Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Stanslaus Shing'oma Mabula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyamagana

Primary Question

MHE. STANSLAUS S. MABULA aliuliza:- Jimbo la Nyamagana lina ukubwa wa kilometa za mraba 256, kati ya hizo kilometa za mraba 71.56 ni eneo la maji ya Ziwa Victoria lakini bado wananchi wake hawapati maji ya uhakika ya bomba hasa kwa zile Kata zilizoko nje ya Mji. Je, ni lini Serikali itahakikisha kuwa wananchi wa Nyamagana wanapata maji ya uhakika hasa ikizingatiwa kuwa wamezungukwa na Ziwa Victoria?

Supplementary Question 1

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niishukuru tu Serikali kwa huu mradi wa World Bank wa Euro milioni 54 kwa niaba ya Jimbo la Nyamagana pamoja na Ilemela. Lakini niseme tu kwa hali ya kawaida kama wananchi wa Jimbo la Nyamagana wangekuwa wanapata maji kwa asilimia 90 sidhani kama Mbunge wao ningekuwa na sababu ya kusimama hapa na kuomba maji. Niseme tu ukweli ni kwamba inawezekana mtandao wa maji umesambazwa kwa kiasi kikubwa lakini upatikanaji wa maji sio sawa na takwimu zinavyosomwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza; zipo Kata za Buhongwa, Lwanima, Kishiri, Igoma na Nyegezi ni lini Serikali itakuwa tayari pamoja na huu mradi wa Euro milioni 54 kuangalia uwezekano wa kuongeza fedha zingine nyingi zaidi ili wananchi kwenye maeneo haya ya Buhongwa na maeneo ya Lwanima na Kata zingine nilizotaja waweze kupata maji kwa uhakika? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, pale kwenye
Jimbo la Ilemela umekuwepo mradi wa Vijiji kumi toka mwaka 2010 mpaka hivi tunavyozungumza leo ni Kijiji kimoja peke yake cha Kayenze ndio kimepata maji.
Ni lini Serikali itahakikisha Vijiji vya Nyamadoke, Kahama, Kabangaja, Igogwe, Igombe, Kabusungu na Nyafula vinapata maji haya kwa wakati kama ambavyo ilikuwa imekusudiwa? Nakushukuru. (Makofi)

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nichukue nafasi hii kumpokea Mheshimiwa Mbunge kwa sababu kila wakati anakuja ofisini kuhusu Mradi wa Maji wa Nyamagana, ndiyo maana Wizara ya Maji na Umwagiliaji pamoja na juhudi za wafanyakazi wote na Serikali tumehakikisha kwamba tumepata hizi Euro milioni 54 tukiwa pamoja na Mheshimiwa Mbunge. Maana yake kila wakati alikuwa anakuja kuzungumza kuhusu wananchi wake na amekuwa anasema inakuwa ni aibu kwa sababu Ziwa Victoria liko pale na watu hawana maji, ndiyo maana amesaidia katika kulisukuma hili ili tuweze kupata mradi huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge amezungumzia baadhi ya Kata. Mradi huu utakapokuwa umekamilika zipo kata ambazo zitapata huduma ya maji, Kata hizi ni pamoja na Kishiri, Buhongwa, Bugarika, Nyegezi, Lwanima pamoja na Igoma. Aidha, vitongoji ambavyo vinazunguka katika hizo kata tutahakikisha kwamba zimepata maji safi na salama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema kwamba tunakarabati miundombinu iliyopo, ikiwa ni pamoja na mabomba yaliyochakaa, yakichakaa maana yake kupeleka huduma ya maji kwa wananchi inakuwa kidogo kuna shida tutahakikisha sasa na vijiji vingine vyote vilivyobaki vinapata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia amehoji kuhusu tamko la asilimia 90. Hesabu ya asilimia 90 tunaihesabu kwa kuchukua population ya watu waliopo katika lile eneo na kuangalia ni watu wangapi wanaopata maji, hatu-cross over kwenda kwenye vijiji vyote, hapana! Tunaangalia una watu wangapi katika Kata ya Nyamagana, je, ni wangapi ambao wanapata maji ndiyo tunapiga mahesabu kuhakikisha kwamba sasa hiyo asilimia tunaipata. Kwa hiyo, kunaweza kukawa na Kata lakini kwa sababu zina watu wachache ukakuta kwamba asilimia hii ni kubwa kumbe kuna Kata ambazo bado hazijapata maji. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo tumeendelea kushirikiana kufuatilia suala la wananchi wa Nyamagana kupata maji, tuendelee kuwasiliana ili kuona ili mradi utakapokamilika kusiwe na eneo litakalobaki bila kupata maji. (Makofi)

