Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Primary Question

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA aliuliza:- Chuo cha Maendeleo ya Wananchi - Gera ni muhimu katika kuchochea maendeleo:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha utendaji wa chuo hicho?

Supplementary Question 1

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwa kuwa mwaka 1975 Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kwa kushirikiana na Shirika la SIDA alianzisha vyuo vya FDC kwa nia ya kutoa ujuzi kwa akina mama wajasiriamali na vijana ili waweze kuongezewa ujuzi na hivyo kuweza kujiajiri; na kwa kuwa Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Nkenge imeandaa mpango mkubwa wa kutoa ujuzi kwa wajasiriamali akinamama na vijana, je, Wizara iko tayari kushirikiana na Ofisi ya Mbunge wa Nkenge katika kutekeleza mpango huo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri alitembelea Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Gera na akakuta zaidi ya shilingi milioni 100 zilizotolewa kwa ajili ya kukarabati zilifanya kazi ndivyo sivyo; na kwa kuwa alitoa maelekezo palepale wale waliofanya kazi chini ya viwango warejee tena kwa gharama yao, je, maelekezo ya Mheshimiwa Waziri yametekelezwa au imebaki kama ilivyokuwa kabla ya kutoa maelekezo yake? (Makofi)

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kama tuko tayari kushirikiana na Ofisi ya Mbunge, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuko tayari kushirikiana naye kwa sababu lengo letu ni moja, tunataka vile vyuo viweze kufanya kazi ili tuendelee kupata nguvukazi ya ufundi na stadi mbalimbali katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ni kuhusu maelekezo yaliyotolewa juu ya ukarabati uliofanyika ambao haujakwenda vizuri. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba maelekezo na uamuzi wa Wizara uko palepale, tutaendelea kufuatilia kuhakikisha kwamba maelekezo yale yanatekelezwa.

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Primary Question

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA aliuliza:- Chuo cha Maendeleo ya Wananchi - Gera ni muhimu katika kuchochea maendeleo:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha utendaji wa chuo hicho?

Supplementary Question 2

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona na naomba niulize swali dogo la nyongeza kuhusiana na mada hii iliyoko mezani.Kwa kuwa Wilaya ya Longido haina chuo hata kimoja, chuo chochote cha Serikali; na kwa kuwa Wilaya hii ya Longido ni ya wafugaji kwa karibu asilimia 100 na ni wilaya ya uhifadhi wa wanyamapori kwa sababu tuna maeneo ya WMA na ya uwindaji, je, Serikali haiwezi kuja kutujengea VETA hasa inayolenga tasnia ya ufugaji mifugo na uhifadhi wa wanyama na mazingira na ikiwezekana Chuo cha Walimu wa Sayansi kwa sababu kuna uhaba mkubwa wa Walimu wa sayansi nchini na tuna ardhi ya kutosha na maji ya Kilimanjaro yanakuja?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba mikoa na wilaya zote nchini zinakuwa na vyuo vya VETA. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeanza kwenye baadhi ya maeneo ambako tayari kuna ujenzi unaendelea na kuna mipango ya kuhakikisha kwamba wilaya zote zinakuwa na vyuo vya VETA. Kwa hiyo, hata Longido tutafika na wakati tunafanya hivyo, tutaangalia zile fani ambazo zitawasaidia wananchi wa pale kuweza kujiendeleza.