuwa tayari itaingia humu Bungeni ambapo Waheshimiwa Wabunge watashiriki kikamilifu katika kuhakikisha kwamba sheria ile tunaiboresha kwa pamoja kwa maslahi mapana ya Taifa letu.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili ameeleza juu ya suala linalohusu nyavu, ya kwamba nyavu hizi zinapokamatwa ghafla tu zinachomwa moto na akanitaka kama niko tayari niweze kufuatana naye kwa ajili ya kuweza kwenda kuwachukulia hatua wale watumishi wa Serikali ambao wanatenda kinyume.
Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Musukuma na Waheshimiwa Wabunge wote na hata wananchi wote wanaoshughulika katika shughuli hizi za uvuvi, Wizara yangu tuko tayari kabisa sisi kama viongozi kwa specific cases kama hii anayoizungumzia Mheshimiwa Musukuma, tutakwenda popote pale na endapo tutabaini watumishi wetu wametenda kinyume sisi kama Mawaziri tuko tayari kuwachukulia hatua kwa ajili ya mustakabali mpana zaidi wa wananchi na wavuvi wetu. (Makofi)

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:- (a) Je, ni utafiti gani umefanyika katika Ziwa Victoria mpaka kufikia hatua ya kuzuia uvuvi wa aina yoyote kwa kisingizio cha uvuvi haramu? (b) Je, ni sheria gani inatumika kukamata nyavu na ndani ya dakika kumi zinachanwa bila ya kumpa mvuvi nafasi ya kujitetea?

Supplementary Question 2

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi. Naomba nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Kwa mujibu wa Kanuni za Uvuvi, ukienda kifungu cha 45(3)(b), naomba nisome, kinasema:-
“No person shall: (b) fish, land or possess, process or trade in Nile tilapia or fish locally known as “Sato” the total length of which is below 25 centimetres.”
Mheshimiwa Spika, ukisoma Kanuni hii, ni kama inafikiria source ya Sato ni moja tu, Nile Tilapia lakini sasa Tanzania tuna-encourage watu kufanya aquaculture, maana yake sources za sato ziko nyingi, lakini tuna maziwa na mito na Kanuni hii imetumika kusababisha usumbufu mkubwa sana kwa watumiaji wa sato nchi nzima. Ni lini Serikali au ni kwa nini Serikali isisitishe sasa kukamata watu kwa kutumia Kanuni hii ambayo yenyewe tu inajichanganya na ina makosa mpaka itakapofanyiwa marekebisho? (Makofi)

Name

Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Answer

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nishukuru sana kwa swali hili la nyongeza la Mheshimiwa Kanyasu, lakini nimpongeze sana Naibu wangu kwa majibu mazuri sana aliyoyatoa hapo awali.
Mheshimiwa Spika, kama alivyoisoma Kanuni yetu na kama Naibu Waziri alivyoeleza, mwezi huu wa Saba, Wizara yangu itakuwa imemaliza zoezi la kufanya mapitio ya Kanuni ya Uvuvi pamoja na Sheria yenyewe ya Uvuvi Na. 22 ya mwaka 2003. Vilevile kwa nyongeza ni kwamba operesheni hizi zinazoendelea na wananchi wetu ambao wanajishirikisha na ufugaji wa samaki, kila wanapofikia kuvuna samaki wao wanawasiliana na ofisi yangu ambayo inakuwa inazo taarifa za uhakika juu ya uvunaji wa samaki hao ili kusije kukatokea usumbufu wa aina yoyote.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika kipindi ambacho Kanuni inarekebishwa, utaratibu umewekwa na Wizara kwa maana ya kwamba mawasiliano yako proper ya namna ya uvunaji kwa sasa wakati tunatengeneza Kanuni ambayo itakuwa ime-favour uvunaji wa samaki katika Ziwa Viktoria lakini wakati huohuo na wale wafugaji wetu wa samaki ambao wanafuga samaki kwenye maji.

Name

Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:- (a) Je, ni utafiti gani umefanyika katika Ziwa Victoria mpaka kufikia hatua ya kuzuia uvuvi wa aina yoyote kwa kisingizio cha uvuvi haramu? (b) Je, ni sheria gani inatumika kukamata nyavu na ndani ya dakika kumi zinachanwa bila ya kumpa mvuvi nafasi ya kujitetea?

