Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Pauline Philipo Gekul

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. PAULINE P. GEKUL Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itafanya tathmini ya miradi ya maji ya visima kumi katika vijiji inayofadhiliwa na Benki ya Dunia?

Supplementary Question 1

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri alifanya ziara katika Jimbo la Babati Mjini na akabaini kero za maji. Kwa hiyo, haya nitakayoyauliza anayafahamu vema na atanipa majibu.
Swali la kwanza, kwa kuwa mradi wa maji wa kijiji cha Malangi umechukua muda mrefu sana na kwa kuwa mradi huu ulitelekezwa na mkandarasi wa awali, na kwa kuwa mradi huu sasa thamani yake siyo shilingi milioni 400 ni shilingi milioni 600.
Je, Serikali iko tayari kutupatia fedha hizo shilingi milioni 600 kwa ajili ya kukamilisha mradi wa maji Malangi ili wananchi hao wapate maji kwa muda mrefu ambao walikuwa wameyakosa?
Swali la pili, kwa kuwa mradi wa maji wa kijiji cha Nakwa wenye thamani ya shilingi milioni 801 umekuwa na changamoto nyingi, mabomba yapo juu hayajawekwa chini, yamekuwa yakipasuka wakati huu ambapo mradi unafanyiwa majaribio, na kwa kuwa vijana ambao pia walichimba mitaro kwa ajili ya kulaza yale mabomba hawajalipwa na mkandarasi ambaye anafanya kazi hiyo. Ilikuwa vijana hao walipwe shilingi 4,000 kwa kila mita wamelipwa shilingi 700.
Je, Naibu Waziri Wizara yako iko tayari kuunda timu ya wataalam kwenda kukagua mradi wa kijiji cha Nakwa ambao umekuwa ukisumbua wananchi hawa kwa mradi huo kuchakachuliwa?

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni kweli nilitembelea Babati na hizi changamoto tukiwa pamoja na Mheshimiwa Mbunge tuliziona na tulizijadili na kutoa maekelezo. Nikuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa utaratibu tuliouweka kwamba kila Halmashauri inapata bajeti. Kwa hiyo, hii fedha kwenye mradi wa Malangi tutahakikisha sasa unasimamiwa vizuri na pale nilitoa maelekezo kwamba Waheshimiwa Wabunge mnapoona inasua sua kwenye Halmashauri kama Mamlaka ya Maji ya Mkoa ambayo ipo chini ya Wizara ya Maji basi ni lazima tushirikiane katika utaalam ili kuhakikisha kwamba miradi inatekelezwa katika viwango vinavyotakiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tumetenga fedha katika mwaka wa fedha unaokuja. Ile bakaa ya upungufu iliyobaki itaongezwa kuhakikisha kwamba mradi huu unakamilika. (Makofi) Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni kijiji cha Nakwa, Mheshimiwa Mbunge mwenyewe ni shahidi unakumbuka kwanza tulitengeneza utaratibu kwamba kama mradi wa maji uliotekelezwa na Halmashauri uko karibu na Mamlaka ya Maji ya Mkoa, wakati wanapotekeleza ule mradi inabidi washirikiane ili kuhakikisha kwamba vile viwango vinavyotakiwa katika mradi viweze kufikiwa na hasa kwa kuwa mara nyingi miradi kama hiyo kwa sababu mamlaka za maji zina maji mengi, kumekuwa na tabia ya Wakurugenzi wanaomba mradi huo uunganishwe kwenye Mamlaka ya Maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala hili pale tuliagiza kwamba Mkurugenzi wa Maji wa Babati sasa ashirikiane na Halmashauri ili kuweza kuhakikisha kwamba huu mradi ambao haukutengenezwa vile inavyotakiwa basi uhakikishe kwamba kwanza wanautekeleza katika viwango vinavyotakiwa. Pia nakubaliana na wewe kwamba Serikali italiangalia hili ili kuhakikisha wale walioharibu hatua stahiki zinachukuliwa.

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Primary Question

MHE. PAULINE P. GEKUL Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itafanya tathmini ya miradi ya maji ya visima kumi katika vijiji inayofadhiliwa na Benki ya Dunia?

Supplementary Question 2

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Geita na Kasamwa kuna shida kubwa sana ya maji na Mheshimiwa Waziri tangu mwaka jana alisema wamepata pesa kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya maji katika Mji wa Geita. Je, ni lini sasa mradi huo wa maji utatekelezwa?

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Geita una miradi miwili, mradi mmoja ni ule ambao tunashirikiana na GGM na umeshatekelezwa mpaka tukafikia asilimia 30 tayari Mji wa Geita unapata maji. Pia unapata kutokana na ufadhili unaotokana na uboreshaji wa mazingira wa Ziwa Victoria.
Mheshimiwa Kanyasu, tayari katika mkopo tuliopata wa milioni 500 kutoka Serikali ya India, sehemu ya fedha hiyo inatarajiwa kuboresha maji katika Mji wa Geita. Sasa hivi tunaendelea vizuri kwa ajili ya kumpata consultant atakayefanya mapitio na kuandaa tender document baada ya hapo kutangaza tenda ili tuweze kupata sasa maji ya uhakika kwa Mji wa Geita.

Name

Hawa Subira Mwaifunga

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. PAULINE P. GEKUL Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itafanya tathmini ya miradi ya maji ya visima kumi katika vijiji inayofadhiliwa na Benki ya Dunia?

Supplementary Question 3

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona.
Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Tabora Mjini lina kata 29, katika kata hizo kata 11 hazipati maji kabisa. Ni tatizo linalotokana na Serikali kudaiwa kiasi cha shilingi bilioni mbili na mkandarasi. Je, ni lini Serikali italipa pesa hizo ili hizi kata 11 ziweze kupatiwa maji?

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza bahati nzuri kwenye sherehe ya Pasaka nilienda Jimboni kwangu nimepita Tabora, nimekuta Mamlaka yetu ya Tabora imenunua mabomba mengi kuhakikisha kwamba katika hizi kata zilizosalia ni kata tisa ambazo zimebaki hazipati huduma ya maji mjini. Kwa hiyo, kata moja tayari inawekewa miundombinu ya maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia mradi ambao tarehe 22 Mheshimiwa Waziri anakwenda kushuhudia kusaini mikataba ya mradi wa kutoa maji Solya kupeleka Nzega, Igunga na Tabora, kata zote zilizobaki sasa zitapata huduma ya maji kutoka kwenye huu mradi mpya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge baada ya mwaka mmoja au miwili Mji wa Tabora tutakuwa tumemaliza kabisa matatizo ya maji.