Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Othman Omar Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Gando

Primary Question

MHE. OTHMAN OMAR HAJI Aliuliza:- Moja kati ya kazi za Polisi ni ulinzi na usalama wa raia na mahali zao, uzoefu unaonesha kila zinapotokea kampeni za Uchaguzi Jeshi la Polisi hutumika kama Taasisi ya Chama Tawala hivyo husababisha ulinzi na usalama (hasa Wapinzani) kutoweka mikononi mwa Polisi:- Je, Serikali haioni kwamba inalitumia Jeshi la Polisi kwa lengo la kudhoofisha Upinzani na kurahisisha kukipatia ushindi Chama chake cha CCM?

Supplementary Question 1

MHE. OTHMAN OMAR HAJI:Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza madogo tu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya tarehe 20 Machi, 2016 ambapo vyombo vya dola vilikamilisha kusimamia zoezi la uchaguzi wa Zanzibar, ambao uliiweka madarakani Serikali
haramu inaongozwa na Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein jambo ambalo wakati huo palitokea tuhuma dhidi ya wafuasi wa CUF kwamba wanapita wakiharibu mali za wafuasi wa CCM, shutuma ambazo ziliwapelekea wafuasi wa CUF kukamatwa, kupigwa, kuwekwa mahabusu……
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na matokeo hayo ambayo yalitokea katika Kisiwa cha Pemba, katika Kisiwa cha Unguja maeneo ya Tumbatu kulitokea nyumba za wafuasi……
Mheshimiwa Naibu Spika, najenga hoja.
Nyumba za wafuasi wa CUF kuchomwa moto na wafuasi wa CCM, kwa kuthibitisha majibu ya Mheshimiwa Waziri Je, kwa nini wafuasi hawa walioshutumia na CUF katika Kisiwa cha Tumbatu, kwa nini mpaka leo hawajakamatwa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, inapotokea Wapinzani wanataka kufanya mikutano, Jeshi la Polisi wanasema wana taarifa za kiintelijensia kwamba hakuna usalama. CCM wanapofanya mikutano yao, Jeshi la Polisi linakusanyika pote ili kulinda mikutano hiyo. Je, kwa nini Jeshi la Polisi linailinda mikutano ya CCM lakini pale ambapo Upinzani wanafanya mikutano hawataki kuilinda?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nataka nimthibitishie pamoja na Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwa ujumla kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein ni halali ambayo imechaguliwa na wananchi kupitia Uchaguzi Mkuu halali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kauli kama hizi katika Bunge lako Tukufu ambazo zinapotosha umma siyo tu kupotosha na kudhalilisha Serikali halali na maamuzi sahihi ya wananchi ziendelee kupingwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili anauliza swali kwamba baada ya uchaguzi kuna wafuasi wa CUF ambao walishutumiwa kwa tuhuma mbalimbali ambao walikamatwa na akatolea mfano wa Kisiwa cha Tumbatu kuna wafuasi ambao hawakuchukuliwa hatua nadhani alikusudia wa vyama vingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya Uchaguzi Mkuu baadhi ya Vyama vya Upinzani ikiwemo chama chake, viongozi walijitokeza kuhamasisha wananchi kufanya mambo ambayo yanakiuka sheria za nchi yetu. Kuna matukio mbalimbali ambayo yamejitokeza ikiwemo kuchomwa moto kwa nyumba, kuchomwa mashamba, kurusha mabomu ikiwemo nyumba ya Kamishna Mkuu wa Polisi wa Zanzibar ambayo kwa uchunguzi uliofanyika mpaka sasa hivi tunavyozungumza watu ambao wamekamatwa kuhusika na urushaji bomu katika nyumba ya Kamishna ni Viongozi Waandamizi wa Chama cha CUF. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Polisi imeshakamilisha uchunguzi wake na suala lipo kwa DPP na linahitajika kupelekwa Mahakamani ili hatua za kisheria zichukuliwe. Kwa hiyo, nataka kusema kwamba, watu hawa ambao wamefanya matukio ya ukiukwaji wa sheria wapo wengi, mpaka sasa hivi zaidi ya watu 24 wameshapelekwa katika vyombo vya sheria na wengine wapo katika hatua mbalimbali za uchunguzi. Kwa hiyo, siyo sahihi kwamba Jeshi la Polisi linafumbia macho uvunjifu wa sheria. Iwe Tumbaktu, Pemba, Unguja ama sehemu yoyote ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yeyote ambaye anakiuka sheria za nchi atachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili ni kuhusiana na hoja ya kwamba mikutano ya CCM inaruhusiwa na Polisi lakini mikutano ya CUF hairuhusiwi. Naomba nikuthibitishie pamoja na Wabunge na wananchi wote kwa ujumla, kwamba hakuna ubaguzi kama nilivyojibu katika swali langu la msingi katika kuhakikisha kwamba Jeshi la Polisi linafanya kazi yake kwa mujibu wa sheria, halibagui chama cha siasa. Tunapozungumza sasa hivi mikutano ya hadhara imezuiliwa kwa vyama vyote ikiwemo Chama cha Mapinduzi. Hakuna sehemu yoyote ambayo Chama cha Mapinduzi kinaruhusu mikutano ya hadhara zaidi ya Waheshimiwa Wabunge waliochaguliwa katika Majimbo yao. Mikutano ya ndani inaruhusiwa kwa vyama vyote na haijawahi kuzuiliwa kwa chama chochote. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Mbunge kama ana uthibitisho wa mikutano halali ya chama chake ambayo imezuiliwa basi atuletee taarifa ili tufuatilie tuweze kuchukua hatua stahiki.