Supplementary Question 3

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwa kuwa baada ya operesheni nyavu zinazotumika sasa ni mbovu sana, hazina kiwango na wala hazistahili kutumika kwa uvuvi, zinawatia hasara sana watumiaji. Je, Serikali ina mpango gani wa haraka kupata nyavu zinazostahili, zinazoweza kukabiliana na mazingira ya Maziwa Viktoria, Tanganyika na mengineyo ili wavuvi wetu mbali na kupata hasara za kuchomewa nyavu wasiendelee kupata hasara za kununua nyavu kila siku chache zinapokuwa zinapita? (Makofi)

Name

Abdallah Hamis Ulega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkuranga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, juu ya suala linalohusu ubora wa nyavu, ni kweli Wizara yangu imepokea malalamiko kutoka kwa wavuvi kutoka pande zote za nchi yetu hasa wavuvi wa Ziwa Viktoria na tumekwenda kujiridhisha. Tupo katika utaratibu wa kuendelea kufanya tathmini ya hali hii. Nataka nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba tunashirikiana vyema na wenzetu wa Wizara ya Viwanda na Biashara kwa ajili ya kuweza kupata viwango halisi vya ubora wa nyavu zetu zinazozalishwa nchini.
Mheshimiwa Spika, pale itakapobainika kwamba liko tatizo juu ya ubora huu, la kwanza tutawataka ama tunawataka wazalishaji wetu waongeze viwango vyao vya ubora, lakini ikibidi sisi kama Wizara tuko tayari kutafuta mpango mwingine wa kuweza kuwanusuru wananchi wetu ili waweze kuendelea na shughuli hii ya uvuvi bila ya tatizo lolote.

Name

Dr. Raphael Masunga Chegeni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza:- (a) Je, ni utafiti gani umefanyika katika Ziwa Victoria mpaka kufikia hatua ya kuzuia uvuvi wa aina yoyote kwa kisingizio cha uvuvi haramu? (b) Je, ni sheria gani inatumika kukamata nyavu na ndani ya dakika kumi zinachanwa bila ya kumpa mvuvi nafasi ya kujitetea?

Supplementary Question 4

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Zoezi la uvuvi haramu limetekelezwa sivyo ndivyo katika maeneo mengi sana na wavuvi wengi sana wamepata hasara kubwa sana kutokana na zoezi hili. Zoezi hili limefanywa na wafanyakazi ambao kwa kweli hawakuzingatia maadili na hata kanuni za kazi zao. Ilifikia mahali Mheshimiwa Waziri akasema kwamba yeye hana wapiga kura wavuvi hao wenye wapiga kura wavuvi mtajijua wenyewe. Nataka kujua kauli ya Serikali, wavuvi ambao wameingizwa hasara kubwa sana watalipwa fidia kiasi gani na lini fidia hiyo italipwa?

Name

Luhaga Joelson Mpina

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisesa

Answer

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, suala la uvuvi haramu tumeeleza mara kwa mara hapa Bungeni na jinsi ambavyo linaendeshwa. Waheshimiwa Wabunge tumewaomba mara kwa mara kwamba kama kuna mtu ambaye ameonewa katika eneo lolote lile tuletewe ili sisi tuweze kuchukua hatua. Leo ni miezi sita Wizara yangu inasisitiza suala la watu walioonewa kuwasilisha malalamiko yao ili waliohusika waweze kuchukuliwa hatua.
Mheshimiwa Spika, zaidi ya hapo Wizara yangu haiwezi kujua ni kitongoji, kijiji na kata gani, ni lini, Mkaguzi nani na alifanya makosa yapi kwa sababu hatua za ukamataji zipo. Sasa ikiendelea kuzungumzwa hivi kila siku kwamba watu wameonewa, halafu ushahidi hupewi, Waziri huwezi kuwa kwenye nafasi ya kuchukua hatua.
Mheshimiwa Spika, hili Bunge ndiyo linalotunga sheria, kwa nini Waziri alaumiwe na kuandamwa kwa kuchukua hatua za watu ambao wamevunja sheria? Nataka niseme kwamba wananchi na watu wote wataendelea kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria tulizonazo leo na kwa mujibu wa Katiba tuliyonayo sasa, watakaguliwa mahali popote na wakibainika watachukuliwa hatua. Watu wote wanaojihusisha na uvuvi haramu bila kujali vyeo vyao, wataendelea kuchukuliwa hatua mahali popote walipo kwa mujibu wa sheria tulizonazo.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inasisitiza kama kuna mtu yeyote ambaye ana ushahidi dhidi ya manyanyaso au uonevu wa aina yoyote umefanywa na Afisa wangu siku hiyo hiyo hatua zitachukuliwa.