Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Primary Question

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Watendaji wa Vyama vya Msingi vya Mazao (AMCOS) wanapatikana kwa njia ya ushindani na wanakuwa na sifa zinazostahili?

Supplementary Question 1

MHE ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza, Mheshimiwa Naibu Waziri atakuwa shahidi kwamba kuna ukiukwaji mkubwa wa sheria kwa sababu kuna watendaji wengi wa hizo AMCOS ambao hawana sifa zilizotajwa kisheria. Kwa hiyo, napenda kujua Serikali inatoa kauli gani kuhusu AMCOS ambazo zimeajiri watendaji ambao hawana sifa?
Mheshimiwa Spika, pili, kutokana na kazi kubwa ambazo wanazifanya watendaji hawa wa AMCOS hasa wale wa Mikoa ya Mtwara na Lindi ambao sasa hivi wanashughulikia zao la korosho na wanashughulika na fedha nyingi sana, Serikali ina mpango gani wa kuwajengea uwezo kwa kuandaa mafunzo maalum ili kupunguza ubadhirifu na upotevu wa pesa ambao siyo wa lazima? (Makofi)

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Spika, kabla sijajibu, naomba nikiri kwamba Mheshimiwa Chikota ni mmoja kati ya Waheshimiwa Wabunge wanaofuatilia sana masuala ya ushirika kwa niaba ya wananchi wake. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu kwamba kama kuna mfanyakazi yeyote na mtendaji wa Chama cha Ushirika ambaye hajakidhi matakwa ya kisheria, kimsingi huyo amekaa mahali ambapo siyo pake. Kama ana ushahidi wa watendaji ambao wameajiriwa kinyume na taratibu au kinyume na sifa ambazo nimezitaja kwa mujibu wa sheria, naomba anipe orodha yao na mimi nitashughulika nao. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, anasema kwa nini Serikali haitoi mafunzo au kuwajengea uwezo watendaji wa vyama vya ushirika, naomba nimfahamishe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba moja kati ya kazi ya Vyama vya Ushirika, hasa Vyama Vikuu, ni kuhakikisha vilevile kwamba watendaji wa Vyama vya Msingi wanajengewa uwezo. Kwa hiyo, tunaendelea kusisitiza kwamba Vyama Vikuu vishirikiane na Vyama vya Msingi kuhakikisha kwamba wanatoa elimu ya mara kwa mara kwa watendaji wa Vyama vya Msingi. Vilevile, nitumie fursa hii kuwaagiza Maafisa Ushirika katika wilaya zote wahakikishe kwamba wanatekeleza jukumu lao la msingi la kuendelea kutoa elimu na kuwajengea uwezo viongozi pamoja na watendaji wa Vyama vya Ushirika.

Name

Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Primary Question

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Watendaji wa Vyama vya Msingi vya Mazao (AMCOS) wanapatikana kwa njia ya ushindani na wanakuwa na sifa zinazostahili?

Supplementary Question 2

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri anakiri kwamba hili tatizo la watendaji wasiokuwa na sifa ni moja ya tatizo kubwa sana kwenye zao la korosho na Serikali inatambua kwamba msimu wa korosho uliomalizika tumepata upotevu mkubwa sana wa pesa.
Sasa Serikali haioni wakati umefika wa kubadilisha sifa zinazotumika za kuwapata hawa watendaji? Nasema hivyo kwa sababu kiwango hicho kidogo cha elimu ni moja ya sababu ya wao kuzungukwa na watendaji wa mabenki na watendaji wengine wanaohusika katika mfumo na matokeo yake pesa nyingi sana zinapotea na wakulima wanapata hasara. (Makofi)

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Spika, ni kweli kama Mheshimiwa Mbunge anavyosema, kwamba mara nyingine elimu na uwezo mdogo wa watendaji wa Vyama vya Ushirika inaweza ikawa kikwazo kikubwa cha wao kuweza kufanya kazi kwa ufanisi, hasa pale kiwango kikubwa cha fedha kikiwa kinahusika. Naomba nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba sheria haisemi kwamba ni lazima mtu awe na elimu ya kidato cha nne, inasema kuanzia. Kwa hiyo maana yake, hata kama kunakuwa na waombaji wa nafasi zile wana elimu zaidi bado wanaweza kuchukuliwa.
Mheshimiwa Spika, naomba nisisitize kitu kimoja, kuwa na elimu kubwa mara nyingine siyo kigezo cha uadilifu na tabia njema. Leo hii tunafahamu Vyama vyetu vya Msingi ni vyama vya wakulima, vinashughulikia maslahi ya watu wa kawaida, ukija kupeleka wataalam, wanaweza wakawa wataalam wana elimu nzuri lakini vilevile wakawa wataalam wa kupiga. Kwa sababu hata huko Serikali Kuu na maeneo mengine unasikia kwamba mara nyingine wapigaji ni watu ambao elimu zao ni kubwa. Kwa hiyo, tutaendelea kuangalia ni namna gani ya kuboresha mazingira ya utendaji wa Vyama vya Ushirika, lakini kwa sasa sheria haimkatazi mtu mwenye degree au masters kuwa Mtendaji wa Chama cha Msingi. (Makofi)