Name

Kiswaga Boniventura Destery

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Magu

Primary Question

MHE. STANSLAUS S. MABULA aliuliza:- Jimbo la Nyamagana lina ukubwa wa kilometa za mraba 256, kati ya hizo kilometa za mraba 71.56 ni eneo la maji ya Ziwa Victoria lakini bado wananchi wake hawapati maji ya uhakika ya bomba hasa kwa zile Kata zilizoko nje ya Mji. Je, ni lini Serikali itahakikisha kuwa wananchi wa Nyamagana wanapata maji ya uhakika hasa ikizingatiwa kuwa wamezungukwa na Ziwa Victoria?

Supplementary Question 2

MHE. KISWAGA B. DESTERY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Kwanza naishukuru Serikali kwa kutupa mradi wa maji pale Magu Mjini, mkandarasi yuko site; lakini pia nipongeze Kampuni ya Alliance Ginnery, mwekezaji amechimba kisima kirefu pale salama na kinatoa lita 9,000 kwa saa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa suala hili la Nyamagana linafanana kabisa na Jimbo la Magu, kijiografia na kwa fursa zilizopo. Katika Tarafa ya Sanyo kwa maana ya Kisesa yote na vijiji vyake pamoja na Tarafa ya Ndagalu kuna hali mbaya sana ya maji katika Vijiji vya Ng’aya, Salama, Ndagalu, Nyabole, Kabila na Mahala...

MHE. KISWAGA B. DESTERY: Mheshimiwa Mwenyekiti, je, kwa sababu Halmashauri tumeomba dharura, ni lini Serikali sasa itatupatia fedha kwa ajili ya kuchimba visima virefu ili tuweze kusaidia wananchi hao?

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kweli kabisa kwamba tumesaini mradi mkubwa ili kupata maji Wilaya ya Magu Mjini, lakini nikiri kwamba kuna kata ambazo ziko pembezoni na huo Mji ambazo bado hazijapewa huduma ya maji, lakini nichukue ombi lako, tuhakikishe kwamba tunapeleka visima, nikuombe Mheshimiwa Mbunge tuwasiliane. Sio wewe tu katika tarafa zako, zipo tarafa nyingi, wengine ni majirani zako, pale Kasoli hakuna maji. Kwa hiyo, niombe tuwasiliane ili tuweze kuangalia tufanyeje kupitia kwenye bajeti zako au maeneo mengine yoyote utakayoona yanawezekana tuhakikishe kwamba hayo maeneo yaliyobaki ya vijiji nayo pia yanapata walau dharura kwa kuchimbiwa visima kama maji yatakuwepo chini ya ardhi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lengo la Wizara ya Maji na Umwagiliaji kuhakikisha kwamba wananchi wote wa Tanzania popote pale walipo, tunawapatia maji safi na salama. (Makofi)

Name

Salma Mohamed Mwassa

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. STANSLAUS S. MABULA aliuliza:- Jimbo la Nyamagana lina ukubwa wa kilometa za mraba 256, kati ya hizo kilometa za mraba 71.56 ni eneo la maji ya Ziwa Victoria lakini bado wananchi wake hawapati maji ya uhakika ya bomba hasa kwa zile Kata zilizoko nje ya Mji. Je, ni lini Serikali itahakikisha kuwa wananchi wa Nyamagana wanapata maji ya uhakika hasa ikizingatiwa kuwa wamezungukwa na Ziwa Victoria?

