Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Primary Question

MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y RHODA E. KUNCHELA) aliuliza:- Kuna mgogoro kati ya Manispaa na wafanyabiashara wanaomiliki vibanda katika masoko ya Buzogwe Soko Kuu na Mpanda Hoteli ambapo Manispaa inawaongezea kodi wafanyabiashara hao bila makubaliano ya pande zote mbili:- Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kumaliza mgogoro huo maana ni muda mrefu sasa na wafanyabiashara wamefunga vibanda vyao wakisubiri muafaka na hivyo Serikali kushindwa kukusanya kodi?

Supplementary Question 1

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Wafanyabiashara kote nchini hivi sasa wanalalamika biashara zao kuyumba na ukweli uliopo ni kwamba tatizo hili bado linaendelea katika Manispaa hii ya Mpanda. Je, Serikali iko tayari kuiagiza Halmashauri kwa spirit ya utawala bora kukaa tena na wafanyabiashara hawa ili kuweza kwa pamoja kujadili kiwango ambacho Halmashauri na wafanyabiashara watanufaika ili sasa pande zote mbili ziweze kufanya kazi bila manung’uniko?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika utendaji bora na ushirikiano na Halmashauri ni kwamba maeneo mengi utendaji unaonekana kukwama kwa sababu wakati mwingine mabavu yanatumika katika kuweka hivi viwango vya kodi na kadhalika. Ni lini Serikali itatoa maagizo ya hakika kabisa ili Halmashauri zisigombane na wateja wao ambao ni hawa wafanyabiashara na sasa hivi tunavyohimiza Halmashauri ziweze kuongeza vyanzo vipya vya mapato ili mapato ya Serikali kokote katika nchi yetu yasipotee tu kwa sababu ya uhusiano mbaya kati ya Halmashauri pamoja na wafanyabiashara? (Makofi)

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, nafarijika swali kama hili kutoka kwa Mheshimiwa Selasini na bahati nzuri yeye ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala na TAMISEMI. Katika nafasi niliyopata kushiriki katika vikao vyake amekuwa akihimiza Halmashauri zihakikishe kwamba zinakusanya mapato yake ili ziweze kujiendesha.
Mheshimiwa Spika, umenisaidia. Sisi Waheshimiwa Wabunge ni Madiwani tukiwa kwenye halmashauri zetu. Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda ilishirikisha wafanyabiashara, zimeundwa Tume zisizopungua tatu na katika jibu langu la msingi nimeeleza hawa ambao wamekuwa wanapangishiwa wamekuwa wakilipa Sh.100,000 mpaka Sh.150,000.
Mheshimiwa Spika, sasa halmashauri katika kuona katika vyanzo vyao ambavyo ni vizuri wakavisimamia iko katika kupandisha kutoka Sh.15,000 ambayo imekuwa ikitozwa zaidi ya miaka 30 na kwenda mpaka Sh.40,000 which is very fair.
Mheshimiwa Spika, ameelezea juu ya suala zima la kutokuwa na migongano baina ya wafanyabiashara na halmashauri. Kama nilivyoeleza katika jibu langu la msingi, ushirikishwaji umekuwepo na hata ninavyoongea leo hakuna hata kibanda kimoja ambacho kimefungwa katika Manispaa ya Mpanda kwa sababu ushirikishwaji umekuwepo. Zimekuwepo Tume zaidi ya tatu kwa ajili ya kuhakikisha kwamba maridhiano yanakuwepo na halmashauri inapata chanzo chake cha pesa na kinatumika sahihi.

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Primary Question

MHE. JOSEPH R. SELASINI (K.n.y RHODA E. KUNCHELA) aliuliza:- Kuna mgogoro kati ya Manispaa na wafanyabiashara wanaomiliki vibanda katika masoko ya Buzogwe Soko Kuu na Mpanda Hoteli ambapo Manispaa inawaongezea kodi wafanyabiashara hao bila makubaliano ya pande zote mbili:- Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kumaliza mgogoro huo maana ni muda mrefu sasa na wafanyabiashara wamefunga vibanda vyao wakisubiri muafaka na hivyo Serikali kushindwa kukusanya kodi?

Supplementary Question 2

MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Siha inafanana na wilaya iliyotajwa hapo lakini kwa tofauti kidogo, Halmashauri ya Siha ina magulio, haina masoko. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano alishatoa maelekezo kwamba akinamama wanaotandaza bidhaa chini na wale ambao ni wa chini kabisa wasidaiwe ushuru.
Mheshimiwa Spika, cha kusikitisha kabisa jana katika Wilaya ya Siha wananchi kwenye soko la Sanya Juu wameenda kulazimishwa kulipa ushuru kwa kutumia polisi na wananchi waliposema Rais alishasema sisi tunaotandika chini tusilipe waliambiwa Rais huyo huyo ndiye anasema tukusanye kodi na bado yeye anatuvuruga kwenye kukusanya kodi, lipeni ushuru na polisi wakapelekwa sokoni na wananchi walipata taharuki sana.
Mheshimiwa Spika, sasa naomba nielezwe kwamba tunawezaje kuwasaidia hawa akinamama ambao ni vipenzi vya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tayari alishatoa maelekezo na yamekuwa yakipuuzwa na Halmashauri zetu. (Makofi)

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Spika, maelekezo aliyotoa Mheshimiwa Rais kwamba wale akina mama ambao wanapanga bidhaa zao ikiwa ni pamoja na wale ambao wanauza ndizi wasibugudhiwe ni msimamo ambao uko thabiti, hauyumbi hata mara moja. Kama kuna Mkurugenzi yeyote ambaye hataki kutekeleza kauli na maelekezo ya Mheshimiwa Rais tafsiri yake ni kwamba Mkurugenzi huyo hajitaki. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nikuhakikishie, leo wakati naingia nilimwambia Mheshimiwa Mollel katika maeneo ambayo nina wajibu wa kwenda kutembelea ni pamoja na Jimbo lake hii ni pamoja na kwenda kutazama eneo la ujenzi wa hospitali mpya ya wilaya. (Makofi)