Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Eng. James Fransis Mbatia

Sex

Male

Party

NCCR-Mageuzi

Constituent

Vunjo

Primary Question

MHE. JAMES F. MBATIA aliuliza:- Sheria ya Maslahi na Mafao ya Majaji Namba tatu (3) ya Mwaka 2007 Kifungu cha 8; inafafanua kuwa Jaji Mkuu, Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi au Jaji wa Mahakama Kuu akifariki dunia akiwa madarakani au baada ya kustaafu, Serikali itagharamia gharama za mazishi na Kifungu cha 10 cha Sheria hiyo kinafafanua malipo ya pensheni na huduma nyingine atakazostahili Jaji wakati wa kustaafu kama ilivyo kwenye Kifungu cha 20 na 21 cha Sheria ya Utumishi wa Umma:- Je, Serikali haioni busara kuifanyia marekebisho sheria hiyo au vinginevyo ili Majaji waweze kupatiwa huduma muhimu na hasa matibabu wakati wanapostaafu?

Supplementary Question 1

MHE. JAMES F. MBATIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Swali la kwanza, Majaji waliostaafu kabla ya mwaka 2013 ambao siyo wengi, hawako kwenye hali nzuri sana wakati wa kupata matibabu. Serikali haiwezi ikatumia busara hili suala likawa ni la kiutawala (administrative) ili bajeti ya Wizara ya Katiba na Sheria ikawahudumia Majaji hawa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Political Leaders Pension Act ya Mwaka 1981 inaelezea pamoja na watu wengine ambao wanatakiwa kupata pension, angalau wapo kazini kwa miaka 10 ni Wabunge. Je, Serikali haioni busara kuleta Muswada hapa Bungeni ili kufufua Sheria hii ya mwaka 1981 ili Wabunge waweze kupata pension? (Makofi)

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la kwanza amezungumza kuhusu Majaji waliostaafu kuanzia mwaka 2013. Kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge ni kweli kwamba, kwa mujibu wa Sheria iliyoanzisha Bima ya Taifa ya Afya, Kifungu Namba 11(3) kinaeleza kuhusu wale watumishi wa Serikali waliokuwa wana-hold Constitutional Office ambao wanaweza kunufaika katika matibabu ya afya. Hata hivyo, katika Kifungu hicho pia, kupitia Sheria hii ya Mwaka 2007 imetamka pia, aina ya watu wanaostahili kupata huduma na stahiki kutokana na sheria ambayo imesomwa ya mwaka 2007.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, katika hili ombi la Mheshimiwa Mbunge la kwamba Serikali ione busara, kwa sababu ni suala ambalo linahusisha pia Sera na Sheria niseme tu kwamba, kama Serikali tunalichukua, lakini siwezi kuweka commitment ya kwamba litafanyika, ni pendekezo limetolewa, linahitaji kwenda kuangalia sera na sheria ambazo zinatuongoza, hasa kuanzia yale mafao ya Majaji, na sheria ambazo pia zinahusika kwa maana ya watoa huduma katika baadhi ya masuala ambayo yanawahusu Majaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili ameuliza kuhusu pension kwa Wabunge. Ombi la Mheshimiwa Mbunge hapa ni kufufua tu sheria, sasa Waheshimiwa Wabunge kwa sababu, masuala haya yanaweza kupitia Tume ya Utumishi wa Bunge na ninyi ndiyo Wabunge, lianzie kwenu kwanza ndiyo lifike Serikalini. Kwa hiyo, hii ni kazi ya Kibunge lianzie katika upande wa Bunge. (Makofi)