Supplementary Question 3

MHE. SALMA M. MWASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uhaba wa maji katika Mkoa wa Dar es Salaam bado ni mkubwa sana, hasa kwenye maeneo ambayo hayana miundombinu ya maji. Miradi ile mikubwa ya maji imeainishwa kwamba itatekelezwa Dar es Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini sasa Serikali itatekeleza miradi hiyo ya maji ipasavyo ili wananchi hao wa Mkoa wa Dar es Salaam waweze kupata maji kwa uhakika na umakini, hasa kwenye maeneo ya Makabe, Goba, Msigani na maeneo yote ya Gongo la Mboto? Ahsante.

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa kama tulivyotoa taarifa katika Bunge hili, tumekamilisha miradi miwili mikubwa, Ruvu Juu na Ruvu Chini. Ruvu Chini inatoa lita milioni 270 kwa siku, Ruvu Juu inatoa lita milioni 196 kwa siku, pia mwezi huu tunakamilisha vile visima 20 Mpera na Kimbiji ambavyo vitatoa lita milioni 260 kwa siku. Kwa hiyo huduma ya maji kwa Jiji la Dar es Salaam na sehemu ya Pwani itakuwa ya uhakika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, iko changamoto ya kupeleka miundombinu, kwa sasa hivi tumesaini mkataba mmoja wa bilioni 32 ya kuweka mtandao wa maji pamoja na kuongeza matenki ya kuhifadhi maji kupeleka kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tumeshafanya mipango tayari, tunahitaji dola milioni 100 ili tuweze kuhakikisha kwamba tunakamilisha usambazaji wa maji katika Jiji la Dar es Salaam. Tunaendelea baada ya muda ambao siyo mrefu sana tutaona kwamba vijiji vyote, maeneo yote, mitaa yote ya Dar es Salaam inapata maji safi na salama, kwa sababu maji yapo kilichobaki ni kusambaza.

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. STANSLAUS S. MABULA aliuliza:- Jimbo la Nyamagana lina ukubwa wa kilometa za mraba 256, kati ya hizo kilometa za mraba 71.56 ni eneo la maji ya Ziwa Victoria lakini bado wananchi wake hawapati maji ya uhakika ya bomba hasa kwa zile Kata zilizoko nje ya Mji. Je, ni lini Serikali itahakikisha kuwa wananchi wa Nyamagana wanapata maji ya uhakika hasa ikizingatiwa kuwa wamezungukwa na Ziwa Victoria?

Supplementary Question 4

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Pamoja na Jimbo la Mbeya Vijijini kuzungukwa na milima inayotiririsha maji mwaka mzima, lakini wananchi katika vijiji vingi hawana maji salama.
Je, ni lini Serikali itajenga miundombinu kwa kuwapatia maji salama wananchi wa vijiji vya Mbeya Vijijini? Ahsante.

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari tunaendelea na usanifu na baadhi tumeshasaini mikataba kwenye Jimbo lake kuhakikisha kwamba wananchi wote wa Mbeya Vijijini, Jimbo la Mheshimiwa Mbunge wanapata maji safi na salama. Tulikuwa tumebuni miradi kwenye vijiji kadhaa lakini baadae tukagundua kwamba yale maji yatakwenda kwenye kijiji cha mwisho na kuacha vijiji vya katikati, tumechelewa kwa sababu ya kuhakikisha kwamba tunaainisha na vijiji vya katikati. Nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mwaka ujao wa fedha mapema kabisa tutasaini mikataba, na mimi Mheshimiwa Waziri ameshanipangia ratiba, katika ratiba Mikoa nitakayoizungukia ni pamoja na Mkoa wa Mbeya. Kwa hiyo ntahakikisha tunaambatana na wewe kwenda kwako ili tuweze kuona hivyo vijiji vyenye uhaba mkubwa wa maji.