Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Victor Kilasile Mwambalaswa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupa

Primary Question

MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA aliuliza:- Je, ni nini Sera ya Magari ya Serikali?

Supplementary Question 1

MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na napenda kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu, vilevile napenda kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa azma yake ya kupunguza matumizi yasiyo ya lazima. Vilevile kwenye issue ya magari naipongeza Serikali kwa kuamua kununua kwa wingi (bulk procurement) ambayo inapunguza bei, na vilevile kununua kwa mtengenezaji badala ya kununua kwa mtu wa katakati ambayo nayo inapunguza bei, nawapongeza.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maswali mawili ya nyongeza.
Sasa hivi Serikali pamoja na kwamba haina sera ya magari, magari mengi yanayotumika ya Serikali ni Toyota, bei ya Toyota Land Cruiser VX bila ushuru ni shilingi milioni 220. Bei ya Toyota Land Cruiser Prado ambazo kwa sifa zote zinafanana ni shilingi milioni 120 bila kodi. Kwa hiyo, Serikali ikiamua kununua magari 20 ya VX na ikaacha ikanunua Prado ita-save karibu shilingi bilioni mbili ambayo inaweza ikatatua matatizo ya maji katika Mji wa Chunya, Mji wa Makongorosi hata Mkwajuni kwa Wilaya mpya ya Songwe. Je, Serikali inasemaje kuhusu kuachana na VX na kutumia Prado kwama inavyotumia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar?(Makofi)
Swali la pili, kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba Serikali inafuata Sheria ya Udhibiti na Ununuzi wa Mali ya Umma Sura ya 410. Sheria hiyo inasisisitiza ununuzi wa mali ya umma ni kwa tender na disposal ya mali ya umma ni kwa tender. Zamani ilikuwa magari ya Serikali yale yanayochakaa yanakusanywa...

MHE. VICTOR K. MWAMBALASWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa. Magari yanakusanywa MT Depot na yanauzwa kwa tender. Siku hizi hawafanyi isipokuwa Idara ya Usalama wa Taifa ndio inauza kwa tender.
Serikali inasemaje kuhusu Viongozi wa Serikali ambao wanajiuzia magari yaliyochakaa badala ya kuuza kwa tender? (Makofi)

Name

Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyosema masuala ya ununuzi wa magari ni masuala yanayosimamiwa na sheria vilevile Wizara ya Fedha ndio inayosimamia GPSA. Kwa maana hiyo, nachukua maoni yake tutaenda tukayafanyie kazi kwa kushirikisha GPSA pamoja na Wizara ya Fedha pamoja na Idara Kuu ya Utumishi ili hatimaye tupate majibu sahihi na hatimae nitakueletea hayo majibu sahihi Mheshimiwa Victor Kilasile Mwambalaswa. (Makofi)

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nataka kuongezea kidogo hasa kuhusu magari baina ya Toyota Prado na Landcruiser VX.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati unanunua kitu unaagalia mahitaji yako, kwanza unangalia bei, unaangalia safety, unaangalia mantainance cost, vitu vyote hivi unaviangalia baada ya hapo ndio unaweza kupima. Ukinunua gari baina ya Zanzibar na Bara ni mazingira tofauti, magari yanayotumika Zanzibar yanatumika kwa siku pengine kilometa 30, hapa mtu anasafiri takribani kilometa 200, 300 mpaka 500 mpaka 1,000 kwa siku, 1,200 naambiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile ukinunua gari inabidi vitu vyote hivi uviangalie, sio uangalie price tu. Uangalie comfort, uangalie safety, uangalie mainatainance cost na vitu vingine vyote. Ahsante. (Makofi)