Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:- Zao la pamba ndilo zao kuu katika Wilaya ya Bunda:- (a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwapatia zao mbadala wakulima wa zao la pamba, baada ya zao hili kuelekea kutokomea kutokana na matatizo ya bei ndogo isiyokidhi mahitaji ya uzalishaji wake? (b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza uzalishaji wa zao la pamba hasa ikizingatiwa kuwa Wilaya ya Bunda yenye majimbo matatu inategemea viwanda vya pamba katika mapato na ajira?

Supplementary Question 1

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, napenda kuuliza maswali ya nyongeza mawili kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, tatizo la upatikanaji wa
pembejeo kwa zao la pamba ni la muda mrefu sana karibu miaka 17 au 20. Ni lini sasa Serikali itakuwa na mikakati maalum ya kumaliza tatizo hili la pembejeo kwa wakulima wa pamba kwa sababu limekuwa sugu kwa muda mrefu?
Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni muda mrefu sana Serikali tumekuwa tukipandisha bei ya pamba kwa kutegemea soko la dunia. Ni lini sasa Serikali itatengeneza mkakati wa kupata bei ya wakulima wa pamba kwa kutegemea soko la ndani?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuchukua hatua mbalimbali ili kuboresha upatikanaji wa pembejeo za pamba. Hatua mojawapo ambayo imeshafanyika ni kuanzishwa kwa Mfuko Maalum wa Wakfu wa Pamba (CDTF), ambao kazi yake kubwa ni kugawa na kuhakikisha pembejeo zinapatikana kwa bei nafuu kwa wakulima wa pamba, kazi ambayo tayari imekuwa ikiendelea kwa miaka kadhaa sasa.
Mheshimiwa Spika, lakini vilevile Serikali inaendelea na mpango wa kuvifufua na kuboresha utendaji wa vyama vya ushirika ili viweze kusimamia upatikanaji wa pembejeo katika maeneo hayo. Jitihada hizi zinahusisha kwa mfano kufufua Chama cha Ushirika cha Nyanza ili kiweze kufanya kazi kuwasaidia wakulima wa pamba lakini vilevile vyama vingine kama SHIRECU, navyo vilevile kazi ya kuvifufua
inaendelea.
Mheshimiwa Spika, kuhusiana na namna gani Serikali inaendelea kuboresha soko la ndani, napenda kumtaarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba, mkakati tulionao kwa sasa
ni ule wa mwaka 2016-2020 wa kujaribu kuhakikisha tunaboresha mnyororo mzima wa thamani kutoka kwenye pamba hadi kufikia kwenye nguo. Katika mkakati huo, Serikali
inahakikisha kwamba tunajenga viwanda na kuhamasisha ujenzi wa viwanda ndani ili nguvu kubwa isielekezwe tena katika kutafuta soko la nje bali kutumia soko la ndani ambalo tunaamini tunalo. Kwa sababu kwa idadi ya Watanzania
iliyopo kama tutaweza kutengeneza nguo ambazo zitatumika ndani, tunaamini kwamba bei ya pamba itaendelea kuimarika.

Name

Munde Abdallah Tambwe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:- Zao la pamba ndilo zao kuu katika Wilaya ya Bunda:- (a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwapatia zao mbadala wakulima wa zao la pamba, baada ya zao hili kuelekea kutokomea kutokana na matatizo ya bei ndogo isiyokidhi mahitaji ya uzalishaji wake? (b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza uzalishaji wa zao la pamba hasa ikizingatiwa kuwa Wilaya ya Bunda yenye majimbo matatu inategemea viwanda vya pamba katika mapato na ajira?

Supplementary Question 2

MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa, zao la pamba linafanana kabisa na matatizo ya zao kubwa la tumbaku la Mkoa wa Tabora; na
kwa kuwa, Mkoa wetu wa Tabora unategemea sana zao la tumbaku. Zao la tumbaku limekuwa na tozo kuanzia 19 mpaka 38 zinazomuumiza mkulima wa tumbaku na kusababisha mkulima huyu faida yake yote kwenda kwenye matozo 38. Je, Serikali ina mpango mkakati gani wa kuhakikisha inapunguza tozo hizi ili mkulima wa tumbaku apate faida kama ilivyopunguza tozo kwenye kilimo cha korosho?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI:
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, kati ya changamoto ambazo wakulima wa mazao hapa nchini wanapata ni tozo nyingi ambazo zinaendelea kuongeza changamoto kubwa
katika uendeshaji wa kilimo. Namwomba Mheshimiwa Mbunge asubiri kusikia hotuba ya bajeti yetu kwa sababu mwaka huu wa fedha unaokuja, Wizara imeamua kuondoa karibu nusu ya tozo zote ambazo ziko kwenye mazao.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sitaki kuwahi kuanza kueleza yaliyoko kwenye hotuba yetu ya bajeti, lakini nimweleze tu kwamba Serikali tayari ilishatambua changamoto hiyo; viongozi wetu wakuu, Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu kila wakati wamesisitiza kwamba tuondoe tozo hizo. Kwa
sasa Wizara imeondoa tozo kwa 50% lakini kama
ninavyosema tukija na maelezo yetu ya bajeti ataona ni tozo gani zimepungua.
Mheshimiwa Spika, vilevile Mheshimiwa Mbunge
atakumbuka kwamba, hivi karibuni katika jitihada za kuondoa changamoto zilizopo kwenye zao la tumbaku (Tabora), Mheshimiwa Waziri Mkuu alienda kule na anajua yaliyotokea kule. Sasa changamoto ya chama kikubwa cha WETCU kuweza kuhudumia vizuri wakulima tayari
inashughulikiwa pamoja na mambo mengine kwa kugawa iwe ni vyama viwili lakini vilevile ubadhirifu ambao umefanyika tayari wahusika wameshachukuliwa hatua.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kimsingi kuna mikakati mingi ambayo inaendelea ya kuhakikisha kwamba tunaboresha zao la tumbaku. Vilevile nimfahamishe Mheshimiwa Mbunge kwamba Jumamosi hii tumeitisha Mkutano wa Wadau wa Tumbaku na nachukua nafasi hii kumkaribisha tarehe 7 kwenye huo mkutano ili aangalie ni
mikakati gani mbayo tumeweka. Nashukuru sana.