Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. Christine Gabriel Ishengoma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA Aliuliza:- Serikali ina mpango mzuri wa kuanzisha mfumo mpya wa kutoa ruzuku za pembejeo kwa wakulima ambao utawanufaisha zaidi. Je, ni lini mfumo huo mpya utaanza kutumika ili wakulima waweze kupata pembejeo kwa wakati wote?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri na Mheshimiwa Naibu Waziri, ninayo maswali mawili ya ngongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 75 ya wakulima hapa Tanzania wakiwemo wakulima wa Mkoa wa Morogoro wanategemea kilimo kwenye uchumi wao. Serikali ina mkakati mzuri wa kupunguza bei kwenye mbolea kusudi iweze kuwa nafuu kwa wakulima. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuanzisha viwanda vya mbolea hapa nchini sambamba na Kiwanda cha Minjingu na Kiwanda cha Mtwara kinachotegea kujengwa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mbolea hasa ya DAP pamoja na UREA ni mbolea ambayo zinatumika sana kwenye kilimo chetu, DAP ikiwa ni mbolea ya kupandia na UREA ikiwa ni mbolea ya kukuzia. Hapa nchini tuna mbolea ya Minjingu ambayo inazalishwa Manyara.
Je, mbona haijawekwa kwenye mkakati huu kusudi wananchi waweze kupata hamasa ya kutumia mbolea ya Minjingu? Ahsante.

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la Serikali kuanzisha viwanda, ni kweli kabisa kwamba Serikali ya Awamu ya Tano moja kati ya mikakati yake ya kuendeleza uchumi ni kuhakikisha kwamba kunakuwa na viwanda nchini. Kwa hiyo, Serikali imekuwa ikihimiza na kuweka mazingira wezeshi ili sekta binafsi na wadau wengine waweze kuanzisha viwanda nchini. Kwa sasa Serikali iko katika mikakati ya kushirikiana na sekta binafsi kuanzisha kiwanda cha mbolea Mkoani Lindi kwa kutumia gesi; na utaratibu huo ukikamilika, tunaamini kwamba mahitaji mengi ya mbolea yatakuwa yamepata suluhu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna kiwanda cha mbolea kinajengwa Kibaha, kwa hiyo, tunaamini kwamba kadiri miaka inavyokwenda, tutakuwa tunazalisha mbolea zetu humu nchini, kuliko kuagiza ambayo inatusababishia kuwa na gharama kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kwamba katika utaratibu wa bulk procument (uagizaji wa mkupuo) tunaanza na mbolea za DAP na UREA, lakini baadaye tutaingia kwenye mbolea nyingine kama NPK na mbolea nyingine ambazo zinatumika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kwa nini hatujaweka mbolea ya Minjingu katika utaratibu huu? Ukweli wa mambo ni kwamba tunapozungumzia kuhusu uagizwaji wa mkupuo, tunazungumzia kuhusu mbolea kutoka nje.
Hata hivyo, bado kuna fursa ya kuendelea kuhimiza kiwanda cha Minjingu kiongeze uzalishaji, kwa sababu kwa sasa uwezo wao kwa mwaka ni tani 50,000 wakati mahitaji yetu ya mbolea ya aina hiyo kwa mwaka ni zaidi ya tani nusu milioni. Kwa hiyo, vilevile kuna suala la uwezo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali iko tayari kushirikiana na Minjingu waongeze uzalishaji ili mbolea yao iweze kutumika kwa wingi zaidi.