Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Primary Question

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza:- Je, ni lini Serikali itawapatia wananchi wa Kyerwa haki yao ya kusikiliza Redio ya Taifa (TBC Taifa) ili kujua yanayoendelea katika nchi yao kama ilivyokuwa hapo awali kabla ya kubadilisha teknolojia ya habari, badala yake sasa wanasikiliza redio za Rwanda na Uganda.

Supplementary Question 1

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali imekiri kuwa Redio ya Taifa haisikiki katika Wilaya ya Kyerwa na wananchi hao wanapofungua redio wanapata Redio ya Rwanda na Uganda kitu ambacho kimewafanya wananchi hawa kuonekana kama wametengwa kwa sababu hawawezi kupata taarifa ambazo ni muhimu zinazohusu Taifa lao.
Je Serikali haioni kuwa wananchi hawa wamekosa haki yao ya msingi ya kupata habari za Serikali hasa hasa kutoka kwa viongozi wao kama Mheshimiwa Rais anapokuwa anaongea na viongozi wengine? Hata mimi Mheshimiwa Mbunge ninapokuwa Bungeni nawawakilisha, hawa wananchi hawapati taarifa yoyote. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Serikali haioni haja ya kuchukua hatua za dharura ili wananchi hawa waweze kupata taarifa ya Redio ya Taifa kwa sababu wanakosa hii haki ya msingi? Laini hata Televisheni ya Taifa haisikiki wala haionekani vizuri. Ahsante. (Makofi)

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent Bilakwate. Pia nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Innocent kwa maswali yake mawili mazuri.
Mheshimiwa Spika, kwanza, naomba unipe ridhaa ya kuelezea suala hili kwa kirefu kidogo kwa sababu tuna Wilaya karibu 84 ambazo hazina usikivu wa redio katika nchi hii na suala hili limesababisha Wabunge wengi mara kwa mara kuuliza maswali yanayohusiana na usikivu wa redio yao ya Taifa. Kwa hiyo, naomba nitoe ufafanuzi kidogo ili kusudi tuweze kusaidiana kwa pamoja na kuhakikisha kwamba tatizo hili linapata ufumbuzi.
Mheshimiwa Spika, kwanza ametaka kujua kwamba Serikali haioni kwamba wananchi wanakosa haki yao ya msingi ya kusikiliza redio yao ya Taifa. Nitoe tu maelezo kwa kifupi kwamba kuna matatizo ambayo yanasababisha au tuseme kuna factors ambazo zinasababisha kuathiri usikivu wa redio katika maeneo mbali mbali. Kwanza, ukirudi nyuma tulikuwa tunatumia mitambo ya medium wave ambayo ilikuwa inaenea katika nchi nzima lakini kutokana na uchakavu wa mitambo hii na gharama kubwa ya kuinunua au kuikarabati imebidi sasa tuweke mitambo ya FM katika kila mkoa. Kwa hiyo, kila mkoa una mtambo wa FM.
Mheshimiwa Spika, sasa masuala ambayo yanaathiri usikivu kwanza ni capacity ya ule mtambo wenyewe lakini pia uwepo wa milima katika maeneo husika kwa mfano kama eneo la Mheshimiwa Innocent kuna milima mirefu ambayo mitambo hii inashindwa kuufikia. Suala lingine ambalo linaathiri usikivu ni ule uharibifu wa baadhi ya vifaa kama power amplifier ambao unatokana na matatizo mbalimbali kama vile radi au kukatika kwa umeme. Katika eneo la Mheshimiwa Innocent, kule Bukoba upo mtambo ambao kuna kifaa kimeharibika – MOSFET imeharibika na imekufa kabisa, kwa hiyo, usikivu umeathirika katika eneo hilo.
Mheshimiwa Spika, hatua za haraka ambazo tumeamua kufanya, kwanza nimeshatoa maagizo ili kusudi wataalam waende katika maeneo yake, katika Wilaya ya Kyerwa ili kuweza kuona jinsi gani ya kutatua tatizo hili kwa sababu kwanza uwezekano upo wa kuweka booster, lakini pia waone kama wanaweza wakanunua kifaa kile ambacho kimeharibika.
Vilevile kuna utaratibu ambao sasa hivi TBC inafanya kuubadilisha mfumo wa satellite uplink ambayo iko Mikocheni, tunaamini kabisa kwamba hii satellite uplink ikirekebishwa ikawa ya kisasa zaidi tutaboresha usikivu kwa asilimia takribani 15 hivi.
Kwa hiyo, niwaombe Waheshimiwa Wabunge ambao maeneo yao hayana usikivu, kufikia mwisho wa mwaka huu tunaamini kabisa hii satellite uplink inaweza ikawa imerekebishwa, kwa hiyo, usikivu utakapokuwa umeboreka katika maeneo yao watupe taarifa. Vilevile, kutokana na uharibifu wa vifaa katika vile vituo vyenyewe, yale maeneo ambayo yana usikivu wakati wowote watakapoona usikivu umesita katika maeneo yale watupe taarifa mapema ili kusudi wataalam wetu waweze kufuatilia.
Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo tunafanya kwa sasa hivi ni huu utaratibu wa kuweka mitambo ya FM yaani kuongeza transmitter katika maeneo mbalimbali. Kwa hiyo, nimetoa maagizo tayari kwamba wataalam wapite katika maeneo ya mipakani waone ni wapi panapostahili kuwekwa boosters lakini ni wapi pia ambao panastahili kuwekwa transmitters mpya. Ahsante. (Makofi)

Name

Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza:- Je, ni lini Serikali itawapatia wananchi wa Kyerwa haki yao ya kusikiliza Redio ya Taifa (TBC Taifa) ili kujua yanayoendelea katika nchi yao kama ilivyokuwa hapo awali kabla ya kubadilisha teknolojia ya habari, badala yake sasa wanasikiliza redio za Rwanda na Uganda.

Supplementary Question 2

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Spika, kwa maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri anasema takribani Wilaya 84 hazipati usikivu. Swali langu, ni kwa nini sasa ile kauli mbiu ya TBC ya Ukweli na Uhakika msiifute na muwe na kauli mpya?

Name

Anastazia James Wambura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, hatuwezi kufuta hiyo kauli mbiu kwa sababu tunatoa taarifa za ukweli na za uhakika, haihusiani kabisa na usikivu. Ahsante. (Makofi)