Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Yussuf Salim Hussein

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Chambani

Primary Question

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN aliuliza:- Kumekuwa na ongezeko kubwa sana la uwekezaji katika sekta ya utalii nchini:- Je, Serikali imejipanga vipi ili kukabiliana na ongezeko hilo?

Supplementary Question 1

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu marefu ya Mheshimiwa Waziri, lakini naomba nimuulize maswali mawili ya nyongeza. Nchi yetu imejaliwa kuwa na vivutio vingi vya utalii na ni dhahiri majibu ya Mheshimiwa Waziri inaonesha nchi yetu inaona utalii ni mbuga na wanyama tu; na ni dhahiri kwamba ukanda wa bahari unawekwa katika majibu kuonekana tu kama nao upo. Ni dhahiri pia kwamba nchi yetu sasa hivi ina eneo kubwa la bahari kuanzia Tanga mpaka Mtwara lakini utalii wa baharini kama diving, fishing na snorkeling unakua kwa kasi na una fedha nyingi sana. Je, Serikali ina mpango gani madhubuti sasa wa kukuza utalii wa baharini katika nyanja hizo za fishing, diving na snorkeling? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili; kuna matatizo makubwa ya upatikanaji wa umeme na maji katika maeneo ya uwekezaji na hili wawekezaji wanalalamika sana hata huko ambako unasema kwamba TANAPA wanafanya kazi pamoja na Ngorongoro. Wawekezaji wanalalamika kwamba kuna urasimu mkubwa wa kupata vibali vya uchimbaji wa visima au kupeleka umeme kwa ajili ya kutumia katika hoteli zao. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kweli kabisa wa kuondoa urasimu na gharama kubwa kwa wawekezaji katika kupata huduma hizi muhimu?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kama amesikia vizuri kwenye jibu langu la msingi nilipokuwa nazungumzia diversification of tourism products (utanuaji wa wigo wa vivutio vya utalii), kwa bahati mbaya kwenye swali la msingi alisikia Ngorongoro na Hifadhi za Taifa za TANAPA akasema ni wanyamapori tu peke yake, lakini ukweli ni kwamba pale Ngorongoro tuna kivutio kikubwa sana ambacho kina sifa kubwa duniani na sasa hivi ni mwelekeo wa watalii wengi sana kuja kuona chimbuko la binadamu duniani ambayo si wanyamapori, hilo ni suala tu la kihistoria.
Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu suala lake la kukuza utalii katika maeneo mengine, ametaja mfano mmoja tu wa eneo la fukwe za bahari. Huo ni mpango wa Serikali na tayari tumekwishafanya kazi ya awali ya kufanya tathmini ukanda mzima wa bahari kutoka Tanga mpaka Mtwara jumla ya kilometa 1,000 na tumebaini maeneo kadhaa ambayo yana umiliki wa aina mbalimbali, maeneo mengine yanamilikiwa na watu binafsi na watu kama hao. Kwa hiyo Serikali iko kwenye mpango wa kuweza kuangalia namna bora zaidi ya kuweza kuelekeza uwekezaji kwenye maeneo hayo ili tuweze kuweka vivutio hivyo vya diving, fishing, snorkeling na aina nyingine ya utalii wa bahari na utalii wa fukwe.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili la upatikanaji wa umeme na maji. Kwa ufupi kabisa, Serikali inayo taarifa juu ya changamoto hizo kwenye eneo hilo na tunachokifanya sasa hivi ni kushirikisha Serikali kwa ujumla wake; Wizara inayohusika na mambo ya umeme na ile inayohusika na maji, lakini pia kushirikisha wadau wa sekta binafsi wanaokwenda kuwekeza kwenye maeneo haya ya hifadhi ili tuweze kuona namna bora zaidi ya kurahisisha kuondoa urasimu, lakini pia kuwapunguzia walaji bei ya huduma hizi.

Name

Catherine Nyakao Ruge

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN aliuliza:- Kumekuwa na ongezeko kubwa sana la uwekezaji katika sekta ya utalii nchini:- Je, Serikali imejipanga vipi ili kukabiliana na ongezeko hilo?

Supplementary Question 2

MHE. CATHERINE N. RUGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi ya upendeleo. Napenda kuuliza swali la nyongeza kwa Waziri wa Maliasili na Utalii. Mkoa wa Mara ni kati ya mikoa iliyobarikiwa kuwa na vivutio vya utalii vikubwa ikiwemo Mbuga ya Serengeti kwa upande wa mashariki (Easten Corridor) lakini pia upande wa magharibi (Western Corridor). Je, ni nini mkakati wa Serikali kwa upande wa Western Corridor ambao imeonekana umesahaulika lakini una vivutio vingi vya utalii especially kwenye Ziwa Victoria lakini pia kuna visiwa? (Makofi)
Ina mpango gani wa kuendeleza utalii katika corridor ya Magharibi?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, historia huwa inaandikwa namna hii na mimi nakuwa ni Naibu Waziri wa kwanza kujibu swali la kwanza kutoka kwa Mbunge, Mheshimiwa Catherine Ruge. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nampongeza kwanza Mheshimiwa Mbunge na napenda kumkaribisha katika jitihada hizi za kuweza kuwahudumia wananchi. Kuhusu swali lake la nyongeza kwa ufupi kabisa. Western Corridor anayoizungumzia ikiwemo eneo linalopakana na Serengeti upande ule wa magharibi, lakini pia Ziwa Victoria pamoja na visiwa vingine vyote ambavyo Mkoa wa Mara ni sehemu yake. Haya ni maeneo ambayo tayari Serikali imeshaweka mipango thabiti kabisa ya kuyaboresha.
Mheshimiwa Spika, hasa kuhusiana na Serengeti yako malango ya kuingia Serengeti yaliyozoeleka, mengi yanatokea upande wa Mkoa wa Arusha, lakini tumekwishaangalia hili na sasa kutokea Mkoa wa Mara, lakini pia kutokea Mkoa wa Shinyanga, tunakwenda kuboresha mageti ili tuweze kuwaruhusu watalii waingie kutoka kwenye kona zote zilizopakana na Serengeti ili kuweza kuruhusu idadi kubwa zaidi ya watalii kuingia katika maeneo haya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge asiwe na wasiwasi, tuko mbioni kuboresha maeneo hayo na wakati wowote ule tunamkaribisha Wizarani kuja kuleta maoni kwa ajili ya kuboresha utalii. (Makofi)