Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA N. MAKILAGI aliuliza:- Zipo sheria nyingi ambazo zimepitwa na wakati na sheria nyingine ni kikwazo katika kufanikisha shughuli muhimu za Taifa letu. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuzitambua sheria zote zilizopitwa na wakati na zile zinazochelewesha ukuaji wa uchumi?

Supplementary Question 1

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana na Ajira napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amethibitisha kwamba kweli ziko sheria ambazo zimeshapitwa na wakati na Tume ya Kurekebisho ya Sheria ya Serikali inaendelea kuzifanyia marekebisho. Ningependa kujua ni sheria gani hizo sasa ambazo ziko katika huo mchakato na pia ningependa kujua hizi sheria zinaletwa hapa lini ili Bunge lako tukufu liweze kuzipitisha? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa kumekuwa na kilio cha muda mrefu na hata leo Mheshimiwa Mwenyekiti imethibitisha kwamba kumekuwa na kilio cha muda mrefu cha Waheshimiwa Wabunge Wanawake na Wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kumekuwa na kilio kikubwa sana cha wanawake na vijana juu ya kutungwa sheria ya mfuko wa wanawake na vijana na walemavu. Lakini pia kumekuwa na kilio cha muda mrefu cha wakulima wadogo wadogo kwamba kilimo chao hakiwaletei tija kwa sababu hakuna sheria inayoweka mfumo mzuri wa wakulima wadogo waweze kuletewa tija. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujua sasa. Serikali ina mkakati gani wa kuleta hizi sheria Bungeni. Hili suala la kuwa kila siku tunaambiwa Serikali itaweka msukumo kuhakikisha asilimia 10 ya wanawake na vijana inatengwa ili tuweze kufikia mahali panapohitajika. Ahsante. (Makofi)

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa namna ambavyo amekuwa mstari wa mbele kutetea maslahi ya akina mama nchini na ni kazi kubwa amekuwa akiifanya kwa ajili ya akina mama wa nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza anauliza ni sheria gani zipo katika mchakato. Kama nilivyosema, kazi kubwa ya Tume ya Kurekebisha Sheria ni kupitia sheria na baadaye kutoa mapendekezo kupitia taarifa mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka huu wa fedha Tume inafanya kazi ya mapitio ya sheria za mambo ya jinai (criminal justice) wanafanya pia mapitio ya sheria ya mambo ya evidence law, utoaji wa ushahidi mahakamani, lakini pia wanafanya mapitio ya sheria ya ufilisi (insolvency law) na vilevile wanafanya mapitio ya sheria ya huduma za ustawi wa jamii. Kwa hiyo, hizo ndiyo kazi ambazo zinafanyika katika mwaka huu wa fedha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika swali lake la pili ameuliza kuhusu lini Serikali italeta sheria mahsusi kwa ajili ya utungwaji wa uundwaji wa mifuko hii maalum kwa ajili ya akinamama na vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Naibu Waziri kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI, mifuko ya akina mama na vijana ipo na inaongozwa na miongozo yake tayari na imekuwa ikifanya kazi katika utaratibu huo wa kuchangia asilimia 10 hizo za mapato ya ndani ya Halmashauri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mwongozi tayari upo. Labda ambacho kinaweza kikafanyika ambapo Serikali imekuwa ikijibu hapa ni kuboresha na kuona namna bora ya kuweza kuwafikishia kwa urahisi zaidi akina mama na vijana huduma hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la wakulima wadogo wadogo kutungiwa sheria. Kama Serikali tunaichukua na tutaona umuhimu wake hapo baadaye wa kuweza kulifanyia kazi.