Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:- Mnada wa Magena Wilayani Tarime ulifungwa na kusababisha adha kubwa kwa Halmashauri ya Mji wa Tarime kupoteza mapato ya ushuru wa mifugo inayouzwa nchi jirani ya Kenya, sambamba na ukosefu wa ajira kwa wakazi wa Tarime:- Je, Mnada huu wa Magena utafunguliwa lini ili kutoa fursa za ajira na kuokoa mapato mengi yanayopotea kwa sasa?

Supplementary Question 1

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa masikitiko makubwa sana nimefedheheshwa na majibu ya Wizara kwa sababu amenijibu kuhusiana na Halmashauri ya Wilaya ya Tarime na mimi nimeuliza kuhusiana na Halmashauri ya Mji wa Tarime ambapo Mnada wa Magena upo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali yangu, kwa kuwa katika majibu yao ambayo hayajakidhi wametamka dhahiri kwamba walifunga mnada huu kwa sababu za wizi wa ng’ombe na usalama. Kwa kuwa Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi imeanzisha Kanda Maalum ya Tarime - Rorya ambapo hivi sasa usalama umeimarika ingawa bado wanaongelea suala la wizi. Vilevile wameainisha kwenye majibu yao kwamba 1996 tu waliweza kupata Sh.260,000,000 na sasa hivi 2015 wanapata Sh.212,000,000, hawaoni kuwa Serikali inapoteza mapato mengi sana kwa kutokuanzisha ule mnada ambao ulikuwa umeshajengwa ambapo kwa sasa hivi unaweza kupata zaidi ya Sh.1,000,000,000? Hilo ni swali la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni dhahiri kabisa na hata kwenye majibu yao wamesema Mnada wa Mtana, Kewenja, Nyamwaga na Chemakolele ipo katika Halmashauri ya Wilaya na ni dhahiri kabisa pia kwamba huu mnada ulihamishwa kwa sababu za kisiasa kwa sababu huwezi ukasema Kirumi ipo mpakani na Kenya. Napenda kujua sasa ni lini Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi itaacha siasa iweze kufanya mambo ya kimaendeleo na Mnada wa Magena ufunguliwe ili wananchi wa Tarime wafaidike? ((Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kupoteza mapato, ni kweli kabisa kuna changomoto kwamba Serikali ingeweza kupata mapato mengi zaidi kwa kuendelea na mnada ule. Hata hivyo, katika hali iliyopelekea mpaka mnada husika ukafungwa, ukweli wa mambo ni kwamba hata kukusanya mapato ilikuwa haiwezekani. Kwa sababu Serikali ina jukumu la msingi la kulinda amani na usalama, kwa kweli ilikuwa haiwezi kuendelea kuruhusu mnada ule utumike wa sababu watu mali zao zilikuwa zinapotea na walikuwa wanatishiwa maisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi, hakuna shughuli za kiuchumi ambazo zilikuwa zinaenda kama ilivyotarajiwa. Kwa hiyo, pamoja na kwamba ingeweza kupata mapato lakini haikuwezekana kuendelea kuwa na shughuli yoyote katika hali ambayo si salama. Hata yeye mwenyewe amekiri kwamba kulikuwa na hali ya kutishia amani na usalama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mnada husika kufungwa na mwingine kuanzishwa kisiasa, nimhakikishie tu Mheshimiwa Matiko kwamba kilichopelekea mnada huu kufungwa na mwingine kuanzishwa siyo sababu za kisiasa ni kwa sababu ulinzi na usalama wa wananchi wa Tarime ulikuwa ni wa muhimu zaidi. Vilevile nimhakikishie tu kwamba kwa hali ya sasa mnada ule mpya unafanya kazi kama ile iliyokuwa inafanywa na mnada wa awali. Cha maana ni wananchi kupata fursa ya kuuza mifugo yao kwenda nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama kuna mnada ambao unafanya kazi ileile vizuri zaidi na hauhatarishi usalama, kwa vyovyote vile Serikali itachukua uamuzi wa kuhakikisha kwamba mnada huo unaendelea badala ya kufikiri kwamba ni lazima kurudi kwenye mnada ambao kwa kweli uendeshaji wake ulikuwa unatishia ulinzi na usalama.

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:- Mnada wa Magena Wilayani Tarime ulifungwa na kusababisha adha kubwa kwa Halmashauri ya Mji wa Tarime kupoteza mapato ya ushuru wa mifugo inayouzwa nchi jirani ya Kenya, sambamba na ukosefu wa ajira kwa wakazi wa Tarime:- Je, Mnada huu wa Magena utafunguliwa lini ili kutoa fursa za ajira na kuokoa mapato mengi yanayopotea kwa sasa?

Supplementary Question 2

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa Mnada wa Magena katika Mji wa Tarime unafanana na mnada ambao unaitwa Mnada wa Kimataifa wa Pugu lakini ukifika hakuna mazingira yoyote ya kimataifa ambayo unaweza ukaonyesha. Ng’ombe wote wanaofugwa mikoani mimi katika Jimbo la Ukonga kule Pugu ndiyo nawapokea na nawalisha watu wa Dar es Salaam. Naomba nijue, ni lini sasa Wizara hii itahakikisha jina la Mnada wa Kimataifa wa Pugu linasadifu na mazingira ya Pugu kwa maana ya malambo, umeme na huduma zingine? (Makofi)

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mnada wa Magena ni Mnada wa Mpakani wakati Mnada wa Pugu ni Mnada wa Upili, kuna tofauti kubwa. Hata hivyo, naungana naye kukiri kwamba kuna changomoto nyingi ambazo zimejitokeza katika uendeshaji wa Mnada wa Pugu. Bado kuna fursa kubwa ya kuufanya mnada ule uwe na hadhi nzuri zaidi kuliko ilivyo sasa. Nimhakikishie tu kwamba tayari hatua zinachukuliwa ili kuboresha huduma katika Mnada wa Pugu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe baada ya kupata uteuzi wa Mheshimiwa Rais, nilikwenda kutembelea Mnada wa Pugu na kuangalia hali ilivyo na tayari tumetoa maelekezo hatua mahsusi zichukuliwe ili kuboresha huduma pale ikiwa ni pamoja na huduma za maji na kuimarisha utaratibu wa kukusanya mapato. Kwa sasa karibuni Mnada wa Pugu utakuwa unatuma mfumo wa kukusanya mapato wa kielektroniki. Hata Mheshimiwa Waziri mwenyewe ameshatembelea Pugu. Kwa hiyo, nimhakikishie tu kwamba baada ya muda Mnada wa Pugu utaendeshwa katika hali ambayo ni nzuri zaidi ili kuweza kuchangia katika pato la Taifa.