Name

Martha Jachi Umbulla

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. OTHMAN OMAR HAJI Aliuliza:- Moja kati ya kazi za Polisi ni ulinzi na usalama wa raia na mahali zao, uzoefu unaonesha kila zinapotokea kampeni za Uchaguzi Jeshi la Polisi hutumika kama Taasisi ya Chama Tawala hivyo husababisha ulinzi na usalama (hasa Wapinzani) kutoweka mikononi mwa Polisi:- Je, Serikali haioni kwamba inalitumia Jeshi la Polisi kwa lengo la kudhoofisha Upinzani na kurahisisha kukipatia ushindi Chama chake cha CCM?

Supplementary Question 2

MHE. MARTHA J. UMBULLA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mara nyingi Jeshi la Polisi linapohitajika kuwahi kwenye matukio ya kuwalinda raia na mali zao wanapata shida sana ya kuwahi kwenye matukio hayo kutokana na matatizo waliyonayo kwenye magari yao, magari mengi yanakosa matairi, mafuta na ni mabovu, tatizo hilo ni karibia nchi nzima lakini nazungumzia katika Mkoa wangu wa Manyara. Je, Serikali ina mpango gani mahsusi kabisa wa kuhakikisha kwamba magari ya Jeshi la Polisi yanakuwa na vifaa hivyo muhimu ili kuhakikisha kwamba ulinzi wa raia na mali zao unakuwa wa uhakika?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri kwamba tuna changamoto ya upungufu wa vitendea kazi kwa ujumla katika Jeshi letu la Polisi na hii inatokana na ufinyu wa bajeti tulionao. Tutajitahidi katika bajeti ya mwaka huu kuongeza fedha kwa ajili ya matumizi kwa Jeshi la Polisi ili tuweze kukidhi mahitaji hayo, siyo tu kwa Mkoa wa Manyara pia kwa nchi nzima kwa ujumla wake.

Name

Peter Ambrose Lijualikali

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Kilombero

Primary Question

MHE. OTHMAN OMAR HAJI Aliuliza:- Moja kati ya kazi za Polisi ni ulinzi na usalama wa raia na mahali zao, uzoefu unaonesha kila zinapotokea kampeni za Uchaguzi Jeshi la Polisi hutumika kama Taasisi ya Chama Tawala hivyo husababisha ulinzi na usalama (hasa Wapinzani) kutoweka mikononi mwa Polisi:- Je, Serikali haioni kwamba inalitumia Jeshi la Polisi kwa lengo la kudhoofisha Upinzani na kurahisisha kukipatia ushindi Chama chake cha CCM?

Supplementary Question 3

MHE. PETER A. P. LIJUALIKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Juzi hapa tumetoka kwenye Uchaguzi Mdogo Ifakara tarehe 23 ambapo kwanza Mwandishi wa Mwananchi Juma Mtanda alitekwa na wanachama na wafuasi wa CCM, wakampora iPad, simu na Kamera, akaenda Polisi akalalamika. Matokeo yake Polisi wakawatafuta watu wa CCM na wakamrudishia. Maana yake ni kwamba Polisi wanawajua wanaofanya uhalifu huu, mpaka leo hakuna ambacho kimefanyika, hakuna kesi wala chochote, hiyo ni moja. (Makofi)
Pili, kwenye uchaguzi ule kuna Askari WP Huruma alipigwa na jiwe na tofali akapasuka, ameshonwa nyuzi tano na amepigwa na wanachama wa CCM, lakini Polisi wanamuachia anatembea, anafanya chochote taarifa ipo. Namwomba Mheshimiwa Waziri anaiambie kama CCM wanaruhusiwa kufanya vurugu mpaka kujeruhi Askari wetu halafu wakaachiwa huru?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Lijualikali anazungumzia tuhuma za wanachama wa CCM kuwajeruhi Askari Polisi, pia kupora Waandishi wa Habari. Kwanza kabisa nashindwa kulijibu swali hili moja kwa moja kwa sababu unapozungumzia tuhuma kwamba hawa ni wafuasi wa chama fulani inahitaji uthibitisho.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoweza kusema…

