Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Sixtus Raphael Mapunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Primary Question

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA aliuliza:- Moja kati ya changamoto zinazowakabili wakulima wa kahawa ni kodi na makato mengi:- Je, ni lini Serikali itazipiga marufuku kodi zote zinazomnyonya mkulima?

Supplementary Question 1

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri na yenye matumaini kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize swali moja la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa muda mrefu unaosemwa na Serikali, umesemwa kwa miaka mingi sana. Hata mwaka 2015, Rais wetu mpendwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli katika kampeni zake alisema hakuna zao lenye tozo na kodi za ajabu ambazo hazi-exist duniani kama zao la kahawa, alisema lina kodi 26. Mwaka jana ametoa kodi moja tu ya usindikaji wa kahawa dola 250, bado kuna kodi 25, hatuoni commitment ya Serikali kwenye hili. Mbona tumefanikiwa kwenye korosho mwaka jana imefuta kodi zote na wananchi wakulima wa korosho wanaishi vizuri? Naiomba Serikali iji-commit kwenye hili mwaka huu iondoshe hizo kodi zote kwa sababu haya matumaini tumeyachoka.

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba suala la tozo, kodi, limekuwa likizungumziwa kwa muda mrefu na ni kweli vilevile kwamba Mheshimiwa Rais wakati wa ziara yake ya kampeni ni moja kati ya masuala ambayo aliahidi kwamba atayafanyia kazi. Sisi kama Wizara tumeendelea kutekeleza sio katika zao la kahawa tu lakini katika mazao yote ya biashara.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Sixtus Mapunda kwamba tarehe 22 Mei, tutakuja na mapendekezo ya kufuta tozo mbalimbali katika mazao ya biashara. Katika hili nimuahidi kwamba tutavuka mategemeo yake. Siku hiyo ya tarehe 22 mimi mwenyewe nitahakikisha namwita aje Bungeni kusikiliza. Katika hili tutaleta, sisi tunasema mapinduzi makubwa, tutaondoa tozo nyingi sana sio katika kahawa pekee bali katika mazao yote ya biashara.

Name

John Wegesa Heche

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA aliuliza:- Moja kati ya changamoto zinazowakabili wakulima wa kahawa ni kodi na makato mengi:- Je, ni lini Serikali itazipiga marufuku kodi zote zinazomnyonya mkulima?

Supplementary Question 2

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Suala la kahawa kule kwetu kuna kata zaidi ya tano zinalima kahawa; Kata ya Mriba, Nyanungu, Itirio na maeneo mengine ya Tarime Mjini pia Kitale wanalima kahawa. Watu wa maeneo mengine wamefyeka kahawa zao kwa sababu wanaona ni kilimo kisichokuwa na tija. Mwenzangu amelalamikia kodi na tozo, ni kweli zipo, lakini kule kwetu nalalamikia bei. Ukichukua bei za kahawa zinazonunuliwa kwa mfano upande wa Kaskazini, japo bado zipo chini, ni tofauti na za Tarime na maeneo mengine ya kule Mara. Ukichukua bei zilizoko Kenya, sisi tuko mpakani, Kenya bei iko juu…
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Kenya mpakani bei inakuwa juu kuliko sisi. Sasa nauliza Serikali ni kwa vipi watu wengine wote bei zao zinakuwa tofauti na sisi? Ni kwa nini wasifanye bei hiyo ipande ili wakulima wale wasifyeke kahawa zao iwe ni kati ya zao ambalo linawapatia faida?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa Mheshimiwa Mbunge anavyosema kwamba nchi za jirani bei ya kahawa ni nzuri kuliko bei tuliyonayo nchini. Moja kati ya sababu zinazofanya bei yetu ya kahawa iwe chini ukilinganisha na nchi za jirani ni kwa sababu ya utitiri wa tozo na kodi ambazo zinafanya ile bei anayopata mkulima kuwa ndogo. Ndiyo maana nimesema mwaka huu tutapunguza tozo na kodi kuzidi mategemeo yenu kwa wakati wowote ule.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kodi hizi sio kwamba zina athari tu kwa bei ya zao hili kwa wakulima lakini zina athari katika mazingira ya ufanyaji biashara. Wawekezaji na wanunuzi wengi wa kahawa hawaji Tanzania kwa sababu kimsingi mazingira ya kufanya biashara ni magumu, ikisababishwa pamoja na mambo mengine na utitiri wa kodi na nyingine zinawagusa wao moja kwa moja. Kwa hiyo, tunapopunguza zitakuwa na faida sio tu ya kuongeza bei anayopata mkulima lakini vilevile kuwavutia wanunuzi wengi zaidi ili ushindani uwe mkubwa na hivyo bei kuongezeka. Naomba naye asubiri tarehe 22 ataona mapinduzi haya ambayo tunayazungumzia.

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Primary Question

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA aliuliza:- Moja kati ya changamoto zinazowakabili wakulima wa kahawa ni kodi na makato mengi:- Je, ni lini Serikali itazipiga marufuku kodi zote zinazomnyonya mkulima?

Supplementary Question 3

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, mazingira ya swali hili yanafanana kabisa na mazingira ya wakulima wa Wilaya ya Mbozi na hasa katika Jimbo la Vwawa. Kwa kuwa, moja ya gharama kubwa ambazo wakulima wa kahawa wanazipata ni pamoja na kusafirisha kahawa yao kupeleka kwenye mnada kule Kilimanjaro. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba Mnada wa Mloo unafunguliwa ili kupunguza ushuru na tozo mbalimbali ambazo zinawakabili wakulima wa zao la kahawa wa Wilaya ya Mbozi?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kabisa kwamba mnada mkubwa wa zao la kahawa upo Moshi. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba katika jitihada za Serikali za kuboresha mazingira ya zao la kahawa suala la minada na mahali panapofanyika ni moja kati ya masuala tunayofanyia kazi. Kwa hiyo, avute subira, nina hakika muda sio mrefu tutakuwa na suluhisho katika hili.