Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Stanslaus Shing'oma Mabula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyamagana

Primary Question

MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. AMINA N. MAKILAGI) aliuliza:- Fedha za miradi ya maendeleo kutotolewa kwa wananchi kwa wakati jambo ambalo limekuwa likisababisha hasara na miradi ya maendeleo kuchelewa kukamilika:- Je, Serikali imejipangaje kukabiliana na changamoto hiyo?

Supplementary Question 1

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini kilichokuwa hasa kinatakiwa kipatiwe ufafanuzi, pamoja na majibu mazuri, tunafahamu namna ambavyo mapato ya Serikali yanapatikana kutoka Serikali Kuu na Serikali za Mitaa. Sasa tunachouliza hapa, miradi mingi ambayo imekuwa ikianzishwa kutoka kwenye Halmashauri inayotegemea fedha kutoka Serikali Kuu, fedha hizi haziji kwa wakati na badala yake miradi mingi sana inakuwa mwaka unaisha, miradi inakaa miaka mitano haikamiliki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tunataka tu kufahamu, miradi hii mingine ambayo kwa kweli ingekamilika ingekuwa msaada mkubwa sana kwa wananchi; kwa mfano, kwenye Jimbo la Nyamagana, uko mradi wa maji wa Fumagila, una zaidi ya miaka mwili sasa na umebakiza fedha kidogo sana kutoka Serikali Kuu, kiasi cha shilingi milioni 256 hazijapatikana mpaka leo. Ni lini fedha hizi zitapatikana ili maji yanayokadiriwa kusaidia watu zaidi ya 16,000 yaweze kuwasaidia kwa wakati na kupunguza mzigo kwa akina mama? Ahsante sana.

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi ni kwamba upungufu wowote unaotokana katika vyanzo viwili vya kuchangia katika bajeti yetu hupelekea tatizo hilo, lakini Serikali imejipanga na kwa pamoja tumeona kwamba fedha hizi sasa zimeanza kutolewa. Miradi yote ambayo haijakamilika, Serikali imedhamiria kuendelea kupeleka pesa ili miradi hii iweze kukamilika. Pamoja na mradi wake wa maji alioutaja wa Nyamagana uliobakiza shilingi milioni 200, ninamwahidi kwamba Serikali itapeleka fedha hizo ili kukamilisha mradi huo pamoja na miradi mingine yote ambayo imefikia katika hatua nzuri za utekelezaji.

Name

Richard Phillip Mbogo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. AMINA N. MAKILAGI) aliuliza:- Fedha za miradi ya maendeleo kutotolewa kwa wananchi kwa wakati jambo ambalo limekuwa likisababisha hasara na miradi ya maendeleo kuchelewa kukamilika:- Je, Serikali imejipangaje kukabiliana na changamoto hiyo?

Supplementary Question 2

MHE. RICHARD P. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Naomba niulize swali dogo la nyongeza. Miradi mingi ya maendeleo imekuwa haifanyiki, sababu kubwa pia ni kutokana na baadhi ya gharama za uendeshaji na Halmashauri zetu kutokupelekewa fedha, kwa mfano gharama za kusimamia mitihani. Je, Serikali inajipangaje kulipa madeni hayo kabla mwaka huu wa fedha wa 2015/2016 haujaisha?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbogo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi na katika jibu la swali la nyongeza la Mheshimiwa Mabula, Serikali imejipanga vizuri, mapato yanaongezeka na miradi yote itapelekewa pesa ili iweze kukamilika kwa wakati.