Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Yahaya Omary Massare

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Magharibi

Primary Question

MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza:- Je, ni lini Vijiji vya Jeje, Kashangu, Idodyandole, Mbugani, Aghondi, Mabondeni, Kitopeni, Ipande, Muhanga, Damwelu, Kitaraba, Kazikazi, Kintanula na Rungwa vitapatiwa umeme katika Mradi wa REA?

Supplementary Question 1

MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri yenye kutia moyo wananchi wa Jimbo la Manyoni Magharibi, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Kalangali kimepitiwa na umeme ukaenda kutua kijiji cha pili cha Mkoa wa Tabora, Kijiji cha Kipili. Wananchi wa Kalangali wanasononeka sana na kupitwa na umeme huu. Je, sasa Wizara hii iko tayari kuingiza kijiji hiki katika mzunguko huu wa kwanza, Awamu ya Tatu ya REA?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii alipokuwa Naibu Waziri alikuja Itigi na alifanya mkutano mzuri sana na wananchi. Sasa yuko tayari kwenda kufanya mkutano na wananchi wa Rungwa kuwahakikishia kwamba Awamu ya Tatu mzunguko wa pili umeme utaenda hadi Rungwa?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza lilihusu Kijiji cha Kalangali ambapo kwa maelezo yake kijiji hiki kimepitiwa na miundombinu ya umeme ambayo imeelekea Mkoa wa Tabora na wananchi wa kijiji hiki hawajapa umeme huo.
Napenda nikubali maelezo ya Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa kuna maelekezo ya Serikali maeneo yote yaliyopitiwa na miundombinu ya umeme mkubwa na ambayo hayajapata umeme yapatiwe. Kwa kuwa kazi katika kijiji hiki ni kushusha transfoma na kuwaunganisha wateja, napenda nimthibitishie nitatoa maelekezo kwa mkandarasi na REAwafanyie kazi kijiji hiki na kipatiwe umeme katika awamu hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ombi la Mheshimiwa Waziri kufanya ziara katika Wilaya ya Itigi, Kijiji cha Rungwa, naomba nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ombi hilo limekubaliwa na ziara itafanyika kama ilivyo utaratibu wetu kutembelea maeneo mbalimbali. Ahsante.