Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Munde Abdallah Tambwe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MUNDE T. ABDALLAH aliuliza:- Pamoja na jitihada za Serikali na mmiliki wa Kiwanda cha Nyuzi Tabora (TABOTEX) ambazo zimewezesha kiwanda hicho kuwa katika hali ya kufanya kazi bado kiwanda hicho kinakabiliwa na ukosefu wa soko la bidhaa zake:- Je, ni kwa nini Serikali isikipatie kiwanda hiki hadhi ya EPZ ili kipate vivutio vitakavyokiwezesha kupata ushindani katika masoko ya nje?

Supplementary Question 1

MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo mawili ya nyongeza. Pamoja majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Viwanda napenda kuuliza maswali kama ifuatavyo.
Swali la kwanza; kiwanda cha Nyuzi cha Tabora kinazalisha vifa tiba ambavyo vinatangenezwa na pamba yetu inayolimwa hapa hapa nchini. Inazalisha vifaa kama pamba, bandage na nyuzi. Je, kwa nini Serikali kupitia MSD isimuunge mkono Mheshimiwa Rais maneno yake aliyotamka Mwanza na kununua vifaa tiba kwenye viwanda vyetu vya ndani hususan Tabora badala ya kuagiza nje ya nchi?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kiwanda hicho kina uwezo wa kutengeneza sare za wanafunzi (uniform). Kwa nini sasa Serikali isitoe agizo, badala ya kununua sare za shule sehemu tofauti, sare za shule zinunuliwe kwenye viwanda vilivyopo nchini? Kwanza, ili kuchochea uchumi pia kupanua ajira hususan katika Mkoa wetu wa Tabora ambao kwa kweli hauna viwanda vya kutosha. Naamini vijana wetu wa Tabora watapa ajira za kutosha kama sare zitanunuliwa katika kiwanda hicho cha nyuzi cha Tabora.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.(Makofi)

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ni kweli kabisa iko haja ya kuunga mkono jitihada zinazofanywa na viwanda vyetu nchini ikiwemo vifaa tiba. Kimsingi viwanda hivi wakati vinaanzishwa vilikuwa na lengo la kusaidia kutoa malighafi katika viwanda vingine, lakini baada ya kuanza biashara huria na mikataba mbalimbali tuliyosaini Kimataifa, tumejikuta kwamba baadhi ya viwanda vyetu vinashindwa kuzalisha kutokana na wadau waliokuwa wanunue vifaa hivyo kutoka kwetu wanaamua kuagiza kutoka nje.
Mheshimiwa Naibu Spika, hilo ni suala ambalo Wizara tayari tumeshaliona na tunalifanyia kazi. Vilevile kuimarisha masoko ya ndani na nje kwa hiyo kitengo chetu kitaendelea kufanyia kazi eneo hilo na hivyo niwaombe MSD waweze pia kufuatilia na kuweza kununua pamba na bandage zinazozalishwa katika kiwanda hiki nasi tutafutilia.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusu uniform; naomba vilevile kuwashawishi wadau mbalimbali ambao wanatumia uniform zinazofanana na zile zinazozalishwa katika kiwanda hiki waweze kukipatia kipaumbele pamoja na viwanda vingine ambavyo viko humu nchini. Niwaombe pia Watanzania wote kupenda bidhaa zetu kwanza. Tufahamu kwamba viwanda hivi vinapokufa vinakosesha ajira kwa watu wetu na kwa kweli uzalendo ni kutumia mali zetu za ndani. (Makofi)

WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nichukue fursa hii kumshukuru na kumkaribisha Naibu wangu mpya. Napenda nitoe jibu la nyongeza kuhusu bidhaa tiba za Tabora Textile.
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Mbunge Munde Tambwe kwa jinsi alivyopigana kufufua kiwanda hiki, watu wa Tabora watamkumbuka. Nataka nisisitize tamko la Mheshimiwa Rais, Wawekezaji wa Tabora Textile na wote mnaozalisha vifaa tiba nendeni sasa hivi MSD, msisubiri MSD iwafuate. Ni agizo la Rais kwamba MSD kwanza inunue vifaa vinavyotengenezwa hapa ndiyo maana ya kutenga bilioni 269 kwa ajili ya tiba. Kwa hiyo wote nendeni mkanunuae vifaa pale, mkauze vifaa vyenu pale kwa kufuata taratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hili la uniform, hili wazo la uniform namshukuru Mheshimiwa Tambwe, maamuzi yetu sasa tutaleta mapendekezo kwenu na watu wasituletee mambo ya WTO. Tukiweza kununua uniform kutoka kwenye viwanda vyetu vya nguo, tutaweza kuchochea viwanda vyetu kufanya kazi na kutumia pamba yetu badala ya kununua nguo zisizofaa zinazotoka nje ya nchi. Hiyo italeta kelele tunategemea ninyi Wabunge mtusaidie kutetea viwanda vyenu vya ndani. Ahsante. (Makofi)