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa
Naibu Spika, ninachoweza kusema ni kwamba uhalifu wa aina yoyote utakaofanywa na mtu yoyote wa chama chochote, dhidi ya raia yoyote ikiwemo Waandishi wa Habari na Jeshi la Polisi ndiyo kabisa. Jeshi la Polisi liko hapa kwa ajili ya kulinda usalama wetu, hatutakubali kamwe mtu yeyote acheze na Jeshi la Polisi na siyo tu Jeshi la Polisi hata Waandishi wa Habari wamekuwa wakifanya kazi vizuri sana ya kuelimisha jamii na kutoa taarifa nzuri kwa umma. Hatuwezi kukubali Waandishi wa Habari au Jeshi la Polisi kufanyiwa matukio yoyote ya kihalifu na raia mwingine yeyote, tutachukua hatua kali za kisheria. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Mbunge kama ana ushahidi wa hilo jambo alete, lakini siwezi nikasema hapa kwamba chama fulani kimefanya jambo fulani bila uthibitisho.

Name

Abdallah Hamis Ulega

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkuranga

Primary Question

MHE. OTHMAN OMAR HAJI Aliuliza:- Moja kati ya kazi za Polisi ni ulinzi na usalama wa raia na mahali zao, uzoefu unaonesha kila zinapotokea kampeni za Uchaguzi Jeshi la Polisi hutumika kama Taasisi ya Chama Tawala hivyo husababisha ulinzi na usalama (hasa Wapinzani) kutoweka mikononi mwa Polisi:- Je, Serikali haioni kwamba inalitumia Jeshi la Polisi kwa lengo la kudhoofisha Upinzani na kurahisisha kukipatia ushindi Chama chake cha CCM?

Supplementary Question 4

MHE. ABDALLAH H. ULEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali fupi la nyongeza. Kwa niaba ya wananchi wa Wilaya ya Mkuranga, Kibiti na Rufiji ningeomba Mheshimiwa Naibu Waziri aniambie sawa na jibu lake la msingi ya kwamba kazi mojawapo ya Polisi ni ulinzi wa raia na mali zao. Je, Serikali inawahakikishiaje wananchi wa Wilaya hii ya Mkuranga, Kibiti na Rufiji juu ya usalama wao na wa mali zao kipindi hiki cha operesheni ya kutafuta wahalifu ili waweze kufanya kazi zao kwa uhuru bila ya kubigudhiwa? Ahsante.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Mkuranga, Kibiti na Rufiji kama ambavyo kila mmoja anafahamu kwamba limekuwa na changamoto ya matukio mbalimbali ya uvunjifu wa amani ambapo mpaka sasa hivi kuna raia wengi wamepoteza maisha, pia mnakumbuka hivi karibuni Askari wetu takribani nane walipoteza maisha kwa mpigo. Mimi binafsi nilifanya ziara katika maeneo hayo ambayo nimeyazungumza na kufanya mkutano wa hadhara na wananchi. Katika mambo ambayo tumeyazungumza alifanya ziara Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi; kuna mambo makubwa matatu ambayo tumeyasisitiza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, tumeendelea kuwasisitiza wananchi kulisaidia Jeshi la Polisi kutoa taarifa juu ya matukio ya uhalifu na wahalifu ambao wanawashuku katika maeneo yao ili kazi ya Jeshi la Polisi iweze kuwa rahisi. Pili, tumeendelea kuwahakikishia wananchi wa Mkoa huo kwamba Serikali itafanya kila linalowezekana kuhakikisha kwamba kwamba amani na usalama wa wananchi wa maeneo hayo linakuwa ni jambo la kipaumbele. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kufanya hivyo ni lazima Jeshi la Polisi liwe karibu na wananchi vilevile, wananchi wawe karibu na Jeshi la Polisi na Jeshi la Polisi liwe karibu na wananchi, kwa maana ya kujenga mahusiano mazuri kati ya pande hizi mbili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kukiomba kwa Mheshimiwa Mbunge akiwa Mwakilishi wa wananchi wa Jimbo la Mkuranga pamoja na Wabunge wengine wa maeneo yale, kuhakikisha kwamba wanaendelea kuwaelimisha wananchi waendelee kuwa karibu na Jeshi la Polisi, kuwasaidia kupata taarifa mbalimbali za uhalifu wakati huu ambapo Jeshi la Polisi na Serikali kwa ujumla inafanya jitihada kuhakikisha kwamba maisha ya wananchi wa maeneo hayo yanalindwa pamoja na mali zao, pamoja na maisha, usalama wa Askari wenyewe ambao wanalinda usalama huo wa raia.