Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Eng. Atashasta Justus Nditiye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muhambwe

Primary Question

MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE aliuliza:- Je, Serikali ina mkakati gani wa makusudi wa kuwadhibiti wakimbizi hasa maaskari ambao hutoroka kambini Nduta na kwenda kujumuika na wananchi, hivyo kuhatarisha usalama wa wananchi?

Supplementary Question 1

MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, itakumbukwa kwamba miaka ya 1990 tulipokea wakimbizi kutoka Burundi na wakawekwa kwenye kambi ya wakimbizi ya Nduta. Baada ya hali ya amani kurejea, ile kambi ilifungwa, Serikali ikawapatia wananchi kuanzisha kijiji cha mfano cha Nduta.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wakimbizi hali ya amani iliyokuwa siyo nzuri tena Burundi, wakimbizi tena walirejea na Serikali ikawaomba wale wananchi waondoke kwa ahadi kwamba itawalipa fidia. Sasa ni lini wananchi hao watalipwa fidia yao? Swali la kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ujio wa wakimbizi mara nyingi pamoja na mambo mengine huwa ina athari za kimazingira na kimiundombinu hasa barabara na maji. Kuna ombi ambalo Kiwilaya tulitoa na Serikali ya Mkoa ikatuunga mkono kuhusu miundombinu ya maji kwa kuwa ujio wao umesababisha kuongezeka kwa watu wanaotumia miundombinu ile ile ya maji na barabara…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa naomba uulize swali tafadhali.
MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITIYE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mheshimiwa Naibu Waziri anajua, juzi juzi alikuwa Kibondo na akajua kwamba tumepeleka ombo UNHCR kwa ajili ya kupata maji.
Je, Serikali imefanya msukumo gani hadi sasa hivi ili tuweze kupatiwa maji?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nilifanya ziara hivi karibuni huko kwenye kambi za wakimbizi na katika ziara hiyo pia tulikutana na maandamano ya wananchi ambao walikuwa wana madai ambayo Mheshimiwa Mbunge ameeleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hatua ambayo tumechukua ni kuweza kuzungumza na UNHCR ili waangalie uwezekano wa kuwalipa; siyo fidia lakini ni kama kifuta machozi. Kwa sababu kwa mujibu wa taratibu, wale wananchi waliruhusiwa kulima pale, lakini eneo lile ni miliki ya Serikali na limetengwa maalum kwa ajili ya kuhifadhi wakimbizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Engineer Nditiye kwamba mazungumzo ambayo tumefanya na UNHCR yameonekana kuzaa matunda na tunatarajia kwamba wananchi hawa wanaweza wakapatiwa kifuta jasho.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala lake la huduma za jamii, moja katika mikakati mikubwa ya Serikali ambayo hata Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofanya Ziara katika maeneo hayo, alitoa msisitizo muhimu wa maeneo ambayo wananchi wanaoishi maeneo yanayozunguka kambi za wakimbizi kuweza kufaidika na huduma mbalimbali za kijamii.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la Nduta, kwa mfano sasa hivi UNHCR wamekubali kutoa nusu ya mahitaji ya madawati yanayohitajika katika maeneo hayo, lakini pia tumefanya nao mazungumzo kuhakikisha kwamba katika maeneo ya huduma za maji na afya wanaweza kutoa michango yao ili wananchi waweze kufaidika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nadhani kabisa kwamba baada ya mazungumzo hayo tunaweza kuona mafanikio kuhusiana na miradi ya maji katika maeneo hayo.