Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Angelina Adam Malembeka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza:- Kuna vijana zaidi ya 300 Mkoa wa Kaskazini Unguja ambao wanajihusisha na kazi mbalimbali za kujitolea kama vile usafi, upandaji miti, kilimo cha mboga mboga na matunda na wapo tayari kijiunga na Jeshi la Ulinzi kama wakifikiriwa:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuwachukua vijana hao kujiunga na Jeshi hasa ikizingatiwa kuwa wana maadili mema na wameweza kujitolea?

Supplementary Question 1

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, kwa kuwa utaratibu aliousema ulishawahi kufanyika katika wilaya mbalimbali hapa nchini na baadaye tukaambiwa utaratibu huo umesitishwa, je, ni lini zoezi hilo litaanza tena ili vijana waweze kujiunga na Jeshi?
Mheshimiwa Spika, pili, ni nini kauli ya Serikali juu ya ajira ya Jeshi kwa vijana wenye maadili mema na uwezo katika Mkoa wa Kaskazini Unguja na Tanzania kwa ujumla?Ahsante.

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, utaratibu niliousema haujasitishwa, bado utaratibu huu unatumika, kila mwaka tunachukua vijana kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa kupitia katika wilaya na mikoa yao. Kwa hiyo, utaratibu huo bado unatumika. Mwaka huu tumefanya zoezi hilo mwezi Desemba na tunategemea tutakapopata fedha baada ya bajeti basi awamu inayofuata utaendelea.
Mheshimiwa Spika, kuhusu vijana anaowazungumzia Mheshimiwa Malembeka, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, ni kwamba tutakapotangaza tena kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa, nitawaomba vijana hao waombe kupata nafasi za kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa na ajira kwenda Jeshi la Wananchi zinapitia katika Jeshi la Kujenga Taifa. Si Jeshi la Wananchi peke yake, kwa sasa vyombo vyote vya ulinzi na usalama vimeamua kwa makusudi kwamba ajira zao zipitie JKT. Kwa hiyo Polisi, Magereza, Uhamiaji, Usalama wa Taifa, Jeshi lenyewe la Wananchi wa Tanzania wote wanachukua vijana waliopitia Jeshi la Kujenga Taifa, kwa hiyo nitawaomba wajiunge huko ili hatimaye waweze kupata ajira hizo.