Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza:- Tatizo la ada kwa wanafunzi katika shule binafsi nchini linazidi kuongezeka siku hadi siku. Mwanafunzi wa darasa la kawaida katika baadhi ya shule analipa mpaka shilingi milioni tatu hali inayosababisha wazazi wengine kuwapeleka watoto wao katika nchi jirani za Kenya na Uganda ili kutafuta nafuu ya ada:- Je, kwa nini Serikali isikae na wadau husika ili kupanga ada elekezi kwa wenye shule binafsi?

Supplementary Question 1

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kutoa elimu bure, lakini kwa kuwa Serikali imesema wazi na inaonesha wazi kwamba mjadala na watu wenye shule binafsi kwa ajili ya kupunguza hizi ada bado haujafanyika; na kwa kuwa baadhi ya shule za msingi za binafsi zimekuwa na mtindo wa kuwalundikia watoto wadogo maswali kutoka 100 mpaka 1,200 kuja kufanya nyumbani, hali ambayo inawafanya watoto wengine waogope kwenda shule kwa kuwa hajamaliza homework na watoto wengine kufanyiwa kazi hizo na wadada wasaidizi wa nyumbani. Je, Serikali inatoa tamko gani kwa walimu ambao hawatumii njia za ufundishaji zinazofuata misingi ya kazi ya ualimu na matokeo yake watoto wanafundishwa na watu wasiokuwa na taaluma ya ualimu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa wazazi wengi wamepeleka watoto katika shule binafsi kwa malengo mbalimbali. Lengo kubwa lingine lilikuwa ni kuwaanda watoto wao kuweza kufanya vizuri katika masomo ya sekondari na chuo kikuu, lakini wazazi wa Mkoa wa Dar es Salaam wamepata sintofahamu juu ya hatma ya watoto wao kukosa mikopo ya kusomea vyuo vikuu wakati maisha yana kupanda na kushuka. Je, Serikali inawaambia nini wazazi wanaosomesha watoto wao katika shule binafsi?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA WIZARA YA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mariam Kisangi ambaye ni mwalimu mbobezi, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali lake la kwanza kuhusu kutoridhika kwake na namna baadhi ya walimu wa shule za binafsi wanavyoendesha mambo yao, naomba tu nisisitize pamoja na kwamba shule ni za binafsi, mitaala, sheria, kanuni na miongozo ni ya umma. Kwa hiyo, hata kama tukitoa ruhusa wamiliki wa shule binafsi waweze kuendesha shule lakini ni lazima wafuate taratibu, sheria na sera iliyopo. Kwa hiyo, tunategemea kwamba kwa kutumia mfumo mpya ambao tumeuleta wa udhibiti ubora ambao kimsingi kila mtu sasa ni mdhibiti ubora kuanzia Kamati au Bodi za Shule vilevile shule zenyewe, tunategemea kwamba upungufu wowote ambao utatokea, utashughulikiwa na wadhibiti ubora ili kanuni zilizopo ziweze kufuatwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile lengo la Serikali la kuingia kwenye mchakato wa kuja na Bodi ya Kitaaluma ya Walimu ni kuhakikisha kwamba walimu wanaofundisha kwenye shule zote ikiwa ni pamoja na shule binafsi ni wale tu ambao watakuwa wana viwango vinavyohitajika lakini ni walimu ambao watakuwa wameandikishwa. Kwa hiyo, tunategemea katika mwaka huu tutakuja na Muswada ili kuhakikisha kwamba mwalimu yeyote ambaye atafundisha ni yule tu ambaye amethibitika kwamba amehitimu na ana ubora unaohitajika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali la pili kuhusu wasiwasi wa wazazi wa wanafunzi ambao wamesoma katika shule za binafsi kupata mikopo ya kwenda katika elimu ya juu, naomba niendelee kuweka wazi jambo ambalo tumekuwa tukizungumza. Bajeti ya mikopo kwa ajili ya wanafunzi wanaoenda vyuo vya elimu ya juu kwa mwaka ni shilingi bilioni 427 wakati wanafunzi ambao tunategemea kuomba mikopo kwa mwaka ni kama 70,000. Mwaka huu wa fedha unaoisha tuliweza kuchukua wanafunzi 30,000 na kwa mwaka unaokuja tunategemea kuongeza idadi hiyo kufikia wanafunzi 40,000. Katika hali ambayo fedha iliyopo inaweza kuwachukua wanafunzi kiasi fulani, ni lazima tufanye uchaguzi. Uchaguzi wetu utaangalia uwezo wa wazazi kulipa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mwanafunzi aliyesoma katika shule binafsi inachukuliwa moja kwa moja kwamba ana uwezo wa kulipa chuo kikuu. Mfano mzuri tu ni kwamba shule nyingi za binafsi nyingine ada zinafika hata shilingi milioni 30 na nyingine unakuta ada ya chini kabisa ni Sh.1,500,000 lakini University of Dar es Salaam kwenye baadhi ya masomo ni mpaka Sh.1,000,000 na Chuo Kikuu Mzumbe ni Sh.1,300,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunachoomba ni kwamba wale watoto ambao hawana uwezo kabisa tuwape nafasi kwanza kabla hatujawachukua wale ambao historia yao inaonesha kwamba wana uwezo wa kulipa. Hata hivyo, kama itadhihirika kwamba kuna mwanafunzi ambaye alipata msaada wa kulipiwa shule za binafsi katika ngazi ya primary na secondary, tutahitaji tu ushahidi, vinginevyo naye atapata ufadhili.