Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Frank George Mwakajoka

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Tunduma

Primary Question

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:- Je, ni kwa nini Serikali haiwapatii wananchi wa Mji wa Tunduma ruzuku ya asilimia 0.3 kama ilivyo kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yenye kuchimbwa madini?

Supplementary Question 1

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa kigezo cha kutoa asilimia 0.3 kwenye Halmashauri ambazo kuna kazi za uchimbaji unaofanywa na migodi inatokana na athari ambazo wananchi wa maeneo hayo wanapata. Katika Mji wa Tunduma kuna forodha ambayo inahudumia nchi karibu nane Kusini na Kati mwa Afrika na kumekuwa na madhara mengi sana kwenye mpaka wa Tunduma ambayo yanafanana kabisa na maeneo wanayochimba migodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, kuna magonjwa ya UKIMWI lakini kuna miongamano mkubwa sana wa magari na kusababisha usumbufu mkubwa kwa wananchi wangu ambao wanashindwa kutekeleza majukumu yao ya kimaendeleo vizuri.
Je, Serikali haioni kwamba sasa ni muda muafaka kuona na sisi kama Halmashauri ya Tunduma tunaweza kupata asilimia 0.3 ya ruzuku kama ambavyo wanapata katika maeneo ambayo wanachimba migodi? Ahsante.

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri na nipende kujibu swali la Mheshimiwa Mwakajoka, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa kama ambavyo kifungu cha 6(1)(u) cha Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa kinavyoeleza, fedha hii ya ushuru wa huduma si kwa ajili ya madhara ni kwa ajili ya wao kupata stahiki ya huduma mbalimbali na mapato yaliyotokana na shughuli za uchimbaji. Kama ambavyo tumeeleza, kwa upande wa Tunduma bado hakuna leseni ya uchimbaji madini ambayo ilitolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa ufuatiliaji tumekuwa makini kufuatilia kutaka kujua kwa nini Mheshimiwa Mbunge amekuwa akitaka kuulizia suala hili. Tumefuatilia katika eneo la Mkombozi na Chapwa ambapo katika eneo la Chapwa kulikuwa na shughuli za uchimbaji wa madini ya ujenzi ya kifusi, lakini yalikuwa yakichimbwa kwa ajili ya upanuzi wa barabara. Kwa sasa tunachokifanya tumeanza kurasimisha ili leseni ziweze kutolewa kwa wale ambao waliokuwa wakichimba kwa kificho basi waweze kuingia katika shughuli hizo za uchimbaji kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu na waweze kugaiwa leseni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge asubiri tu, leseni zitakaporasimishwa kwa wachimbaji wale katika eneo la Chapwa pamoja eneo la Mkombozi basi wataweza kupata ushuru huu wa huduma au service levy.

Name

Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Primary Question

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:- Je, ni kwa nini Serikali haiwapatii wananchi wa Mji wa Tunduma ruzuku ya asilimia 0.3 kama ilivyo kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yenye kuchimbwa madini?

Supplementary Question 2

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye maeneo ambapo shughuli nyingi za uvuvi zinafanyika kunapatikana athari za kijamii za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja. Kama ilivyo kwenye maeneo zinapofanyika shughuli za uchimbaji wa madini ambapo maeneo yanayozunguka migodi hii yanapata mrahaba kama sehemu fulani ya ku-recover athari hizi.
Je, Serikali haioni sababu sasa sheria hii iweze kutumika kwenye maeneo ambako shughuli za uvuvi zinafanyika na kusababisha athari mbalimbali za kijamii kwa ajili ya ku-recover sehemu ya athari hizi? Nashukuru.

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge ameulizia suala la kupata service levy kutokana na uvuvi katika Ziwa Victoria. Naomba niseme tu suala la uvuvi haliko katika Sheria ya Madini ambayo tunaisimamia sisi. Nadhani ni vema Mheshimiwa Mbunge akaifuatilia Sheria ya Serikali za Mitaa kuona kama kuna stahiki ambayo unaweza ukaipata kutokana na masuala ya uvuvi. Ahsante.

Name

Kasuku Samson Bilago

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Buyungu

Primary Question

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:- Je, ni kwa nini Serikali haiwapatii wananchi wa Mji wa Tunduma ruzuku ya asilimia 0.3 kama ilivyo kwa wananchi wanaoishi katika maeneo yenye kuchimbwa madini?

Supplementary Question 3

MHE. KASUKU S. BILAGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilileta swali hapa Bungeni ili kujua maeneo yenye madini katika Wilaya ya Kakonko. Maeneo yaliyoanishwa na Serikali katika majibu yake ni pamoja na chokaa iliyoko eneo la Nkogongwa, dhahabu iliyoko Ruhuru Nyakayenzi na Nyamwilonge. Baada ya kuwa maeneo hayo yametambulika wananchi walichangamkia wakataka kuchimba madini lakini ghafla Serikali ikasitisha leseni za uchimbaji.
Ninachotaka kujua ni lini Serikali itafungua utoaji wa leseni kwa wachimbaji wadogo wadogo wa Wilaya ya Kakonko ili waweze kuanza uchimbaji? Ahsante. (Makofi)

Name

Stanslaus Haroon Nyongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Mashariki

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI (MHE. STANSLAUS H. NYONGO): Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mabadiliko ya Sheria ya Madini ya mwaka 2010 na mabadiliko yake ya mwaka 2017 pamoja na Kanuni zake za mwaka 2018, ni kwamba sasa hivi Tume ya Madini ambayo imeundwa ndiyo itakuwa na wajibu wa kutoa leseni kwa wachimbaji wakubwa, wadogo na wachimbaji wote wa kati. Ni juzi tu Mheshimiwa Rais ndiyo ameteua Mwenyekiti wa Tume ya Madini ambayo sasa ndiyo inaendelea na michakato ya kuchakata kwa maana ya kutoa leseni kwa watu wote walioomba leseni za kuchimba madini. Kwa hiyo, nimueleze Mheshimiwa Mbunge aendelee kuhamasisha wachimbaji wake waombe leseni na sasa Tume imeanza kufanya kazi, watapata leseni walizoomba na wataendelea na uchimbaji. Ahsante sana.